Msongamano wa magari kwenye mizani Tanzania sasa ni "Janga"
Zikiwa zimepita siku chache tangu Waziri Mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda aagize malori
yarejee kutumia utaratibu wa zamani wa kupima mizigo kwenye mizani, hali bado ni tete
kutokana na misururu mikubwa iliyokuwepo Jumapili, Oktoba 13, 2013 kwenye mizani ya
Mikese na Kibaha.
Mwandishi wa habari hizi alishuhudia msururu wa malori na
mabasi zaidi ya 105 kwenye mizani ya Mikese mkoani Morogoro bila kujali idadi ya magari
madogo yaliyokuwepo kwenye foleni ya kutoka Dar es Salaam kuelekea Morogoro.
Mashuhuda
waliokuwepo kwenye mizani ya Mikese walisema kuwa mizani inayopima magari ya kutoka
Morogoro imeharibika tangu jana ndiyo maana inatumika mizani ya upande mmoja tu (wa
kutoka Dar es Salaam). Kulikuwa na dalili za mafundi kufanya matengenezo kwenye maegesho
ya mzani huo ambapo malori na mabasi huwa yanasimama.
Katika mizani ya Kibaha
mkoani Pwani hali nako haikuwa shwari sana licha ya kuwa mizani ya pande zote mbili
ilikuwa ikifanya kazi. Magari ya kutoka Dar es Salaam peke yake yalikuwa zaidi ya
90 bila kuhesabu magari madogo yaliyokuwa kwenye foleni hiyo ya kuelekea Morogoro.
Hivi
karibuni, Waziri Mkuu alitengua uamuzi wa awali wa Serikali uliotolewa Oktoba Mosi,
2013 na Waziri wa Ujenzi ambao ulikuwa ukiondoa msamaha wa tozo kwa uzito wa magari
uliozidi ndani ya asilimia tano ya uzito unaokubalika kisheria.
Vilevile, Waziri
Mkuu aliamua kuunda kamati maalum kamati ambayo aliipa muda wa mwezi mmoja na kuitaka
ikutane na wadau ambao ni Chama cha Wamiliki wa Malori nchini (TATOA) na Chama wa
Wamiliki wa Mabasi yaendayo Mikoani (TABOA) ili kupata ufumbuzi wa mgogoro uliojitokeza.
“Natoa
kipindi cha mwezi mmoja kwa wizara husika na wadau hao kukamilisha kazi hiyo. Katika
kipindi hicho cha mpito, utaratibu ulikuwepo awali kabla ya tangazo la tarehe 01 Oktoba
2013 lililotolewa na Wizara ya Ujenzi, utaendelea kutumika,” alisema.
"Kwa
kuwa bado kuna mgogoro kati ya Wizara ya Ujenzi, Wasafirishaji wa malori na mabasi
kuhusu utekelezwaji wa kanuni 7(3), ambao wanasema haitekelezeki kirahisi, naiagiza
Wizara ikutane na wadau. Wakae na kujadili namna bora ya kutekeleza kanuni hii, Wizara
ya Ujenzi, Wizara ya Uchukuzi, Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa
Serikali, waunde timu ya wataalamu ambao watakutana na wawakilishi wachache wa TATOA
na TABOA ili wapitie kanuni hizi kwa lengo la kupata mwafaka," alisema Waziri Mkuu.