2013-10-16 08:54:09

Siku ya Chakula Duniani kwa Mwaka 2013


Kila mwaka ifikapo tarehe 16 Oktoba, Jumuiya ya Kimataifa inaadhimisha Siku ya Chakula Duniani ambayo kwa Mwaka 2013 inaongozwa na kauli mbiu "watu wenye afya wanategemea mfumo bora wa chakula".

Hii ni siku ambayo Jumuiya ya Kimataifa inafanya tafakari ya kina kuhusu umuhimu wa maboresho ya mfumo wa usalama wa chakula na lishe, utunzaji bora wa chakula pamoja na changamoto kwa wadau mbali mbali kuchangia katika mchakato wa kuwa na uhakika wa usalama wa chakula duniani.

Maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani yatahitimishwa hapo tarehe 20 Oktoba kwa wakazi wa Roma kushiriki katika mbio za Marathoni, ili kuchangia mfuko wa uhakika wa usalama wa chakula duniani.

Tukio hili linaadhimishwa kwa namna ya pekee kwenye Makao Makuu ya Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa, FAO yaliyoko mjini Roma, sanjari na kumbu kumbu ya kuanzishwa kwa FAO kunako mwaka 1945. Takwimu za FAO zilizotolewa hivi karibuni zinaonesha kwamba, kuna zaidi ya watu millioni 842 wanaokabiliwa na lishe duni. Jumuiya ya Kimataifa imeendelea kushuhudia uhalibifu mkubwa wa mazingira unaosababisha athari katika mabadiliko ya tabianchi. FAO inasema, mambo yote haya yanatishia uhakika wa usalama wa chakula kwa siku za usoni.

Mfumo wa Chakula unajengeka katika mazingira, watu na taasisi mbali mbali, mchakato unaowezesha upatikanaji wa mazao ya kilimo, yanayosindikwa na hatimaye kuwafikia walaji. Kila hatua ya mchakato huu ina athari zake katika maisha ya mlaji ambaye anapaswa kuchagua lishe bora zaidi.

Maadhimisho ya Siku ya Chakula Duniani iwe ni fursa kwa Jumuiya ya Kimataifa kufanya tafakari ya kina kuhusu mustakabali wa mamillioni ya watu wanaoteseka kutokana na baa la njaa duniani.







All the contents on this site are copyrighted ©.