2013-08-24 08:33:50

Ujumbe kwa Maadhimisho ya Siku ya 87 ya Kimissionari Duniani 2013


Baba Mtakatifu Francisko ameandika ujumbe kwa ajili ya Maadhimisho ya Siku ya 87 ya Kimissionari Duniani, inayoadhimishwa tarehe 20 Oktoba 2013. RealAudioMP3
Itakumbukwa kwamba, kwa mara ya kwanza Siku hii iliadhimishwa kunako mwaka 1927 baada ya Papa Pio wa Kumi na moja kuridhia ombi lililokuwa limetolewa na Taasisi ya Uenezaji wa Imani.

Ikaamriwa kwamba, kila Mwaka, Jumapili ya Mwisho wa Mwezi Oktoba, itumike kwa ajili ya kuhamasisha shughuli na mikakati ya kimissionari ndani ya Kanisa Katoliki, ili waamini waweze kutambua na kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa maisha na utume wa Kanisa kwa kuchangia kwa hali na mali, kama kielelezo cha mshikamano wa kidugu na Makanisa mahalia ambayo yalikuwa yanaanza kupokea Ujumbe wa Habari Njema.

Ni siku ambayo inatumika kukusanya mchango kwa ajili ya kufadhili miradi na shughuli za kichungaji kwa ajili ya kuwaendeleza: Makleri, Watawa na Makatekista, ambao kimsingi ni wadau wakuu wa shughuli za Uinjilishaji unaogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili.

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa Maadhimisho ya Siku ya 87 ya Kimissionari Duniani anasema, Maadhimisho haya yanafanyika wakati huu Mama Kanisa anapokaribia kufunga Mwaka wa Imani, ambao umekuwa ni fursa makini kwa ajili ya kuimarisha urafiki na Kristo katika hija ya maisha ya Kanisa kwa kutangaza kwa ari, nguvu na ujasiri mkuu Injili ya Kristo.

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe huu anapenda kuangalisha mambo makuu manne: Imani ni zawadi yenye thamani kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu; Mwaka wa Imani, Vikwazo vya Uinjilishaji ndani ya Kanisa; Uinjilishaji kwa njia ya vyombo vya mawasiliano ya jamii na mwishoni himizo kwa kila mwamini kuwa ni mdau wa mchakato wa Uinjilishaji mpya.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, Imani ni zawadi yenye thamani kubwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu inayomwezesha mwamini kufungua akili na moyo wake, ili kumfahamu na kumpenda Mwenyezi Mungu, ili kujenga uhusiano wa dhati na hatimaye, kushiriki katika maisha ya Kimungu. Mwenyezi Mungu anawapenda watu wake, lakini anahitaji jibu makini na ujasiri wa imani, unaomwezesha mwamini kumwilisha pendo na kuonja huruma yake isiyokuwa na kifani.

Ni zawadi inayotolewa kwa wote, mwaliko kwa kila mtu kujisikia kwamba, anapendwa na kuthaminiwa na Mwenyezi Mungu, kwani hii ndiyo furaha ya wokovu. Ni zawadi shirikishi inayowachangamotisha waamini kuendelea kutangaza Habari Njema ya Wokovu, ili mataifa waweze kuwa ni wanafunzi wa Yesu, kielelezo makini cha ukomavu wa Jumuiya ya Kikanisa.

Baba Mtakatifu Francisko anasema, kila Jumuiya ina ukomavu kwani inakiri imani, inaadhimisha Liturujia kwa furaha, inaishi fadhila ya upendo na kutangaza Neno la Mungu bila kuchoka hadi pembezoni mwa Jamii, hususan kwa wale ambao bado hawajabahatika kumfahamu Kristo. Uthabiti wa imani katika ngazi ya mtu binafsi na Kijumuiya unajionesha katika uwezo wa kuieneza na kuwatangazia wengine; unamwilishwa katika mapendo, unashuhudiwa kwa wote wanaokutana nao katika hija ya maisha yao.

Baba Mtakatifu Francisko katika tafakari yake kuhusu Mwaka wa Imani anasema, Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican ni fursa makini kwa waamini kutambua kwa mara nyingine tena uwepo wa Mama Kanisa katika ulimwengu mamboleo na utume wake kwa watu na mataifa. Umissionari ni dhamana inayowaunganisha watu kutoka katika kila kabila, tamaduni na kila mwamini mmoja mmoja, kwani mipaka ya imani inapenya katika tamaduni na mioyo ya watu.

Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican umebainisha kwa kina umuhimu wa kupanua mipaka ya imani kwa kila mbatizwa na kwa kila Jumuiya ya Kikristo ili kila mtu aweze kutolea ushuhuda wa imani kwa Kristo na Kanisa lake. Ni wajibu wa kila Jumuiya kutafsiri wajibu huu kwa kuendelea kuwa ni wafuasi wa Kristo wakimshuhudia Kristo kwa watu wa mataifa kama kiini na utambulisho wao wa Kikristo. Waamini wote wanatumwa na Kristo kufanya hija pamoja na ndugu wengine, kwa kuungama na kushuhudia imani kwa Kristo na hivyo kuwa kweli ni watangazaji wa Injili.

Baba Mtakatifu anaialika Familia ya Mungu kutoa kipaumbele cha kwanza kwa ari na moyo wa Kimissionari inayopaswa kujionesha kwa namna ya pekee katika mikakati ya shughuli za kichungaji na malezi endelevu kwa kutambua kwamba, wajibu huu unakamilika kwa njia ya ushuhuda kwa Kristo mbele ya Mataifa na watu wote. Umissionari unagusa undani wa utume na maisha ya kila Mkristo.

Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba, wakati mwingine shughuli za Uinjilishaji zinapata vikwazo kutoka ndani ya Kanisa lenyewe: waamini wanakosa ari, furaha, ujasiri na matumaini ya kutangaza kwa wengi Ujumbe wa Injili ya Kristo pamoja na kusaidia kurahisisha mchakato wa watu wanaotaka kukutana na Yesu katika ulimwengu mamboleo. Dhana hii inapingana na matumizi ya nguvu kama njia ya kutangaza Injili ya Kristo, bali kutangaza kweli za Kiinjili na wokovu wa Kristo katika ukweli na uwazi pamoja na kuheshimu mawazo ya wengine.

Waamini wanachangamotishwa kuwa na ujasiri wa kuwashirikisha wengine furaha ya kukutana na Yesu kwa heshima, huku wakitambua kwamba, wao ni vyombo vya Injili. Yesu anaonesha njia na dhamana hii amewakabidhi wafuasi wake ili kuowaonesha wengine dira na njia ya kufuata sanjari na kuendelea kutangaza Injili hadi miisho ya dunia. Inasikitisha kuona kwamba, ukweli huu unachafuliwa kwa kukuza zaidi uhalifu na kashfa.

Umefika wakati kwa waamini kuhakikisha kwamba, wanatolea ushuhuda wa maisha adili ya Injili, kwa kuitangaza na kuishuhudia kwanza kabisa ndani ya Kanisa, kwa kutambua kwamba, haiwezekani kutangaza Injili ya Kristo pasi na Kanisa na kwamba, huu ni utume wa Familia nzima ya Mungu. Maadhimisho ya Liturujia, Neno la Mungu na Sakramenti zote hata katika maisha ya binafsi ni mchakato unaolishirikisha Kanisa zima kwa niaba ya Yesu mwenyewe. Hii ndiyo nguvu ya Kimissionari kwamba, Wamissionari kamwe wasijisikie wapweke, kwani wao ni sehemu ya Fumbo la Mwili wa Yesu, yaani Kanisa linaloongozwa na Roho Mtakatifu.

Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba, Waamini wanaishi katika ulimwengu wenye maendeleo makubwa ya vyombo vya mawasiliano ya Jamii vinavyorahisisha mchakato wa watu kuweza kukutana, kufahamiana na kushirikishana mang’amuzi; kuna mwingiliano mkubwa; watu wana fursa ya kushirikishana taaluma na mang’amuzi yao ya kitamaduni; utalii ni jambo jingine linalowasukuma watu kutembelea sehemu mbali mbali za dunia.

Licha ya maendeleo yote haya, wakati mwingine inakuwa ni vigumu kwa waamini kuweza kufahamiana, hali inaonesha kwamba, kuna idadi ya waamini wanaoendelea kupoteza imani yao; watu wasiojali au wanaovutika kwa urahisi na dini za watu wengine; wengine wameasi kabisa kiasi kwamba, kuna haja ya Uinjilishaji Mpya. Kuna idadi kubwa ya watu ambao bado hawajabahatika kusikia Habari Njema ya Wokovu. Ulimwengu unaendelea kushuhudia athari za myumbo wa uchumi kimataifa unaojionesha katika masuala ya fedha, uhakika na usalama wa chakula; mazingira, bila kusahau tunu msingi za maisha.

Maisha ya watu wengi yanaendelea kukabiliana na kinzani, hali inayosababisha ukosefu wa amani na usalama, changamoto ya kuendelea kutangaza kwa ari na ujasiri mkubwa ujumbe wa matumaini, upatanisho, umoja, ukaribu na huruma ya Mungu; wokovu pamoja na nguvu ya upendo wa Mungu kwa waja wake inayoweza kuvunjilia mbali nguvu za giza na hatimaye, kumwongoza mwanadamu katika kutafuta mafao ya wengi.

Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe wake kwa Maadhimisho ya Siku ya 87 ya Kimissionari Duniani kwa Mwaka 2013 anasema, mwanadamu anahitaji kutembea katika mwanga unaopatikana kwa kukutana na Yesu Kristo, changamoto kwa waamini kushuhudia mwanga huu kwa njia ya upendo na matumaini yanayobubujika kutoka katika imani.

Umissionari wa Kanisa ni ushuhuda wa maisha yanayoangazia njia inayowajalia watu matumaini na mapendo. Kanisa ni Jumuiya ya waamini wanaohamasishwa na nguvu ya Roho Mtakatifu ili kuishi na kuonja ile ladha ya maisha ya kukutana na Yesu Kristo, ili hatimaye, kuwashirikisha wengine mang’amuzi na furaha ya ndani ya Ujumbe wa Wokovu ulioletwa na Kristo. Roho Mtakatifu analiongoza Kanisa katika safari hii.

Baba Mtakatifu Francisko anawahimiza waamini wote kuwa ni wadau wakuu wa utangazaji wa Habari Njema ya Wokovu, lakini kwa namna ya pekee: Wamissionari wa zawadi ya imani, watawa na waamini walei wanaojitosa kimasomaso kwa ajili ya kutangaza Injili katika tamaduni na nchi tofauti. Anayashukuru Makanisa mahalia kwa mchango wao katika azma ya Uinjilishaji mpya kwa kuonesha ari na mwamko mpya wa Injili kwa Makanisa ya zamani. Ni utajiri mkubwa kwa kila Kanisa na Jumuiya kutoa Wamissionari, watambue kwamba, si kwamba, wanapoteza bali wanafaidika zaidi.

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika Maaskofu na Mashirika ya Kitawa na Kazi za Kitume kuwa makini katika wito wa kimissionari kwa watu wa mataifa kwa kusaidia Makanisa mahalia ambayo yana upungufu mkubwa wa Mapadre, ili kuimarisha utume na maisha ya Jumuiya ya Kikristo. Jukumu hili pia lishughulikiwe na Mabaraza ya Maaskofu Katoliki katika maeneo husika. Makanisa yaliyobahatika kuwa na utajiri mkubwa wa miito ya Kipadre na Kitawa yawe tayari kusaidia Makanisa ambayo yanaonesha ukata wa wahudumu wa Injili.

Wamissionari wajitahidi kuishi ile furaha ya kutoa huduma kwa Kanisa mahalia wanapotangaza imani na kuleta mwamko na ari kubwa zaidi kwa Makanisa mahalia kama njia ya kushirikisha imani kwa kuwawezesha wafuasi wa Kristo kutajirishana. Baba Mtakatifu anapongeza shughuli na mikakati inayotekelezwa na Mashirika ya kimissionari yanayohamasisha shughuli za kimissionari sehemu mbali mbali za dunia, kuendeleza dhamana hii katika majiundo ya waamini na Jumuiya zao, kwa kutambua pia umuhimu wa majiundo ya kimissionari kwa Familia ya Mungu. Jumuiya za Wakristo zioneshe moyo wa ukarimu na upendo kwa kujitoa kwa hali na mali katika kusaidia mikakati ya Uinjilishaji.

Baba Mtakatifu anahitimisha ujumbe wake kwa Maadhimisho ya Siku ya 87 ya Kimissionari Duniani kwa kuwakumbuka waamini wanaokumbana na mateso na madhulumu ya kidini sehemu mbali mbali za dunia, wasikate tamaa, bali Jumuiya ya Kimataifa ijitahidi kuhakikisha kwamba, hata wao wanapata haki msingi na uhuru wa kuabudu. Hawa ni mashahidi na wafia dini wa nyakati hizi, Mama Kanisa anatambua na kuthamini mchango wao. Baba Mtakatifu anawasihi waendelee kuwa waaminifu kwa Kristo naye anawasindikiza kwa sala na sadaka yake, watambue kwamba, Kristo ameushinda ulimwengu.

Maadhimisho ya Mwaka wa Imani iwe ni fursa ya kuimarisha urafiki na Kristo kwa kuwa na matumaini ya pendo kuu na endelevu kutoka kwa Kristo. Baba Mtakatifu Francisko anawatakia kheri na baraka Wamissionari wote wanaojitosa kwa ajili ya kutekeleza dhamana ya utangazaji wa Habari Njema ya Wokovu hadi miisho ya dunia, waonje furaha ya kutangaza Injili ya Kristo.

Ujumbe huu umehaririwa na
Padre Richard Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.








All the contents on this site are copyrighted ©.