Tanzania na China watiliana mkwaju wa mikataba mitano!
Serikali ya Tanzania imeasaini mikataba ya makubaliano (MoUs) mitano ambayo itasadia
kutoa fursa za biashara, mafunzo na masuala ya sayansi na teknolojia kwa Watanzania.
Mikataba
hiyo imetiwa saini Alhamisi, Oktoba 17, 2013 mbele ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda na
Waziri Mkuu wa China, Mhe. Li Keqiang mara baada ya viongozi hao kufanya mazungumzo
rasmi ya Kiserikali jijini Beijing, China.
Mikataba hiyo ni Mkataba wa Ushirikiano
baina ya Tanzania na China kwenye masuala ya Sayansi na Teknolojia; Mkataba wa Kuruhusu
bidhaa za baharini ziweze kuuzwa China; Mkataba wa Ushirikiano baina ya Tanzania na
China kwenye masuala ya Utalii. Mingine ni Mkataba wa Makubaliano baina ya Tanzania
na China wa kuanzisha Ukanda wa Kisasa wa viwanda vya nguo pamoja na kukuza zao la
pamba na wa mwisho ni mkataba wa kutoa vitalu namba 60 na 61 kwa ajili ya ujenzi wa
ubalozi wa China jijini Dar es Salaam.
Katika mazungumzo yao, Waziri Mkuu ambaye
yuko katika siku ya pili ya ziara ya kikazi yake ya siku tisa kwa mwaliko wa Serikali
ya nchi hiyo, alimweleza Waziri Mkuu wa China kwamba anaishukuru Seriklai ya nchi
hiyo kwa misaada mbalimbali ambayo China imekuwa ikiitoa kwa Tanzania.
“Tunaishukuru
kwa misaada mbalimbali na mikopo ambayo imekuwa ikitolewa kwa masharti nafuu ikilinganishwa
na mikopo ya kibiashara ambayo hutolewa na nchi nyingine na kawaida ina gharama kubwa
kwa Taifa,” alisema Waziri Mkuu wakati akizungumza na waandishi wa habari mara baada
ya kumaliza mazungumzo na mwenyeji wake.
Alisema alitumia fursa hiyo kusisitiza
uwekezaji kwenye sekta za kilimo, nishati, elimu na miundombinu hasa reli, bandari
na teknohama. Kwenye kilimo, Waziri Mkuu alikumbusha suala la upatikanani wa soko
kwa zao la tumbaku lakini akaomba uwepo umuhimu wa pekee kwa wawekezaji wa viwanda
vya kusindika korosho katika mikoa ya kusini.
“Katika ziara yangu nitapenda
kusisitiza haja ya uwekezaji kwenye zao la korosho... nitazungumza na maafisa wanaohusika
ili tuone jinsi ya kulipa msukumo zao hili ambalo lina soko kubwa sana hapa China,”
alisema.
Alimweleza Waziri Mkuu wa China dhamira ya Serikali ya Tanzania kulipa
deni la dola za marekani milioni 24.6 ambalo lilitolowa kama mkopo kwa ajili ya kufufua
kiwanda cha nguo cha urafiki.
“Tumeahidi kuanza kulipoa deni hilo katika mwaka
wa fedha 2014/2015. Waziri wa Fedha alishaandika barua kwa Serikali ya China tangu
mwezi Septemba kuonyesha nia ya Serikali ya kulipa deni hilo,” alisema Waziri Mkuu
Ijumaa,
Oktoba 18, 2013 Waziri Mkuu atafungua mafunzo ya siku 10 kwa maafisa 20 kutoka idara
na taasisi za serikali za hapa nchini yanayoendeshwa kwa pamoja baina ya Chuo cha
Uongozi cha China na Taasisi ya Uongozi ya Tanzania; atatembelea kiwanda cha Aluminium
hapa Beijing, atakutana Bodi ya Tumbaku, Kampuni za Umeme za China Power Investment
(CPI) na State Grid Corporation. Pia atakutana na kampuni ya mafuta ya CNOOC. Jioni
atakutana na Watanzania waishio Beijing kwenye ubalozi wa Tanznaia nchini China.