2013-08-27 14:26:07

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 22 ya Kipindi cha Mwaka wa Kanisa


Ni Dominika nyingine tunakutana katika safari ya wokovu tukijaribu kusifu jina la Bwana kwa njia ya tafakari ya Neno lake. Ni Dominika ya 22 ya mwaka C. Mama Kanisa atupa chakula ndilo Neno la Bwana akisema Unyenyekevu ndiyo iwe dira ya maisha yetu kwa ajili ya kujipatia zawadi yakushiriki maisha ya Kimungu na heri ya Watakatifuwa mbinguni.

Mpendwa mwana wa Mungu Tukitaka kweli kuupata uzima wa milele ni lazima kujijengea uadilifu na unyoofu wa moyo unaojitokeza katika unyenyekevu. Kunyenyekea ni kutumaini yote katika Bwana aliye mkuu kuliko vitu vyote na kwamba katika yeye kuna msamaha wa dhambi na hatimaye uzima wa milele. Baada ya kutekeleza jambo basi mmoja lazima aingie katika kutenda kwa maana Mtakatifu Yakobo asema, imani bila matendo ni bure. Ndiyo kusema kuhangaikia kundi la wasiojiweza, wasio na chakula, tuseme walio ns shida mbalimbali katika maisha yao ambao kwa sababu hiyo mfumo jamii umewasukumiza mbali.

Mpendwa msikilizaji katika Injili ya Dominika hii Bwana yuko katika sherehe katika nyumba ya Mfarisayo mmoja ambaye amewaalika watu kadhaa kwa ajili ya kusherehekea pamoja. Anatoa fundisho kuhusu unyenyekevu , fundisho hili linawalenga watu wa aina mbili: mwenye sherehe na wale walioalikwa katika sherehe. Kwa mwenye sherehe fundisho linagota bila kuchelewa akisema unapofanya sherehe ndugu yangu usiwaalike wale ambao wanaweza pia kufanya kama ulivyofanya na hivi wakakualika! Bali waalikeni wale ambao kwa namna yoyote hawataweza kufanya hivyo.

Jambo hili linagusa mara moja maisha yetu, yaani mara kadhaa tumejenga urafiki na watu ambao kwa namna fulani wanalipa kama wasemavyo vijana leo. Huu ni urafiki ambao umepimwa katika mantiki ya kimahesabu, yaani nipe nikupe! Kwa namna hiyo tendo la kujitoa liko katika mmonyoko kwa maana bila nipe hakuna msaada au tuseme upendo usiodai faida. Mfumo wa maisha ya kikristu au maisha ya kawaida umeingiliwa na kirusi.

Wakati fulani kirusi hiki huingia katika imani na hata kuweza kufikia kusema kuwa Mungu anatupa zawadi mbalimbali kwa sababu tumefanya jambo fulani. Jambo hili lazima kulitazama kwa umakini, Mungu si nipe nikupe bali ni upendo mkamilifu ambao hujitoa pasipo kutarajia malipo.

Mpendwa msikilizaji sehemu ya pili ya fundisho la Bwana inaelekezwa kwa wale walioalikwa katika sherehe. Bwana anaona kila mmoja anahangaika kujipatia nafasi ya mbele, kwa namna yoyote katika mantiki ya kutaka kuonekana. Kila mmoja anaonesha ubinafsi wake katika sherehe hiyo. Bwana anasema ni vema na vizuri kuchukua viti vya nyuma ili basi kama unastahili utaalikwa kwa viti vya mbele.

Bwana hakemei kwa mtindo wa mauzi bali anasema ni vema tukatambua kuwa wale wa kwanza watakuwa wa mwisho na wa mwisho watakuwa wa kwanza. Wale wanaojishusha watakwezwa na vivyo hivyo kinyume chake. Kumbe wajishushao wataweza kushiriki kile chakula cha ufalme wa mbinguni. Kwa hakika hiyo sherehe yataka kuwakilisha sherehe ya uzima wa milele mbinguni.

Kwa ajili ya kuingia katika chakula hicho yatudai unyenyekevu na hekima. Kama nitachagua viti vya mbele maana yake tayari ninacho kila kitu katika utawala wangu na sihitaji tena msaada wa mtu mwingine kwa hivi nitakuwa nimemaliza safari yangu hapahapa!

Nina kila kitu katika maisha haya. Nikichagua njia ya kukaa nyuma maana yake basi mwenye sherehe atanivuta na kunisogeza mahala pazuri kumbe kuna kupiga hatua zaidi. Haya yanagusa yule mwalikwa. Kuhusu mwenye sherehe sharti ni moja kuwaalika wale wasiojiweza, waliosukumizwa pembezoni mwa jamii kwa ajili ya kujipatia tiketi ya kuweza kuingia katika ufalme wa mbinguni.

Tumsifu Yesu Kristo.

Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.