2013-10-12 08:40:41

Liberia -Siku ya Kimataifa ya mtoto wa kike.


Taifa la Liberia , Ijumaa lilikuwa msitari wa mbele kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Mtoto wa Kike. Kwa ajili hiyo, Rais Ellen Johnson-Sirleaf wa Liberia, aliitangaza siku hiyo ya Kimataifa kwa ajili ya mtoto wa kike, rasmi kama Sikukuu ya Kitaifa lakini lakini ya kikazi.
Hapo siku ya Jumatano Wizara ya mambo ya nje ya nchi hiyo ilitoa mwito kwa mashirika yote ya kitaifa na kimataifa yakiwemo mashirika kama vile Shirika la kuwahudumia watoto la Umoja wa Mataifa, UNICEF, na Plan Liberia, pamoja na wizara mbalimbali za serikali ya Liberia, kuungana na Wizara ya Jinsia na Maendeleo ya nchi hiyo ili kuandaa Khafla mbalimbali kwa ajili ya kuadhimisha sikukuu hiyo ipasavyo.
Rais Sirleaf anasema kwamba kuadhimisha siku hiyo ya kimataifa kwa ajili ya wasichana kunaenda sambamba na azimio la Umoja wa Mataifa (United Nations General Assembly Resolution 66/170) la Disemba 19, 2011 lililoikumbatia siku ya Oktoba 11 kama “Siku ya Kimataifa kwa ajili ya Mtoto wa Kike”
Maadhimisho ya siku hiyo mwaka huu (2013) yanalengo la kuangazia mada ya “Mbinu mpya kwenye elimu na majifunzo ya wasichana”. Maadhimisho hayo pia yananuia kujadiliana juu ya mbinu mkakati kwa ajili ya uboreshaji wa elimu ya wasichana nchini Liberia, na kuzindua Ripoti maalum kuhusiana na Mtoto wa kike nchini humo.
Ujumbe uliotoa Mwito wa kuadhimisha siku hiyo nchini Liberia pia umesema maadhimisho hayo nimwendelezo wa yale yaliyojiri kwenye kongamano lililofanyika nchini humo mwezi Julai 2013. Kongamano hilo lililohudhuriwa na wasichana kutoka pembe zote za Liberia lilijadili mbinu za kuwajengea wasichana uwezo wa kujadili na kutekeleza maazimio ya kumwendeleza mtoto wa kike nchini humo.
Maadhimisho ya Siku ya kimataifa ya Mtoto wa Kike yanatoa fursa kwa Liberia kutazama upya haki za wasichana na changamoto za kipekee zinazowakumba watoto wa kike ndani ya jamii kote duniani, na hivyo kuonyesha mshikamano na jumuiya ya kimataifa katika jitihada za kuthamini mchango wa wasichana kwenye jamii. Ni fursa pia ya kutafuta mbinu muafaka za kuwekeza kwa ajili ya kuwawezesha watoto wa kike ki maisha na kupinga kabisa kuwabagua, na uonevu wowote wa kijinsia dhidi ya wasichana.











All the contents on this site are copyrighted ©.