2013-10-18 09:00:57

Rais Mahmoud Abbas akutana na kuzungumza na Papa mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko, Alhamisi tarehe 17 Oktoba 2013 amekutana na kufanya mazungumzo na Bwana Mahmoud Abbas kiongozi wa Wapalestina mjini Vatican. Baba Mtakatifu amewataka Wapalestina na Waisraeli kufanya maamuzi magumu kwa ajili ya kulinda na kudumisha amani itakayoungwa mkono na Jumuiya ya Kimataifa.

Bwana Mahmoud pamoja na ujumbe wake alikutana na kuzungumza pia na Askofu mkuu Dominique Mambert, Katibu mkuu wa mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa mjini Vatican.

Katika mazungumzo kati ya Baba Mtakatifu Francisko na mgeni wake, kwa pamoja wamegusia hali ya Mashariki ya kati na kwa namna ya pekee wamekazia umuhimu wa kuendeleza majadiliano kati ya Israel na Palestina. Pande hizi mbili zimeonesha matumaini kwamba, suluhu ya amani inaweza kupatikana na hatimaye, amani ya kudumu kuweza kutawala kati ya mataifa haya mawili; amani itakayoungwa mkono na Jumuiya ya Kimataifa.

Kwa pamoja viongozi hawa wawili wameguswa na hali tete nchini Syria na kwamba, wanatumaini kuona kuwa wadau wanaohusika na mgogoro wa Syria wataanzisha mchakato wa majadiliano na upatanisho ili kung'oa mzizi wa vita mapema iwezekanavyo. Wameridhika na uhusiano baina ya pande hizi mbili na kwamba, wataendelea kufanya upembuzi yakinifu ili kuwa na makubaliano mapana zaidi katika maisha na utume wa Kanisa huko Palestina.

Baba Mtakatifu na mgeni wake, wamezungumzia pia kuhusu hali ya Jumuiya za Wakristo katika eneo la Wapalestina na Mashariki ya Kati katika ujumla wake. Wameguswa na mchango wa hali na mali unaotolewa na Wakristo kwa ajili ya mafao ya wengi.







All the contents on this site are copyrighted ©.