Jimbo Katoliki Mbeya lakabidhiwa ardhi kwa ajili ya ujenzi wa Chuo cha Wauguzi
Kama wasemavyo wahenga kuwa machozi ya mtu mzima hayaendi bure ndivyo ilivyotokea
kwa Askofu Evaristus Marcus Chengula wa Jimbo Katoliki Mbeya kwa Serikali ya Mkoa
wa Mbeya kuhusu ardhi ya Kijiji cha Lupata aliyoanza kuililia tangu mwaka 2009 kwa
ajili ya kuwasaidia watanzania kwa kujenga Chuo cha Uuguzi na Uganga bila mafanikio,
lakini kweli Mwenyezi Mungu hamtupi mja wake, hatimaye, kilio hicho kimesikika baada
ya kukabidhiwa rasmi ardhi hiyo na Mkuu wa Wilaya ya Rungwe.
Askofu amewahi
kutoa kilio hicho kwa Serikali na kuhoji sababu ya kukwama kwa mchakato huo hata
alidiriki kusema endapo ardhi hiyo ya Mungu imekuwa na mlolongo mkubwa kwa maneno
yaliyozoeleka serikali kuwa ' mchakato' unaendelea basi itafika wakati Kanisa litahamishia
ujenzi wa Chuo hicho cha Uuguzi na kupeleka maeneo mengine yenye kiu ya maendeleo
endelevu.
Askofu Chengula alitoa kilio chake katika Jubilei ya 50 tangu kufunguliwa
kwa Hospitali ya teule ya Wilaya ya Igogwe inayomilikiwa na Jimbo katoliki la Mbeya,
ambapo mgeni rasmi katika Maadhimisho hayo alikuwa Mkuu wa wilaya ya Rungwe Bwana
Chrispin Meela. Alimhakikishia Askofu Chengula na kumwambia kwamba, atakipata kipande
.
Akizungumza katika Jubilei hiyo Bwana Meela alisema baada ya kusikia mahubiri
ya Askofu kutoa kilio chake kwa uchungu aliona ipo sababu ya kufanya haraka kufuatilia
suala hilo na kulikamilisha na hivyo baada ya kupitia nyaraka za awali na kupata matokeo
ya tume ya uchunguzi iliyoundwa na Katibu tawala wa Wilaya ya Rungwe aliamua kutoa
ardhi kwa niaba ya Rais Jakaya Mrisho Kikwete ambaye ndiye mwenye ardhi kikatiba.
Alisema
kazi yake kubwa kama Mkuu wa Wilaya ni kusimamia haki na sheria na kwamba katika suala
la ardhi hiyo aliangalia taratibu zinasemaje na baadaye alichukuwa maamuzi baada ya
kupima manufaa ya suala lenyewe kwa umma anayoiongoza.
"Nyaraka zilionesha
kuna ubabaishaji mwingi kwa sababu taratibu zote za kutuma maombi zilifuatwa kuanzia
ngazi ya Kijiji, nikaona Rungwe tuna upungufu wa wauguzi 128, nikaona Chuo kitakuwa
mkombozi katika zahanati na vituo vya afya ambavyo vina upungufu mkubwa wa wataalamu
kwa hiyo ninakukabidhi ramani hii Baba Askofu anzeni mara moja kujenga baada ya Desemba
22 watakapokuja watu wa upimaji na ahadi ya Watoto wa Kijiji hiki na Rungwe kwa ujumla
kupewa kipaumbele usisahau,"alisema Mkuu wa Wilaya.
Hayawi hayawi yamekuwa
ndivyo ulivyokamilika msemo huo hivi karibuni baada ya wakazi wa Kijiji cha Lukata
Kata ya Kinyara,wilayani Rungwe kukabidhi rasmi ardhi yenye ukubwa wa ekari zaidi
ya 5 kwa Askofu Chengula kwa ajili ya kujenga Chuo cha Wauguzi katika Hospitali Teule
ya Igogwe inayomilikiwa na Jimbo Katoliki Mbeya
Tukio hilo limefanyika katika
eneo lililopo jirani na Hospitali hiyo ambapo Katibu wa Hospitali Japhet Kalindu,
Mganga Mkuu Dr. Oyeti Mwakosya na viongozi wa Chama na serikali wakiwemo machifu walihudhuria
na kushuhudia makabidhiano hayo na kupita kuweka alama ya mipaka.
Ninakumbuka
kauli ya Mkuu wa Wilaya wakati wa jubilei ya Hospitali hiyo alimwambia Askofu kuwa
katika Wilaya yake anao mzigo mkubwa wa wanafunzi zaidi ya 4,000 kati ya 5,000 waliomaliza
kidato cha nne mwaka jana ambao wapo wanazurula mitaani baada ya kuchaguliwa wanafunzi
800 kati yao kuendelea na kidato cha tano.
Awali Mganga Mkuu wa Hospitali ya
Igogwe,Dkt.Mwakosya alisema chuo kinatarajia kuanza na wanafunzi 90 wa ngazi ya cheti
kutokana na mipango ya serikali na wanatarajia kuendelea kutoa kozi za ngazi ya stashahada
na shahada kwa wauguzi na kwamba ujenzi wa chuo ni faraja kwa Wilaya na Jimbo Katoliki
la Mbeya.
Wakizungumza baada ya kukabidhiwa eneo hilo kwa niaba ya Askofu
Chengula wa kanisa Katoliki Jimbo la Mbeya ambaye ndiye mmiliki wa Hospitali ya Igogwe,Mganga
mkuu Dkt. Mwakosya na Katibu wa afya,Kalindu waliwashukuru wananchi kwa kukubali kulitoa
eneo hilo ambalo baada ya kuliomba lilizuwa mgogoro na hivyo kukwamisha mikakati ya
ujenzi wa chuo cha uuguzi tangu mwaka ya 2009.
Hata hivyo baadhi ya viongozi,chifu
mkuu na wananchi wa Kijiji cha Lukata wameelezea furaha yao huku Mratibu Elimu Kata
ya Kinyala ambaye alikuwa anatuhumiwa kuwa miongoni mwa wananchi tisa wa Kijiji hicho
waliokuwa wakipinga Hospitali ya Igogwe kugawiwa eneo hilo akitamka kuwa hana kinyongo
na eneo hilo huku akiwatania wazee wa jadi wamlinde na hatari yeyote inayohusishwa
na imani za kishirikina.