2013-09-07 11:02:39

Siku ya Kimataifa ya Kumuenzi Mwenye Heri Tereza wa Calcutta


Mama Kanisa ana furaha tele kutokana na tendo la Umoja wa Mataifa kuingiza kwenye kalenda yake, kwa mara ya kwanza kabisa, siku ya Kimataifa ya matendo ya huruma, au International Day of Charity kwa lugha ya kimwombo. Hii ni siku itakayoadhimishwa kila mwaka ifikapo tarehe 5 mwezi Septemba.

Askofu mkuu Francis Chullikatt, Mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Umoja wa Mataifa, anasema kwamba Mama Kanisa analichukulia tendo hilo kama alama ya kumuenzi Mama Teresia wa Calcutta aliyefariki dunia mnamo tarehe 5 mwezi Septemba mwaka 1997, na ambaye matendo yake ya huruma yaliugusa ulimwengu mzima kama ishara ya upendo mkuu wa kujitoa mwenyewe bila ya kujibakiza kwa ajili ya ndugu zake waliokuwa wanasukumizwa pembezoni mwa jamii.

Kwa kumuenzi hivi mama Teresa wa Kalkutta, Mons. Chullikatt anasema kuwa ni ishara ya Umoja wa mataifa pia kuzithamini kazi za huruma zinazoendeshwa na Kanisa Katoliki kote ulimwenguni kwa manufaa ya wote wanaosahauliwa na jamii na kusukumizwa pembezoni mwa jamii.

Askofu huyo pia amesema kwamba nia ya kanisa katoliki kuonyesha mapendo kupitia matendo ya huruma ni kumfuasa Kristo mwenyewe aliyejitolea hata kufa juu ya msalaba kwa ajili ya ndugu zake, na hivyo kuwaonyesha namna ya kupenda wote wenye kumfuasa.

Itakumbukwa kwamba Mama Teresa wa Calkutta mwenyewe alisema mara nyingi kwamba kazi aliyokuwa akifanya haikuwa ya kijamii, au Social work, bali ilitokana na maisha ya tafakari yake ya ndani sana kama mtawa, na iliugusia hasa mwili wa Kristo, ndani ya ndugu zake.

Mama Teresa alitunukiwa tunu ya Nobeli ya Amani hapo tarehe 11.12.1979, kutokana na kazi zake za kijasiri na moyo wa mapendo makuu.

Kulingana na Mons. Chullikat kanisa Katoliki ndilo shirika kubwa zaidi lisilo la kiserikali duniani linalotoa huduma nyingi zaidi hasa za kielimu na kiafya. Zaidi ya asilimia 26 ya huduma zote za kiafya duniani hutolewa na Kanisa Katoliki. Naye mama kanisa hutoa huduma hizo sio kama sehemu ya kazi za kijamii, bali kama sehemu ya kazi zake za kichungaji zinazotokana na mapendo ya Kikristo yabubujikayo kutoka moyoni na yanayowakumbatia wengine kama zawadi kutoka kwa mwenyezi Mungu.









All the contents on this site are copyrighted ©.