2013-09-25 08:24:52

SECAM Kukutana na Viongozi wa kiserikali wa Afrika mjini NY


Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar, SECAM likishirikiana na mashirika ya kimataifa ya kikanisa yenye kuhusika na maendeleo ya jamii, limepanga kukutana na baadhi ya viongozi kutoka nchi za Afrika wakati wa Mkutano Mkuu wa 68 wa Umoja wa Mataifa unaofanyika mjini New York kuanzia tarehe 23 hadi 25 Septemba 2013. Lengo la mkutano huo ni kujadiliana pamoja na viongozi hao wa kitaifa juu ya mikakati kwa ajili ya maendeleo endelevu barani Afrika kwa siku za usoni.

Maaskofu wa SECAM wanauona huu kama wakati muafaka wa shirikisho hilo kufanya mazungumzo ya ana kwa ana na viongozi watakaokuwa wanayawakilisha mataifa ya Afrika kwenye mkutano huop wa New York. Mazungumzo hayo yanawania kumulikia maswala yanayojitokeza katika jitihada ya kutimiza malengo ya millenia kwa ajili ya maendeleo (MDG), na mikakati ya maendeleo ya bara baada ya mwaka 2015.

Maaskofu wanakubaliana kwamba ni muhimu kutoa kipaumbele cha kwanza katika kujenga uwezo wa wana wa bara la Afrika kuweza kujiendeleza wenyewe, maendeleo ya kudumu na wala sio maendeleo ya msimu, au yenye kuwafaidi watu wachache huku watu wengi wakiendelea kuhangaika bila ya matumaini. Wanasema maaskofu hao kwamba kuna umuhimu wa kuhakikisha kwamba maendeleo endelevu kwa ajili ya bara Afrika linatia maanani maswala ya maadili, hadhi ya binadamu na maslahi ya watu wote hasa wale walio wanyonge zaidi na wenye kusukumizwa pembezoni mwa jamii.

Baadhi ya marais watakaokutana na wawakilishi wa SECAM ni pamoja na Ellen Sirleaf Johnson, Rais wa Liberia na Mwenyekiti wa kamati ya juu ya viongozi wa serikali wa Umoja wa Afrika. Wengine ni Jacob Zuma wa Afrika Kusini, John Mahama wa Ghana, Haile Mariam Desalegu wa Ethiopia na mwenyekiti wa Kamati ya Umoja wa Afrika, Daktari Nkosazana Dlamini-Zuma.

Mashirika ya kimataifa yatakayowakilishwa kwenye majadiliano hayo ni pamoja na CAFOD, CIDSE, Trocaire, Caritas Internationalis, na Cordaid, Manos Unidas, Misereor na SCIAF.








All the contents on this site are copyrighted ©.