2013-10-15 07:53:57

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 24 ya Kipindi cha Mwaka C wa Kanisa


Nakuleteeni Tafakari masomo ya Dominika ya 24 ya mwaka C wa Kanisa. Injili inatupa changamoto ni namna gani twaweza kuwa wema katika maisha yetu ya Kikristu. Bwana wetu Yesu Kristu anapofundisha hupenda kufundisha akitumia mazingira halisi toka mawazo na kuingia jambo gusika, kumbe, hutumia mifano akitaka kutuambia Mungu Baba ni nani!

Kwa kutumia lugha halisi na mifano Bwana anagusa mioyo na mambo hayo hubaki katika kumbukumbu. Katika Injili tunayoitafakari Bwana Mtakatifu Luka anatupa mifano mitatu aliyoitumia Bwana katika kupeleka jibu la Mungu Baba ni nani.

Mungu Baba tunayemsikia katika mfano wa kwanza ni yule ambaye yu karibu nasi, ambaye anafuatilia maisha yetu ili tusipotee na hata tukichomoka toka katika zizi basi hufanya kila aina ya bidii kuturudisha. Kumbe Mungu Baba yuko karibu nasi kwenye familia, vituo vya kazi na mahali pote ambapo tunapata kuishi. Ndama mmoja au shilingi moja ikipotea basi huacha walio wengi au zilizo nyingi ili kuhakikisha moja iliyopotea inapatikana.

Ndiyo kusema Mungu Baba anataka hata mmoja wetu asipotee bali awe na uzima wa milele. Ni tofauti na Mungu wa Mafarisayo ambaye ni kwa ajili ya wenye haki tu! Mungu Baba ni yule ambaye hamtengi hata mmoja bali ni kwa ajili ya wote wema na wabaya.

Mpendwa msikilizaji, mfano wa tattu ni ule wa mwanampotevu, ambaye kwa hakika katika hali ya kawaida asingepaswa tena kufanyiwa sherehe kubwa namna ile. Lakini Baba kwa upendo mkamilifu pasipo kuuliza ulikuwa wapi anamvika mavazi na pete ya thamani kubwa. Anatuonesha furaha ya kurudi kundini yule aliyepotea. Inatuonesha matunda ya toba kwa awaye yote katika maisha ya hapa duniani tukielekea mbinguni.

Baba anasema, tufanye sikukuu! Bwana anasimulia na kuonesha moyo wa Mungu unaowaka mapendo na furaha iliyofungamana na kusamehe na si furaha kuwaka moyoni bali hata kuifurahia furaha hiyo.

Mpendwa msikilizaji mwanafalsafa Machiavelli aliwahi kusema “siasa ni hali ya kutokuwa mwema” hii ni hali ambayo imeenea sasa katika ulimwengu wa leo, inajionesha katika kutotenda haki kwa wananchi. Basi leo Bwana anataka kutupeleka upande mwingine yaani namna ya kuwa mwema katika maisha yako! Ni kuishi na kutenda Huruma kwa wengine kama Baba alivyomtendea mwanampotevu. Ni kuwarudisha walioenda mbali nasi karibu nasi.

Huruma ambayo Baba anaionesha inakuwa kinyume na kaka mkubwa ambaye alikuwa amejaa hasira kwa sababu ya kusamehewa mdogo wake kahaba aliyetumia vibaya mali ya Baba yake. Huyu kaka mkubwa tunaweza kusema ni mwenye kutenda pasipo imani, maana imani yatupeleka mpaka pale ambapo upendo haufungwi na sheria na mipaka ya mahesabu bali unajitoa katika hali zote.

Basi yafaa kuangalia sisi tunayo imani au ni watendaji wa shughuli zinazohusiana na imani? Imani si tu katika vitu vya nje bali ile ambayo hutupeleka katika kushirikishana utajiri wa mbinguni, matendo ya kimungu, huruma ya Kimungu nk.

Mpendwa, nikutakie safari ya mabadiliko ya kiroho ukitaka kujifunza matendo na huruma ya kimungu daima ili kuweza kuwa daraja kwa ajili ya wokovu wa wengine.Tumsifu Yesu Kristo.

Tafakari hii imeletwa kwako na Pd. Richard Tiganya C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.