Ndugu na Jamaa ya Mzee Nelson Mandela wameanzisha mtandao wa kijamii kwa heshima ya
Mzee Madiba, unaolenga kusambaza ujumbe wa amani na utulivu; haki na upatanisho; mambo
ambayo Mzee Madiba aliyapatia kipaumbele cha kwanza katika utawala wake kama Rais
wa Afrika ya Kusini.
Watumiaji wa mtandao huu wataweza kushirikisha wengine
ujumbe wa amani na upendo pamoja na kuweka picha zao kwa heshima ya Mzee Madiba, aliyesimama
kidete kupinga utawala wa ubaguzi wa rangi nchini Afrika ya Kusini. Huu ni mfano wa
kuigwa kwa viongozi wa nchi za Kiafrika kutoa kipaumbele cha kwanza kwa ajili ya ustawi
na maendeleo ya watu wao.
Mtandao huu umeanzishwa kunako mwezi Machi 2013
na kwa sasa una idadi kubwa ya wafuasi wanaoshirikishana habari kwa njia ya mtandao.
Baadhi ya watu wanasema, pengine huu ni ujanja wa kutaka kutumia jina kubwa la Mzee
Mandela kwa ajili ya mafao binafsi! Lakini wadau wa mtandao huu wanasema kwamba, lengo
ni kusambaza mawazo yatakayoliwezesha Bara la Afrika kucharuka kwa ustawi na maendeleo
ya wengi!