2013-08-26 10:30:42

Uongozi ni dhamana nyeti!


Ole wenu Waandishi na Mafarisayo..

Somo la Injili : Mt 23:13-22. Tafakari ya Jumatatu, tarehe 26 Agosti, 2013

Leo Bwana wetu Yesu Kristo anachagiza uongozi wo wote katika jamii. Tabia ya uongozi mzuri wa watu ni kujiwekea utaratibu wa kujipima utendaji wake. Kujiwekea nidhamu ngumu ya kujikosoa na kupokea kwa radhi vipindi au wakati wa kukosolewa. Gwiji la falsafa ya Wagiriki aliyeishi miaka 500 kabla ya Kristo - Socrates aliwahi kusema, maisha yasiyotafakariwa au yasiyo na kujichunguza, hayafai kuyaishi (unexamined life is unworthy living). Na kipimo sahihi cha kujipima ni watu wetu, familia zetu, na wateja wetu.


Katika ofisi za serikali au makampuni kuna mtindo wa kuweka masanduka ya maoni (suggestion boxes). Yesu naye alitumia "suggestion box" alipokuwa na mitume wake Kaisarea Filipi (Mt 16:13-17), "..watu wanasema mimi ni nani?" Tusipoweka utaratibu wa kupimwa, tutapimishwa na watu wetu kwa lazima. Ingawa waswahili husema mtu mzima hagombwi - siku moja mtu mzima atatukanwa na anaowangoza kama Yesu alivyofanya leo kwa Waandishi (Mt 23:16) "..ole wenu viongozi vipofu.."

Bwana wetu Yesu Kristu anataka kutuambia nini leo :

1. Uongozi wo wote ule ni dhamana tuliyoichukua kutoka kwa Mungu na kwa watu tunaowaongoza. Daima waongozwa wanahitaji na wana matarajio ya kupata nafuu, hauweni, uzima tele (Yoh 10:10), huruma na msamaha. kutoka kwa uongozi wanataka kuonja kutetewa na kujaliwa. Yule anayeongozwa hujiweka chini kwa anayemuongoza kama kondoo au mtoto. Na ndio maana Mungu kwa kinywa cha nabii Ezekieli anasema, "mimi mwenyewe nitawachunga kondoo zangu.."(Ezek. 34:11-16). Jicho la kiongozi ni kujipima kama kweli unavyoongoza watu wako wanaonja unafuu katika maisha yao.

Baba au mama katika familia yako jipime mwisho wa wiki au mwezi - je watoto wangu wanajisikiaje wakiwa nami? Je, sipeleki ila sura ya ujemedari wangu wa jeshi (kama baba ni askari) kwa watoto wangu na mke wangu nyumbani? Hata kama wewe ni Brigedia jeshini - unaporudi nyumbani vya sura ya ubaba kwa na watoto wako. Watoto waseme toka moyoni "baba yetu.."na sio brigedia fulani.

2. Viongozi wakae na watu wao na wawasilize. Viongozi waonje shida zao, matatizo yao, hofu zao. Kiongozi mzuri ni msikivu wa daima, azijua sauti za kondoo wake. "..Kondoo husikia sauti yake, naye huwaita kondoo wake kila mmoja kwa jina lake.." (Yoh 10:3). Daima maamuzi mengi tunafanya kimakosa kwa kujisikiliza sisi wenyewe. Tunakuwa na mtindo wa "top bottom approach" katika Uongozi wetu. Tukumbuke daima tunaozeka nyumba ya nyasi, daima wale walio chini huona matundu mengi hivyo umsaidia mwezekaji nyumba kuifanya kazi yake vizuri.


Kwa kuwa kila mmoja wetu ni kiongozi kwa nafasi yake, tujiombee Jumatatu hii Roho wa Mungu atuumbe upya ili ndani ya familia zetu, jumuiya, parokia na kazi zetu tupate viongozi wa mfano wa Kristu mwenyewe.

Mtumishi wenu – Padre Benno Michael Kikudo
Jimbo kuu la Dar es Salaam.








All the contents on this site are copyrighted ©.