2013-10-17 10:20:23

Makatekista ni majembe katika mchakato wa Uinjilishaji wa kina!


Wakumbukeni viongozi wenu, wale waliowaambia neno la Mungu. Tafakarini jinsi walivyoishi na matokeo ya mwenendo wao, mkaige imani yao . Ebr. 13:7. Ni tafakari inayoletwa kwako na Padre Pambo Mkorwe, OSB, Mama Kanisa anapoadhimisha Mwaka wa Imani.

Awali ya yote, tumwelewe Katekista kama mtu aliyesheheni mafundisho ya Imani [yaani Katekesi], na hivyo huwajibika katika kuwafundisha watu maundisho hayo, ili watu wapate kuijua imani yao na kuiishi na pia kuiishi miongozo adilifu tunayopewa na Mama Kanisa Mtakatifu. Katika mazingira yetu ya kawaida, Katekista huitwa pia mwalimu wa Dini. Mwalimu huyu wa dini huchukua nafasi yake, mara baada ya ngazi ya familia na huendelea na wajibu huo hadi mwisho wa maisha yetu ya imani.

Ni yeye huwaandaa watu kwa ajili ya sakramenti ya Ubatizo, huwatayarisha wazazi wanaomleta mtoto kwa ajili ya ubatizo; huwatayarisha vijana wetu kwa ajili ya Sakramenti ya Ekaristi Takatifu na Kipaimara. Huwaandaa waamini kabla ya kupokea Sakramenti ya ndoa. Na pia katika mazingira yaliyo mengi, Katekista hushughulika katika kuwazika wafu wetu.

Kwa hayo yote, tunaona kuwa Katekista/Mwalimu wa dini ni mhimili haswa katika maisha yetu ya Imani. Mwamini Mlei, amep;itia mikononi mwa Katekista, Makatekista wenyewe wametokana na kazi ya Makatekista; Watawa nao, wamepitia mikononi mwa Makatekista, Mapadre, ni matunda ya kazi njema ya makatekista, Maaskofu ni matunda ya kazi ya Makatekista, Makardinali, Papa na waamini wote wenye wadhifa mbalimbali katika Kanisa na Serikali, sote tu matunda ya kazi njema ya Katekista, aliyetufundisha imani na maadili. Katika hayo yote, ebu tuone uzito na umaana wa kazi ya Katekista.

Baada ya kutmbua hayo, tujiulize sisi sote, ni namna gani tunaenzi kazi ya makatekista, ikiwa ni pamoja na kuchangia hali njema ya maisha ya makatekista. Waamini wapendwa, hapa tufikiri zaidi juu ya jukumu letu la kuwategemeza Makatekista wetu, ili waendelee kuitenda kazi yao kwa ufanisi zaidi. Wito huu utuelekee kwanza kabisa sisi Mapadre, tukitambua kwamba, Makatekista ndio mikono yetu ya kuume katika utumishi wetu hasa huko maparokiani na vigangoni, pia katika jumuia ndogondogo.

Pia waamini walei waguswe na mwito huu wa kuwategemeza Makatekista, kwani katika dunia yetu ya leo, kwa kiasi kikubwa sana, kwani mafundisho yale ya imani yaliyopaswa kutolewa na wazazi katika familia, wazazi hawafanyi hivyo kutokana na visingizio mbalimbali na badala yake Makatekista wetu ndio hutusaidia katika kazi hiyo. Tunawategemezaje? Tufikiri kwa pamoja juu ya uzito na umaana wa kazi yao , na tusaidie kuinu hali yao ya maisha.

Pamoja na wito huo kwa Mapadre na Waamini, tumrudie Katekista mwenyewe! Unajionaje katika utume wako? Umeupokea utume wako kama kazi ya msingi kabisa katika maisha ya Imani ya watu wa Mungu? Katekista, tambua kwamba wewe ni Mwalimu na Kiongozi wa watu. Hivyo, ili utume wako uwe na maana haswa ni vema sana ukajijengea haiba ile ya mwalimu mwema na mwadilifu. Ukizingatia uadilifu basi hata neno utakalolisema litakuwa na mamlaka.

Kwa kuwa Katekista, hapo tayari una madaraka kama mwalimu. Lakini je, madaraka yako yana mamlaka. KATEKISTA WEWE NI KIONGOZI, BASI NA UWE KIONGOZI MWENYE MADARAKA NA MAMLAKA. Hapo ndipo unapoalikwa kwa uweza wako wote kuishi maisha yaliyo adilifu, maisha yaliyo kielelezo bora kwa wale uwafundishao. Usipokuwa mwadilifu, utakosa mamlaka; yaani mafundisho yako hayatakuwa na nguvu ya kufundisha, kuonya, kuelekeza wala kusahihisha. Waamini wanapenda pia kuona unakiishi kile unachokisadiki na kukifundisha.

Jitoe kikamilifu katika utume wako, ukitanguliza utukufu wa Mungu mbele, nawe utapata yote yaliyo mema sasa na halafu. Fanya kila uwezazo ili upokeleke na ukubalike na watu kwa maisha yako adilifu. Ni hapo tu ndipo utaona faraja kuu katika utumishi wako. Basi, na uufanye utumishi wako uwe furaha yako.

Mungu akubariki na kukutegemeza katika utumishi wako mwema na mwaminifu, na mwisho wa kazi yako njema sana hapa duniani, wewe pamoja na wote uliowahudumia, mkastahili kufika mbinguni, Amina.

Pd. Pambo Martini Mkorwe O.S.B.








All the contents on this site are copyrighted ©.