2013-09-03 08:35:11

Mwaliko maalum wa kuombea amani Mashariki ya kati.


Wakristo duniani kote wanaalikwa hapo Jumamosi tarehe saba (07.09.2013) kuwaombea waathirika wa vita na migogoro inayoendelea huko Syria na nchi nyingine za Mashariki ya kati. Ni mwaliko uliotolewa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa sala ya Malaika wa Bwana siku ya Jumapili alipokutana na kusali na maelfu ya waumini kutoka sehemu mbalimbali za dunia. Baba Mtakatifu ameiomba jumuiya ya waumini, kupitia kwa Mama Bikira Maria, Malkia wa Amani, kusali, kufunga na kujinyima kwa ajili ya nchi ya Syria na mashariki ya kati kwa jumla.

Na hapa jijini vatikani, siku hiyo ya tarehe 7, kwenye uwanja wa kanisa kuu la Mt. Petro, kuanzia saa moja jioni hadi saa sita usiku (kwa majira ya kiitalia) waumini watakusanyika na kuunganika kwa sala, moyo wa toba na makesha maalum kwa nia hiyo ya kuomba amani Syria, Mashariki ya kati na kote duniani.

Akitoa mwito huo, Papa Fransisco amesema kwamba dunia inahitaji kuona vitendo vya mshikamano wa sala na kusikia maneno ya kutia moyo na yenye kuleta amani.

Makanisa mahalia na watu wote wenye mapenzi mema wameombwa kuandaa mikutano ya sala siku hiyo ya tarehe 7 Septemba ambayo ni siku ya vigilia ya kuzaliwa kwake mama Bikira Maria, inayoadhimishwa na Mama kanisa kila mwaka ifikapo tarehe 8 Septemba. Ni mwaliko kumwomba Mama huyu aliye Malkia wa Amani kuisaidia dunia kujenga kila siku, utamaduni wa amani na mazingira ya amani yaliyo muhimu kwa mafao ya watu wote duniani.











All the contents on this site are copyrighted ©.