2013-10-15 08:06:39

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 27 ya Kipindi cha Mwaka C wa Kanisa


Tupo pamoja tena katika kumegeana mkate kama lilivyo agizo la Bwana, tayari safari yetu katika mwaka huu wa Kanisa iko katika kituo cha Dominika ya 27. Bwana azidi kutufundisha kwa njia ya Neno lake aksema, imani ndogo iliyokamilifu yatenda mambo ya ajabu tusiyoweza kuyafikiria, ndiyo kusema lazima iwe imani inayokabidhi maisha ya mtu mwenyewe mwenye imani katika mikono na uweza wa Mungu.

Katika somo la kwanza tunaona Nabii Habakuki analalamika na kunungunika mbele ya Mungu akisema mbona hataki kusikiliza kilio chake! Hata hivyo yafaa kutambua kuwa mateso wanayoyapata hawa wana wa Israeli ni kwa sababu ya ukaidi wao ambao ndio uliowafanya watekwe na makabila mengine. Inavyoonekana ni mpango wa Mungu kuwaaacha ili waonje nini maana ya kumwacha yeye na kuwaelekea miungi wengine!

Lakini hata hivyo anawahaidi kama watamgeukia yeye na kujenga uaminifu tena atawaondoa katika taabu yao hiyo. Mwaliko kwetu ni kujenga imani na mapendo kwa Mungu kama tunataka kuondokana na utumwa unaosababishwa na ukaidi wa mioyo yetu na hivi kutupelekea katika anguko la dhambi.

Ndiyo kusema wimbo wa katikati wa Dominika hii umewekwa mahali pake ukituambia, Ingekuwa heri leo tusikie sauti yake, tusifanye migumu mioyo yetu. Katika mwendelezo huo Mt Paulo anakuja na agizo kwa Mt. Timotheo, akimwambia yafaa kuchochea karama uliyopewa kwa njia ya kuwekewa mikono, na kwa namna hiyo unadaiwa kumshuhudia Kristu kwa nguvu zako zote na hata ikikulazimu kupata mateso mengi.

Mpendwa msikilizaji, umepokea karama za Bwana kwa njia ya ubatizo na kwa njia ya sakramenti nyingine basi inakulazimu kuchochea karama hizo na kuziishi kwa furaha ukimweka Bwana katika nafasi ya kwanza katika maisha yako ya umisionari. Hapa ndipo kuna kuishi imani yako inayotakiwa ijidhirishe katika kujikabidhi mikononi mwa Mungu.

Mwinjili Luka anaweka maneno ya Bwana mbele yetu anayetualika kukua katika imani, ambayo kwayo twaweza kutenda miujiza mbalimbali na hasa mwujiza mkuu wa upendo. Wajibu wa Mkristu ni kushika imani na kuishi imani hiyo kwa unyenyekevu, pasipo madai yoyote mbele ya Mungu au mbele ya watu. Jukumu kubwa hilo linatekelezwa na kuonekana katika Injili Bwana anaposema inatosha tu kusema sisi ni watumwa tusio na faida.

Ndiyo kusema, Bwana anataka kutuambia tuishi tumaini la kweli katika Bwana tukitarajia ya kwamba yote atatenda kwa mapendo yake mara baada ya sisi kutekeleza wajibu wa kuishi imani yetu katika yeye kama Mt Paulo atuambiavyo akisema, kwangu kuishi Kristo.

Baada ya kuupata huo utangulizi sasa, polepole tujiulize hili fundisho la Bwana juu ya imani linatoka wapi? Kwa hakika fundisho hili linakuja baada ya Mitume kumwambia Bwana tuongezee imani, kama ambavyo hata sisi tunalo hitaji la kujitafiti na kumwomba Bwana tukisema, tuongezee imani! Tukishaweka swali hili mbele ya Bwana yafaa tena kujiuliza lakini imani ni nini?

Je, ni ujuzi?, Je, ni maarifa? Je, ni maisha ya utekelezaji wa sheria za kidini au tuseme ni nini? Katika haya tuliyoyataja kama imani ingekuwa ndo hayo basi imani ingekuwa ni kitu cha kumiliki na kwa namna hiyo kingekuwa kitu cha kukuzwa!

Kutokana na swali hilo Bwana anakuja na namna tofauti ya kuitazama imani na anatufundisha nasi kufuata mkondo huo. Bwana anasema kama mngelikuwa na imani kiasi cha chembe ya haradali, mngeuambia mkuyu huu ngoka na ungewatii! Bwana anataka kusema imani haiko katika vipimo vya kimahesabu, na wala si ujazo bali ni kuitika mwaliko wa Bwana na kujikabidhi nikiwa nilivyo hata katika udhaifu wangu katika mikono ya Mwenyezi Mungu ambamo hakuna kisichowezekana.

Imani ni laini mno kama mbegu ya haradali na ni nguvu kwa wakati huohuo iliyo ndani ya mbegu hiyo ambayo huvunja suke ili maisha yaweze kutokea au kuzaliwa! Imani ni nguvu ya Kimungu inayoongoza maisha ya mwanadamu anayekubali mapenzi ya Mungu. Kumbe yatosha kusadiki na kujikabidhi katika nguvu hiyo takatifu.

Kwa imani ndogo yatosha kubadili maisha yetu kwa maana udogo huu unajikita katika mtima wa Mungu mwenyewe na kwa namna hiyo hubadili maisha ya ulimwengu, cha msingi ni kuishi imani hiyo kwa unyenyekevu. Inatosha imani kidogo kuweza kuondoa woga ambao hujitokeza katika maisha yetu unaotokana na mwenendo na mporomoko wa waamini wakristu katika Kanisa la leo. Woga huu haupaswi kukua kwa maana kama tukiamini Kanisa huongozwa na Roho Mtakatifu basi yeye atafanya kazi yake apendavyo na kuliongoza lifikie mwisho wa nyakati.

Kwa kumtanguliza Roho Mtakatifu tayari tunaingia katika kuepuka kujitafutia utukufu wetu wenyewe bali utukufu wa Bwana mwenyewe. Ndiyo kusema baada ya kuishi imani yetu, baada ya kutumikia tunapaswa kusema sisi ni watumwa wasio na faida. Kanisa linapaswa kutumikia Bwana aliye kichwa chake na wala si mtu mwingine awaye yote likisema mimi ni mtumishi wa Bwana nitendewe kama Bwana utakavyo. Ni kwa namna hiyo linajikabidhi katika maongozi ya Roho Mtakatifu mwanzilishi na kiongozi wa Kanisa.

Mpendwa msikilizaji, huu, ndio wito wako daima kujikabidhi mikononi mwa Mungu ambaye ni chanzo cha maisha yetu na ukomo wake. Kuishi maisha ya pamoja yanayoongozwa na unyenyekevu unaojikita katika kuutangaza ukuu wa Mungu anayeongoza Kanisa kwa njia ya Roho Mtakatifu. Nikutakie heri na furaha daima katika maisha yako yak ila siku ukijitahidi kushiriki zawadi za Kimungu zitujiazo kwa njia ya imani. Tumsifu Yesu Kristo na Maria.

Tafakari hii imeletwa kwako na Pd. Richard Tiganya C,PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.