2013-09-18 14:10:15

Kanisa lahimizwa kuutangaza ukweli bila uficho


Kanisa lenye kujitenga na ulimwengu na mazingira yanayolizunguka si kanisa la Kimissionari. Na ukweli lazima uwe kiini cha mafundisho yote ya kanisa licha ya mazingira yanayolizunguka. Upendo na huruma ya Kikristo vinadai daima kuutangaza ukweli kwani bila huo Kanisa linaacha kuwa kanisa.
Haya ndiyo mawazo yaliyojitokeza kwenye tafakari ya Askofu Mkuu wa Dublin, Ireland, Mons. Diarmuid Martin alipokuwa akizungumzia wito na wajibu wa vyombo vya habari vya Kikatoliki nchini humo. Hii ilikuwa ni fursa kwake Askofu Mkuu Martin kuyamulikia maswala mawili ya uinjilishaji mpya, ambayo ni UJUMBE, na namna ya kuendeleza uinjilishaji mpya nchini Ireland.
Habari zilizochapishwa kwenye gazeti la kila siku la L’Osservatore Romano linalochapishwa mjini Roma, linamnukulu Askofu huyo akisema kwamba kanisa linavihitaji vyombo vya habari, haliogopi kumulikwa kwa kasoro ndani yake na kwamba linahitaji zaidi waumini kutiwa moyo wa kuendelea kwenye njia ya wongofu.
Gazeti hilo lilikuwa linamhoji askofu huyo kuhusu hasa wajibu wa waandishi wa habari na vyombo vya habari vya kanisa Katoliki na linagusia hasa muundo mbinu utafutao kusawazisha tamaduni jamii, kitu ambacho kinaonekana kuwaathiri hata waandishi wakatoliki ambao wanaonekana kuendeleza fedheha na machongelezo licha ya mema mengi ndani ya Kanisa.
Anasema Askofu Martin kwamba kanisa haliogopi kukosolewa, bali zaidi lina haja ya waandishi wanaowachangamotisha jamii ya waumini kuendelea kwenye njia ya wongofu, na kwamba kipaumbele cha kwanza cha Kanisa ni kuitangaza habari njema ya wokovu na kuhakikisha kwamba waumini wanapata malezi bora ya kiimani yaliyo kamili, matimilifu na ya kweli. Jambo la pili ni kuwaandaa waumini kuishi bila ya kuitilia shaka imani yao, na kuwajengea uwezo wa kuwa vyombo vya kuipeleka habari njema ya wokovu pote duniani, bila kuogopa kukumbana na tofauti za kitamaduni na zinginezo, hata kutoka kwa wale wasio kabisa na imani, huku wakijitahidi kuongoza na kuendeleza mazungumzo yenye kujenga, katika kutafuta mafao ya wote na ukweli. Hiyo ndiyo maana ya umissionari wa kanisa, kwani Kanisa kamwe haliwezi kujitenga na ulimwengu kwani limo ulimwenguni na mazingira ya kiulimwengu yanaliathiri kanisa kama vile yanavyoiathiri miundo mbinu yoyote ile kwenye jamii.
Uinjilishaji hudai kumtangaza wazi kabisa Kristo na habari njema ya wokovu. Hii ndiyo Kerygma au kiini cha ndani kabisa cha uinjilishaji kama inavooneakana kwenye mafundisho ya mitume. Bila hilo uinjilishaji huishia kuwa tendo la kiroho la kibinadamu na wala sio swala la kiroho ndani ya Yesu Kristo, aliye peke yake Mkombozi aliyekufa na kufufuka kwa ajili ya kumshuhudia Mungu ambaye ni upendo. Hivyo basi, haya yote yana kuwa na athari juu ya namna kiini cha Ujumbe wa uinjilishaji, ambacho ni Kristo, ujumbe wa upendo, unatangazwa. Ujumbe huo hauna budi kuwa kweli ujumbe wa upendo.
Askofu mkuu wa Dublin anamshukuru Baba Mtakatifu Mstaafu Benedicto wa XVI kwa kulisaidia kanisa la Ireland kujenga uhusiano na maeneo ya malezi ya Ireland ya kizazi kipya. Anaendelea kusema kwamba baba Mtakatifu Mstaafu Benedikto wa XVI na Baba Mtakatifu wa sasa Franscisko wameonyesha utayari wa kuzungumza na wanaume na wanawake wanaoishi na kulelewa kwenye tamaduni mamboleo, jambo ambalo linatia matumaini kwa dunia nzima, kwani uinjilishaji na mazungumzo lazima viambatane hata kama ni vitu viwili tofauti.
Askofu huyo ameutaja mjadala wa hivi karibuni kati ya Baba Mtakatifu Francisko na Eugenio Scalfari, mwandishi wa habari asiyemwamini Mungu wa gazeti maarufu la kila siku nchini Italia kama mfano wa uinjilishaji mpya, ambao unapaswa kuigwa na uandishi wa Kikatoliki. Amesema hii haimaanishi kufuata mkumbo bali kuwa na uwezo wa kuonyesha hasa sura halisi ya Kanisa katika ulimwengu mamboleo.

K







All the contents on this site are copyrighted ©.