2013-10-15 11:18:51

Watoto wachangamotishwa kuwa ni Wamissionari!


Askofu Gervas Nyaisonga wa Jimbo Katoliki Dodoma, amewataka watoto kutambua kwamba wao ni zawadi kutoka kwa Mungu, kwa hiyo jukumu lao kubwa ni kuwa Wamisionari kwa kuitangaza Injili kila mahali ili wasiomjua Mungu waweze kumkiri na hatimaye, waweze kuokoka.

Askofu Nyaisonga amesema hayo Jimboni Dodoma katika kituo cha hija Mbwanga wakati wa adhimisho la Ibada ya misa takatifu ya kongamano la maadhimisho ya hija ya Mwaka wa Imani kwa watoto wa Shirika la kipapa Jimboni Dodoma. Askofu Nyaisonga amesema kuwa watoto, wanatakiwa kulisaidia Kanisa kwa kulitangaza Neno la Mungu, kuanzia majumbani mwao, shuleni, kwenye michezo na kuwahamasisha wengine wampende Mungu na kuchukia dhambi.

Askofu Nyaisonga pia amewataka watoto wa Tanzania wamuombee Baba wa taifa hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ambaye anatimiza miaka 14 tangu alipofariki dunia. Amesema ni jukumu la watoto kumuombea ili siku moja Kanisa limtangaze kuwa mwenyeheri.

Kwa Upande wake Askofu Mstaafu Mathias Isuja Joseph wa Jimbo Katoliki Dodoma, amewataka watoto kusoma kwa bidii ,ili kwa siku za baadaye waweze kuishi maisha mazuri.


Na wakati huo huo, Askofu Gervas Nyaisonga wa Jimbo Katoliki Dodoma amewataka Wakristo nchini Tanzania kuishi maisha ya utumwa na kutambua kuwa Yesu Kristo ndiye mmiliki wao. Amesema kuwa si jambo la aibu kujiita mtumwa bali ni heshima hasa kuwa mtumwa wa Yesu Kristo kwani Yesu mwenyewe ndiye anaye wajibika kwa watumwa wake.

Askofu Nyaisonga amesema kuwa wapo baadhi ya watu ambao hawaamini kama Mungu yupo na kuendelea kutenda Dhambi kwa kuwa hawaoni wala kusikia sauti ya Mungu ikiwakemea waache uovu wao. Hata hivyo amesema ni vema Wakristo kuwa kama Mtume Paulo alipo ulilizwa wewe ni nani, naye akajibu mimi ndiye mtumwa wa Yesu Kristo akimaanisha kuwa yeye ni mali ya Yesu Kwani bila Yesu hawezi chochote.








All the contents on this site are copyrighted ©.