2013-08-23 07:51:42

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 21 ya Kipindi cha Mwaka C wa Kanisa


Ninakuleteeni kipindi tafakari Neno la Mungu masomo Dominika. Tayari tuko Dominika ya 21 ya mwaka C. Mwaliko toka Neno la Mungu: Jitahidini uingie katika mlango mwembamba ili upate kuokoka. RealAudioMP3

Katika Historia na ndivyo ilivyo Bwana wetu Yesu Kristo ndiye mlango mwembamba. Ili kuweza kuingia katika mlango huo mwembamba inatudai kujikaza na kuwa ushujaa wahali ya juu. Mlango mwembamba ni Neno la Mungu, ni upendo wa kimungu ambao lazima humfikie yule ambaye anaonekana hasitahili kufikiwa, ni Bwana ambaye anaenda Yerusalemu kwa ajili ya kupokea kikombe cha mateso na hatimaye kifo.

Ni kwa jinsi hiyo basi wokovu ni jambo la kuhangaikia. Kutokana na mahangaiko juu ya wokovu linakuja swali kwa Bwana likisema “Hivi ni wachache wanaokoka? Bwana atatoa jibu kwa namna tofauti. Jambo la msingi kwa Bwana si wangapi wanaokolewa bali ni kwa namna gani na kwa njia gani wanaokolewa!

Bwana anatoa fundisho lake akitumia mfano wa watu ambao wako mlangoni wakitaka kuingia ndani ya sherehe lakini hawawezi kuingia. Ilikuwa rahisi kwao kuingia mapema kwa kupitia mlango mwembamba lakini hawakufanya hivyo na hivi kwa mlango mkubwa Bwana amekwishajiandaa kufunga! Mlango mwembamba unawakilisha suala la kwamba si rahisi kupita umati bali mtu mmojammoja.

Kumbe haitoshi kuwa mmojawapo wa wanajumuiya ya Wakristo lazima kuwajibika. Mlango mwembamba ni chujio, kumbe anapita mmoja baada ya mwingine. Kumbe, wokovu ni jambo linalomgusa mtu mmoja katika uhalisia wake na mtu huyo katika uhuru kamili huchagua kuokoka. Ni kwa jinsi hiyo tunafikiria tena, kama mlango ni mwembamba basi ni kwa ajili ya wale ambao wanaweza kujiingiza katika hali ya ukubwa wa mlango, yaani kuwa katika vipimo halisi.

Si rahisi kuupanua huu mlango maanake umekwisha kuwekwa vivyo hivyo. Vipimo vyenyewe ni kumfuasa Bwana kwa kuitikia mashauri ya Injili.

Mpendwa msikilizaji kulikuwa na mwanafunzi mmoja analalamika kuwa chumba chake ni kidogo na hivi anakosa hewa, ni katika hilo mwalimu alimwambia kadiri utakavyojitahidi kuwa mdogo ndivyo ukubwa wa chumba utaongezeka. Fundisho la Bwana kuhusu uongozi lawezapia kutujuvya vema juu ya hili. Anayetaka kuwa mkubwa lazima awe kama mdogo anayetumikia. Katika Injili ya Mathayo 5:1-13 juu ya Heri Nane tunakutana na heri moja isemayo Heri waliomaskini wa roho maana ufalme wa mbinguni ni wao. Hii yatufundisha kuwa katika chumba cha sherehe wanaingia wale tu ambao umaskini wa roho umewafanya wawe wepesi!

Mpendwa msikilizaji, umesikia watu waliokuwa nje ya mlango mkubwa wakisema: sisi tulikula na kunywa pamoja nawe, hili tatizo ambalo latuonesha kuhangaikia mambo ya kula na hivi kujenga miili ambayo inashindwa kupita katika mlango mwembamba na matokeo yake lazima kusubiria mlango mkubwa ambao haiwezekani kupita kwa sababu umati ni mkubwa na hivi inafika muda Bwana harusi anafunga.

Unene huu si wa kimwili bali ni unene katika fikira za kidunia: rushwa, unyanganyi, uongozi mchafu na mambo kama hayo. Haya yote yazuia mtu asifike katika mlango mwembamba.

Bwana katika sehemu ya pili ya Injili anataja makundi ambayo yatakuwa yameketi chakulani pamoja na Bwana yaani toka pande zote za dunia. Hawa ni wale katika maisha yao waliwekwa pembezoni, walijitahidi kuishi maisha ya kiinjili na wakajitahidi polepole kuingia katika mlango mwembamba. Ni wale ambao walishika sheria ya Bwana, wakitubu na kuomba msamaha daima. Na sasa wanaonja matunda na furaha ya huruma ya Mungu ambayo waliitafuta katika maisha yao.

Mpendwa msikilizaji kila mmoja wetu anaowajibu wa kujua wapi aliko katika sehemu hizi mbili. Hakuna mwingine ambaye atakuja na kuweka maelezo marefu au mafupi juu ya wapi uliko. Angalia maisha yako kuhusu sakramenti za Kristukama wazipokea vema, angalia kanuni ya Imani na kisha angalia kama uko usikivu kwa mamlaka halali iliyowekwa na Mwenyezi Mungu.

Angalia maisha yako katika uwanja wa fikra na maadili ukilinganisha na heri Nane za Mlimani ambazo ni mwongozo wa maisha yako ya kila siku pamoja na amri za Mungu. Kwa kifupi somo la pili latuambia wajibu wa kuishi daima katika imani kama atakavyo Baba yetu wa mbinguni ni wajibu wa kila mmoja wetu hata kama kuna mateso. Ni kwa namna hiyo twaweza kuingia katika mlango mwembamba.

Tumsifu Yesu Kristo.

Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.