2013-09-11 16:02:42

Ombi la vijana wa Ulaya kwa serikali zao


Vijana wa ulaya wanawataka viongozi wa serikali zao kushirikiana nao kikamilifu kwenye jitihada za kutafuta suluhisho katika swala la ukosefu wa ajira.

Hili ni ombi la kundi la vijana 350 wawakilishi wa vijana kutoka nchi mbalimbali za bara la ulaya waliokusanyika nchini Ubelgiji kwenye mkutano wa vijana ulioandaliwa na bunge la Umoja wa Ulaya.

Vijana hao wameuomba Umoja wa Ulaya kushirikiana nao kwani wao wanajiona kama suluhisho la kuaminika kwenye maswala ya kielimu, ukosefu wa fursa za kazi na maswala mengineyo ya kijamii, ikiwa tu watahusishwa kwenye maisha ya ujenzi wa jamii na maamuzi ya kisiasa. Nao wamesema wako tayari kuvitumia vipaji vyao vingi na uwezo wa kufikiria kwenye uvumbuzi na ujasiria mali kwa manufaa ya bara zima la Ulaya.

Kwake Mgr Omella, Askofu wa jimbo la Calahorra y La Calzada-Logroño (Spain), ukosefu wa ajira kwa vijana ni donda kwenye soko huria linalosababisha myumbo uchumi. Mons. Omella alizungumzia juu ya hali ya vijana nchini Uhispania na akasema kwamba kuna umuhimu wa mbinu mkakati ili kuweza kulitatua tatizo hilo, na hasa katika kutoa elimu ifaayo hasa kwenye shule za ufundi ili kuwawezesha vijana kuwa na mbinu za kuwasaidia kwenye kazi au za kuandikwa au za kujiandika wao wenyewe, huku akisema kwamba tendo la vijana wengine kuacha shule ili kutafuta ajira sio suluhisho kwani elimu ni muhimu katika utendaji wa kazi za aina yote kwenye jamii.

Naye Sarah Prenger, Mratibu wa Shirika la Vijana Wafanyakazi Wakristo barani ulaya aliongelea changamoto zinazowakabili vijana wa ulaya na mikakati iliyopo ya kuwasaidia kuweza kuyamudu maisha yao.

Mengine yaliyojitokeza kwenye kikao hicho ni pamoja na umuhimu wa kuwategemeza vijana na kuhakikisha kuna mbinu za ushirikiano kati yao. Mkutano huo pia umezisifu kazi za vijana kote ulimwenguni na moyo wao wa kujenga utamaduni wa kimataifa. Akiongea kwenye mkutano huo, Padre Msalesiano wa Don Bosco, Yohanne D’Andrea amesema kwamba swala la elimu ya kufaa kwa vijana ni swala linalotoka kwenye undani wa moyo, kwani linakumbatia malezi ya kiutu na kimaadili ya mtu mzima, mwili na roho.

Mkutano huo uliandaliwa na wanabunge la Ulaya, Patrizia Toia (S&D) na Thomas Mann (EPP) – wakisaidiana na Konrad-Adenauer-Stiftung, Rete Juventutis, Wasalesiani wa Dono Bosco Ulimwenguni, na COMECE. Waandalizi wa mkutano huo sasa wanawataka viongozi wa kitaifa, pamoja na umoja wa ulaya kwa ujumla kuwasikiliza na kuwahusisha vijana kwenye sera na mikakati ya kuliendeleza bara hilo. Wamewaalika pia vijana kuanzisha juhudi za pamoja kwa ajili ya kuyakusanya mawazo yao na kuyawasilisha wakati wa uchaguzi wa bunge jipya la ulaya mwezi Mei 2014.












All the contents on this site are copyrighted ©.