2013-09-07 11:28:14

Kampeini ya WCC dhidi ya ufisadi...


Baraza la Makanisa Ulimwenguni (WCC) linawataka wafuasi wake kujiunga na kampeni ya kimataifa kwa ajili ya kusitisha ufisadi, dhambi ambayo inawaathiri hasa maskini. Takwimu zinaonesha kwamba kila mwaka zaidi ya dolla trilioni moja za kimarekani hupotea kutokana na rushwa, ufisadi na ukwepaji wa kodi.

Kampeni ya kimataifa dhidi ya ufisadi imepanga matukio kadhaa kwa ajili ya wiki ya tarehe 14 hadi 20 Octoba 2013. Mwito huu ambao umepewa jina Exposed 2013, utawahamasisha watu kote duniani dhidi ya uovu wa ufisadi. Kampeni hii inaongozwa na kundi la wakristo lijulikanalo kama Micah Challenge International. Jina la kundi hili linatokana na kifungu cha Mika 6:8 – “Bwana anataka nini kwako, ila kutenda haki, na kupenda rehema, na kwenda kwa unyenyekevu na Mungu wako!”

Kampeni hii inatarajia kuandaa vigilia ya zaidi ya 2000 sehemu mbalimbali za dunia kwa ajili ya watu maskini. Mbali na vijilia, kikundi cha Micah Challenge International kinatarajia kukusanya sahihi milioni moja wakati wa kampeni hiyo na kuwasilisha sahihi zingine milioni moja kwenye mkutano mkuu wa nchi maskini duniani au G20 utakaofanyika mwezi Novembar 2014.


Naye katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Kasisi Olav Fyske Tveit anasema kwamba Baraza la Makanisa Ulimwenguni limeamua kujihusisha na kampeni hii kwa kufuata mwito wa Mungu wa kuwapendelea na kuwa karibu zaidi na watu maskini. Kasisi Olav Fyske Tveit anasema kwamba ufisadi unaendelezwa na miundo mbinu ya kiuchumi, kitamaduni na kimaadili ambayo inaongozwa na ubinafsi na uchu wa mali, na utajiri wa haraka. Pia makundi ya kisiasa na hata viongozi na watu binafsi wanao mchango wao katika kuendeleza ufisadi kwenye jamii. Hivyo ni wajibu wa kila mmoja kushiriki kwenye juhudi za kuipinga miundo mbinu hiyo ambayo inaendeleza unyanyasaji wa watu wengi, na kwamba ni katika kuishika haki ya kiMungu tu dunia itakapoweza kukabiliana vilivyo na donda sugu la ufisadi.
Amesema Kasisi Tveit kwamba Exposed 2013 ni juhudi muhimu inayoenda sambamba na jitihada za Baraza la Makanisa la kuwa karibu na makanisa mahalia kwenye jitihada zao za kuupinga unyanyasaji wa kiuchumi. Malengo ya kampeni ya Exposed 2013 pia yanalingana na mada ya mkutano mkuu ujao wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni, utakaofanyika mjini Busan, Jamhuri ya Korea mnamo October 30, 2013 hadi Novemba 8, 2013.
Programu ya Baraza la Makanisa Ulimwenguni inayoshughulikia maswala yanayohusiana na umaskini, mali na Mazingira hushughulikia pia biashara inayozingatia haki, unyanyasaji wa kiuchumi, heshima kazini, na maadili ndani ya dunia ya utandawazi.









All the contents on this site are copyrighted ©.