Waungwana wajadili kuhusu maboresho ya sheria ya kurekebisha mabadiliko ya Katiba!
Mkutano kati ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Mrisho Kikwete na
viongozi wa vyama vya siasa vyenye uwakilishi Bungeni umemalizika Ikulu, Dar Es Salaam,
Jumanne, Oktoba 15, 2013 kwa pande hizo mbili kukubaliana kama ifuatavyo:
Moja,
kwamba vyama vyote vya siasa nchini vyenye mawazo, maoni na mapendekezo ya kuboresha
Sheria ya Kurekebisha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba viwasilishe mapendekezo yao haraka
Serikalini ili ifatutwe namna ya kuyashirikisha mapendekezo hayo katika marekebisho
ya Sheria hiyo.
Pili, kwamba vyama vya siasa nchini, kama wadau muhimu katika
mchakato wa Katiba Mpya, viangalie namna ya kukutana na kujenga mfumo wa mawasiliano
na maridhiano wa jinsi kwa pamoja vitakavyosukuma mbele mchakato huo kwa maslahi mapana
ya nchi yao na mustakabali wa taifa. Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD) kimepewa
jukumu la kuratibu jambo hilo ikiwa ni pamoja na kuandaa mkutano wa vyama hivyo na
wadau wengine nchini.
Viongozi wa vyama vyama vya siasa waliokutana na Mheshimiwa
Rais Kikwete ni Mheshimiwa Profesa Ibrahim Lipumba, Mwenyekiti wa CUF; Mheshimiwa
Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa CHADEMA na Mheshimiwa James Mbatia ambaye ni Mwenyekiti
wa NCCR-Mageuzi.
Wengine ni Makamu Mwenyekiti wa CCM Mheshimiwa Philip Mangula,
Mheshimiwa Isaack Cheyo ambaye amemwakilisha Mwenyekiti wa Chama cha UDP Mheshimiwa
John Cheyo na Mheshimiwa Nancy Mrikaria ambaye amemwakilisha Mwenyekiti wa TLP Mheshimiwa
Augustine Mrema. Waheshimiwa John Cheyo na Mrema wako nje ya nchi.
Wengine
ambao wameambatana na wenyeviti wao ni Mheshimiwa H. Mnyaa na Bwana Julius Mtatiro
wa CUF, Waheshimiwa Tundu Lissu na John Mnyika wa CHADEMA na Bwana Martin Mng’ongo
wa NCCR-Mageuzi.