2013-08-27 11:14:19

Pandeni miti kumuenzi Papa Francisko


Wakristo nchini Kenya wamehimizwa kuanza kupanda miti kwa matayarisho ya kuisheherekea sikukuu ya Mtakatifu Fransisko wa Assisi hapo tarehe 4 Oktoba 2013. Haya yamesemwa hivi karibuni na Padre Hermann Borg.

Padre Borg aliashiria kuwa Mtakatifu Francisko ni mfano bora kwa Wakristo popote duniani na akamsifu Baba Mtakatifu Francisko kwa kumuenzi Mtakatifu Francisko wa Assisi kwa kuchagua jina hili ambalo lina changamoto nyingi katika: kusimama kidete kutetea misingi ya amani, utunzaji bora wa mazingira na huduma makini kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Padre Borg amewahimiza watu binafsi na vikundi; jumuiya za akina mama, vijana pamoja na wanafunzi kushirikiana kwa pamoja ili kupanda miti kwa wingi kwani ilikuwa ni fadhila ya Mtakatifu Francisko kupenda, kuthamini na kuyatunza mazingira. Alizichangamotisha jumuiya za watawa, shule, hospitali, taasisi za elimu ya juu na vyuo vikuu kujiunga kwenye zoezi hili makini ambalo linanuia kuzishirikisha Parokia zote kwenye majimbo yote nchini Kenya kupanda miti kama njia ya kumuenzi Baba Mtakatifu Francisko kwa vitendo!

Ili kuonyesha umoja na ushirikiano kwa ajili ya mafao ya wengi Padre Borg anawaalika pia waamini wa dini zingine kushiriki kwenye zoezi hili la kupanda miti ili kudumisha amani miongoni mwao, kwani ilikuwa sala kuu ya Mtakatifu Fransisko kuona kila mwanadamu akiwa chombo cha amani.

Alisema ushirikiano wao utaimarisha hata juhudi zao za pamoja kwa ajili ya kuiendeleza amani duniani kote, kwani dunia ina uhitaji mkubwa wa umoja, amani, upendo na mshikamano na kwamba, Wakatoliki na Wakenya wote kwa ujumla wao wanaweza kuwa chanzo cha amani hiyo kwa kuanzia na zoezi la kupanda miti. Alinukuu mafanikio makubwa ya makundi yaliyokuwa ndoto ya mtu mmoja au watu wachache na hatimaye, yakaweza kuwaunganisha watu wengi kutoka sehemu mbalimbali za dunia.

Makundi haya, ambayo yangeweza kuigwa hata kwa zoezi la kumuenzi Mtakatifu Fransisko wa Asisi hapo tarehe 4 Oktoba 2013 ni kama vile Green Belt Movement ya hayati Prof. Wangari Maathai na mikutano mikuu miwili iliyofanyika nchini Kenya mnamo 2007 ambayo ni ule wa Umoja wa Mataifa juu ya Mazingira na Jukwa la Masuala ya Kijamii.








All the contents on this site are copyrighted ©.