2013-09-16 15:06:41

Ni upendo pekee wa Mungu unaoweza kuziba pengo la maumivu moyoni linaoachwa na maovu ya binadamu


Msamaha una nguvu ya kipekee inayoweza kumwokoa binadamu na dunia kutokana na dhambi, na magonjwa mengine ya kimaadili na kiroho. Pia ni upendo peke yake unaoweza kujaza utupu na pengo ambalo huachwa na matendo maovu kwenye moyo na historia ya mwanadamu.

Ni maneno ya Baba Mtakatifu Francisko kwenye mahubiri yake siku ya Jumapili wakati wa Sala ya Malaika Malaika wa Bwana kwenye uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro, Mjini Vatican.

Akigusia masomo ya Jumapili na hasa Injili ya Mtakatifu Luka 15, papa alielezea kwa kina msamaha wa Mungu unaolinganishwa na hadithi tatu kwenye injili hiyo. Nazo ni juu ya Kondoo aliyepotea, Shilingi iliyopotea, na ile ya mwana Mpotevu – ambayo inaonyesha baba na watoto wake wawili, mwana mpotevu, na yule aliyejifikiria kuhesabiwa haki, kuwa mtakatifu.

Methali zote tatu, anasema Papa, zinagusia hasa furaha ya Mungu itokanayo na msamaha. Furaha ya Mungu ni kusamehe, anakazia Baba Mtakatifu Francisko. Ni furaha ya mchungaji anayempata kondoo wake aliyepotea, furaha ya mama anayeipata shilingi yake iliyokuwwa imepotea, na furaha ya Baba, anampata mtoto wake aliyekuwa amepotea, aliyekuwa kama mfu, na sasa amepata tena uhai, amerudi nyumbani.

Ni upendo pekee unaoweza kutoa msamaha wa aina hii na kufurahia matunda yake, anasema Papa, kwani sio jambo la hisia tu, bali nguvu ya kiroho itokanayo na Mungu mwenyewe.

Anaendelea kuwa kila mwanadamu anajipata kwenye nafasi ya yule kondoo aliyepote, ile shillingi iliyopotea, na hata kwenye nafasi ya mwana anayekatalia mbali uhuru wake halisi wa kuwa mwana mpendwa na kufuata sanamu za uongo, vionjesho vya furaha, ambavyo vinamfanya kupoteza kila kitu.

Habari njema anayoitangaza kwa maneno haya Baba Mtakatifu Francisco ni kwamba Mungu hamsahau au kumtupa hata mmoja wa wana wake wapenzi, kwani Mungu ni Msamaha, na Mungu ni Upendo, ukweli ambao mwanadamu anaushuhudia kutokana na kujifanya kwake mtu, ndani ya nafsi ya Yesu Kristu.

Japo Mungu hamsahau mja wake, Mungu huheshimu uhuru wa mtoto wake, huku akimsubiri kwa mapendo makuu amrudie yeye Baba yake. Naye Mungu aliye mwaminifu humpokea tena kwa furaha kubwa, kila amrudiaye kwa moyo mkunjufu. Nao moyo wa Mungu hufanya shangwe.

Hata hivyo, anakazia Baba Mtakatifu kwamba changamoto kubwa ni kwamba mwanadamu hujiona kuwa mwenye haki daima na kuwahukumu wengine, na hata kumhukumu Mungu mwenyewe. Mwanadamu anapofikiri kwamba ni jukumu la Mungu kuwaadhibu na kuwahukumu kufa wenye dhambi badala ya kuwasamehe, anaingia kwenye hatari ya kubaki nje ya nyumba yake Baba, kama alivyofanya kijana mkubwa kwenye injili ya Jumapili. Badala ya kuingia ndani na kufurahia kurudi kwa mdogo wake anamkasirikia Baba yake ambaye anamkaribisha na kumfanyia sherehe mdogo wake.

Anaonya baba Mtakatifu kwamba mwanadamu huenda akakosa fursa ya kuungana na Mungu kikweli kama anakosa moyo wa huruma, kwani furaha ya msamaha haiwezi kuwa kwenye moyo usio na huruma, hata kama mhusika anafuata amri zote, kwani ni upendo tu, unaoweza kuokoa, sio tu kufuata maagizo. Ni mapendo kwa Mungu na kwa jirani ambayo yanakamilisha amri na sheria zote.

Baba Mtakatifu anawachangamotisha wanaojisikia kuwa wenye makosa makubwa kwamba hakuna dhambi zisizoweza kusamehewa na Mwenyezi Mungu na kwamba ni muhimu kukuza moyo wa kuwasamehe wengine ili kuweza kuupokea pia msamaha utolewao kwa kila mwanadamu.











All the contents on this site are copyrighted ©.