2013-08-24 10:40:01

Waamini wanafunga na kusali kwa ajili ya kuombea amani duniani!


Jumuiya ya Waamini wa Kanisa Katoliki nchini Tunisia, Jumapili tarehe 25 Agosti 2013 inasali kwa ajili ya kuombea amani, umoja na mshikamano wa kitaifa kwa nchi za Kiarabu ambazo kwa siku za hivi karibuni zimekumbwa na vita pamoja na machafuko ya kisiasa na kijamii, kiasi cha kusababisha mateso na mahangaiko makubwa kwa watu wasiokuwa na hatia.

Askofu mkuu Ilario Antoniazzi wa Jimbo kuu la Tunis, nchini Tunisia anasema kwamba, Kanisa linaendelea kufuatlia matukio ya ukosefu wa misingi ya haki, amani na mshikamano huko Mashariki ya Kati, kwenye nchi za Kiafrika na Kiarabu. Waamini wanapenda kutumia Jumapili kwa ajili ya kumpigia Mungu magoti ili kumlilia aweze kuwajalia tena zawadi ya amani, utulivu na mshikamano wote wanaoendelea kuteseka kutokana na vita.

Hii itakuwa ni siku ya kufunga na sala na kwamba, ni siku maalum iliyotengwa kwa ajili ya kuwakumbuka na kuwafariji wote wanaoteseka kutokana na vita. Ni matumaini ya Kanisa Katoliki nchini Tunisia kwamba, kwa maombezi ya Bikira Maria Malkia wa amani, Mwenyezi Mungu ataweza kuwasikiliza na kuwasaidia katika mchakato wa kutafuta amani ya kudumu sehemu mbali mbali za dunia.







All the contents on this site are copyrighted ©.