Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda ameondoka Dar es Salaam, Jumanne, Oktoba 15,
2013 kwenda China kwa ziara ya kikazi ya siku tisa kwa mwaliko wa Serikali ya nchi
hiyo inayotarajiwa kuanza , Oktoba 16, 2013. Lengo la ziara ya Waziri Mkuu ni kutangaza
fursa za uwekezaji nchini Tanzania, fursa za biashara, za utalii na kutafuta mitaji
kwa ajili ya sekta zilizo chini mpango wa matokeo makubwa ya haraka (Big Results Now
Initiative).
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Wizara ya Mambo ya Nje na
Ushirikiano wa Kimataifa Waziri Mkuu atakuwa na mazungumzo na Waziri Mkuu wa nchi
hiyo, Mhe. Li Keqiang na viongozi wa Serikali ya China katika katika sekta za uchukuzi,
mawasiliano, viwanda, madini na nishati.
Atatembelea mji wa Beijing na majimbo
ya Shenzen, Chengdu na Guangzhou ambako atakutana na Makamu wa Rais wa China, Rais
wa Benki ya Exim ya China, Rais wa Benki ya Maendeleo ya China, wakuu wa mashirika
makubwa na kampuni kubwa nchini China na kufanya nao mazungumzo.
Waziri Mkuu
Pinda ataungana na Wakuu wa Nchi watano kwenye ufunguzi wa maonesho ya kibiashara
ya magharibi mwa China (Western China International Fair – WCIF) ambako atahutubia
washiriki wa maonyesho hayo. Pia atatembelea maeneo kadhaa ya uwekezaji na kufungua
Kongamano la Uwekezaji baina ya Tanzania na China litakalofanyika Guangzhou.
Vilevile,
Waziri Mkuu anatarajiwa kufungua mafunzo ya siku 10 kwa maafisa 20 kutoka idara na
taasisi za serikali za hapa nchini yanayoendeshwa kwa pamoja baina ya Chuo cha Uongozi
cha China na Taasisi ya Uongozi ya Tanzania. Mafunzo hayo ni sehemu ya mpango wa Serikali
kuboresha utendaji wa Maeneo ya Uzalishaji kwa Mauzo ya Nje (EPZ).
Waziri
Mkuu ambaye anafuatana na Mawaziri wanne, wabunge wawili, wakuu wa mikoa watatu, wakuu
wa taasisi wa Serikali na wawakilishi kutoka sekta binafsi, anatarajiwa kukutana na
Watanzania waishia China huko Beijing na Guangzhou.
Tanzania imekuwa na uhusiano
na ushirikiano wa karibu na China, nchi kubwa ya Bara la Asia, tangu mwaka 1964.
China
yenye ukubwa wa kilometa za mraba 9,596,961 ina wakazi wapatao 1,349,585,838. Kwa
mujibu wa takwimu za Shirika Fedha la Kimataifa (IMF) nchi hiyo ni ya pili kwa uchumi
mkubwa duniani.