2013-10-04 08:37:28

Miaka 50 ya waraka wa "Amani Duniani".


Msingi wa amani unaanzia kwenye asili takatifu na ya kimungu ya binadamu. Nayo hati ya kichungaji juu ya amani duniani "Pacis In Terris" inaazimia kuwakumbusha binadamu asili hiyo ya binadamu, ya jamii na hata ya uongozi na madaraka. Ni asili hii Takatifu ambayo inawaashiria watu binfsi, wana familia, vikundi mbalimbali kwenye jamii na hata mataifa kufanya juhudi za kuendeleza mahusiano ya haki na mshikamano.

Ndivyo anavyosema Baba Mtakatifu Francisko kwenye maadhimisho ya miaka hamsini ya hati ya kichungaji Pacis In Terris.

Kama Yesu Kristo mwenyewe alivyofanya, anasema Baba Mtakatifu, kila mmoja anao wajibu wa kujenga amani kwa kuishi kwa haki, ukweli na upendo, huku akichangia, kwa uwezo wake, maendeleo ya kina ya binadamu, ndani ya mantiki ya ushirikiano na mshikamano halisi.

Ukumbusho wa Hati ya Pacis In Terris umefanyika muda mfupi baada ya kutangazwa siku ya kumtawadha hadhi ya utakatifu, Mwenye Heri Yohanne wa XXIII, Baba Mtakatifu aliyeichapisha hati hiyo mnamo tarehe 11/04/1963.

Ulikuwa ni wakati wa vita baridi, anasema Papa Francisko, na dunia nzima ilikumbwa na kilio kwa mateso yaliyowafika watoto kwa wazee. Ni wakati huo ambapo Papa Yohanne wa XXIII alipotoa mwito kwa jamii ya kimataifa kuchunguza dhamira na kumwelekezea Mungu maombi ya amani

Hiki ni kilio kilichoelekezwa kwa watu waliokuwa kwenye madaraka, lakini zaidi kilikuwa kilio kilichoelekezwa mbinguni, kwa Mungu mwenyewe. Kutokana na mwito huo wa Papa Yohanne wa XXIII kulianzishwa mjadala mrefu na mgumu kati ya pande zilizokuwa zikizizana. Mwito huo ulitoa uwanja wazi kwa ajili ya majadiliano ya kina, mjadala ambao hatimaye uliendelezwa na Baba Mtakatifu aliyefuatia, Mwenye Heri yohanne Paulo II.
Mbegu za amani alizopanda Mwenyeheri Yohanne wa XXIII zimezaa matunda, anasema Papa Francisko.

Baba Mtakatifu anaendelea kuwaalika wote kutafakari ikiwa kweli mafunzo ya pacis In Terris yana maana ndani ya kizazi cha leo, huku akijiuliza kama maneno AMANI, Mshiklamano na HAKI yana maana tu ndani ya kamusi au hata pia kwenye maisha ya kila siku ya kila mwanadamu. Changamoto iliyoko, anasema Baba Mtakatifu, ni kwamba hakuwezekani kuwa na amani ya kweli na ulinganifu kati ya watu, ikiwa hakuna kujishughulisha, kwa udi na nta, katika kujenga jamii bora zaidi yenye kuzingatia haki na mshikamano; jamii inayoshinda ubinafsi, umimi, na mafao ya vikundivikundi, katika kila hali; Jamii inayojua kumthamini kila mwanadamu, aliye na asili Takatifu, ya kimungu; Jamii inayowakumbatia watu wote.











All the contents on this site are copyrighted ©.