2013-09-21 08:16:24

Uinjilishaji mpya: kupitia mitandao ya kijamii


Mitandao ya kijamii imeonyesha kuvifuatilia kwa karibu Vyombo vya habari vya Kanisa Katoliki kwenye siku za hivi karibuni. Wengi wanasema hii ni kutokana na watu wengi kuvutiwa na Baba Mtakatifu Francisco ambaye habari zake huchapishwa kwanza kwenye vyombo hivyo. Vyombo kama gazeti la kila siku lenye kuchapishiwa mjini Roma la Osservatore Romano, lililoanzishwa mnamo mwaka 1861, na Radio Vatican, ambayo imekuwa ikirusha matangazo yake hewani tangu mwaka 1931 vimeonyesha ongezeko la watu wenye kuvifuatia kwa karibu kwenye mitandao ya kijamii kama vile Tweet na facebook.

Naye Baba Mtakatifu Francisko anaendelea kuwa kiongozi anayefuatiliwa zaidi kwenye mtandao wake wa Tweet ambapo ndani ya miezi sita ya wadhifa wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro tayari ana zaidi ya wafuasi millioni tisa na laki tatu, na zaidi ya watu millioni sabini hupata kusoma ujumbe wa Baba Mtakatifu kila siku kutokana na wenzao kuuweka ujumbe huo kwenye kurasa za mitandao yao. Nao mtandao rasmi wa mawasiliano ya Vatican sasa una zaidi ya wasomaji milioni kumi, laki mbili na sabini kutoka kote ulimwenguni wanaousoma wakitumia lugha mbalimbali za dunia.

Hii ni wazi ishara ya uinjilishaji mpya ya kizazi kipya, kwenye mazingira mapya ya mawasiliano ya kijamii yanayoendelezwa na utumiaji wa teknolojia za kisasa, anasema Askofu Mkuu Claudio Celli, rais wa Baraza la kipapa kwa ajili ya mawasiliano ya kijamii.

Akizungumza mjini Roma na gazeti la kila siku la Osservatore Romano siku moja kabla ya kuanza mkutano mkuu wa Baraza la Kipapa la mawasiliano ya kijamii, Mons. Claudio Celli amesema kwamba uwezo wa Baba Mtakatifu Francisko wa kuwasiliana na watu wa tabaka mbalimbali na kuweza kueleweka nao, ni namna mpya ya kuendeleza mawasiliano ya kijamii ndani ya Kanisa.

Anasema Askofu Mkuu Celli kwamba mambo manne yanajionyesha wazi kwenye staili ya mawasiliano ya Papa. Kwanza kabisa Baba Mtakatifu anatumia lugha ya kawaida, inayoelewekana mtu wa kawaida kwa urahisi. Pili anao ujumbe ambao unaigusa mioyo na dhamiri za watu kwani unagusia hasa mateso ya watu na safari ya ndani, mwaliko kwa kila mtu kujitafiti mwenyewe. Papa anafahamu kile kilischo moyoni na hivyo kumfanya kupendwa na watu wengi hata wale waio amini, na watu wa dini nyingine za kikristo na zisizo za Kikristo.

Kitu cha tatu kinachomfanya Papa Francisko kuwa kipenzi cha wingi, anasema Mons. Celli, ni namna yake ya kujieleza: Papa Francesco haongei tu, bali hutumia ishara zenye kuonyesha utajiri wa kile anachokizungumzia, kitu ambacho kinatokana na utajiri wake wa kiroho.

Na mwisho kabisa, Papa anajua kugusa fikira na hisia za watu hata kupitia kwa lugha ya mafumbo, lugha ambayo hutoa ujumbe husika zaidi hata ya maneno. Yeye hutumia sentesi rahisi kuelezea hata dhana zisizo rahisi hata kidogo. Mfano utakaokumbukwa ni ule wa alioutoa kama mwaliko kwa mapadri na Maaskofu kuwa wachungaji wanaoijua hata harufu ya kondoo wao.

Wakati Baraza la Kipapa kwa ajili ya mawasiliano linafanya mkutano wao mkuu kuanzia tarehe 19 hadi tarehe 21, Septemba 2013, rais wa Baraza hilo anasema papa Francisko anatoa changamoto kwa Kanisa kuukumbatia mwuono mkubwa wa kusafiri kwa pamoja na jumuiya ya binadamu kwenye safari ya maisha ya hapa duniani. Mawasiliano yawe ni njia ya Mama Kanisa kukutana na wanae, kuwa karibu nao na kujadiliana kiaminifu katika kukumbana na changamoto za kila siku katika kuishi ukweli wa imani na maisha matimilifu.

Kwenye mkutano wake, Baraza la Kipapa kwa ajili ya mawasiliano ya Kijamii litaangazia namna mpya ya kuwasiliana inayoonekana kwenye maisha ya papa Francisko. Hili litafanyika ndani ya mada ya mkutano huo ambayo inalenga kuangazia Mitandao ya Mawasiliani na Kanisa.

Mada hii imetokana na changamoto iliyotolewa na baba Mtakatifu mstaafu Benedetto XVI kwenye ujumbe wake wa mwisho juu ya siku ya mawasiliano duniani ambapo aliongea kwa kirefu juu ya mitandao hiyo, na kuchangamotisha uwepo wa Kanisa kwenye mtandao wa internet, fursa mpya kwa ajili ya uinjilishaji.











All the contents on this site are copyrighted ©.