2013-08-23 11:15:41

Jengeni utamaduni wa Utalii unaowajibisha: kiroho, kiutu na kimaadili!


Kardinali Antonio Maria VegliĆ², Rais wa Baraza la Kipapa la shughuli za kichungaji kwa ajili ya wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi katika ujumbe wake kwa washiriki wa mkutano wa shughuli za kichungaji nchini Argentina anawataka wakazie umuhimu wa utalii unaowajibisha.

Anasema, watalii wanapaswa kufaidika na mikakati ya kichungaji inayofanywa na Mama Kanisa katika kulinda na kudumisha misingi ya maisha bora ya kiroho, kimaadili, kiutu na kimaendeleo. Sekta ya utalii inapaswa pia kujikita katika mchakato wa kupambana na umaskini wa kipato na kihali, changamoto inayoendelea kutolewa na Baba Mtakatifu Francisko katika utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Mkutano huu ambao umefunguliwa hapo tarehe 21 Agosti, na kuhitimishwa tarehe 23 Agosti, 2013 umepembua Waraka wa Mababa wa Aparecida kuhusu Utalii kama sehemu ya mchakato wa ujenzi wa Ufalme wa Mungu na maboresho ya utu na heshima ya binadamu. Mababa wa Aparecida wanabainisha kwamba, katika mapambazuko ya Milleniab ya tatu ya Ukristo, kuna nyanja mbali mbali za shughuli na mikakati ya kimissionari na kati ya sekta hizi, utalii unapaswa kupewa msukumo wa pekee.

Kanisa pia linapaswa kujielekeza katika Uinjilishaji wa kina katika michezo, Sinema na kwenye Maduka Makubwa. Huku ndiko ambako kuna umati mkubwa wa watu unaojionesha katika uhalisia wa maisha ya kawaida. Sekta ya Utalii ni uwanja mpya unaoweza kutumiwa na Mama Kanisa katika Uinjilishaji Mpya, ili kukabiliana na changamoto za nyakati hizi katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Ukarimu upewe msukumo wa pekee, kwa kushirikiana na wadau mbali mbali katika miundo ya Kanisa.

Sekta ya Utalii ni kati ya sekta ambazo zinaendelea kucharuka kwa kuchangia kwa kiasi kikubwa katika ukuaji wa uchumi na inaweza kuwa ni chanzo cha fursa za ajira kwa vijana wengi wanaoteseka kutokana na hali ngumu ya maisha na ukosefu wa fursa za ajira, kiasi cha kuwafanya waanze kuishi kwa "kubangaiza".

Ni mwaliko wa kukuza na kudumisha utalii wa kijamii unaojenga na kuimarisha mshikamano wa upendo sanjari na kukataa mambo ambayo ni kinyume cha utu na maadili mema. Huu ndio utalii wa ngono, unaopaswa kupatiwa ufumbuzi kutoka katika chanzo chake. Waamini wajengewe uwezo kwa njia ya Mafundisho Jamii ya Kanisa, ili kudumisha utalii unaowajibisha: kiutu na kimaadili, ili watu waweze kuheshimiana na kuthaminiana na wala si kugeuzwa kuwa ni chombo cha kukidhi tamaa za watu. Utalii uwe ni kikolezo cha maendeleo endelevu na utunzaji bora wa mazingira.

Wajumbe wa shughuli za kichungaji, Baraza la Maaskofu Katoliki Argentina, wamejadili pamoja na mambo mengine kuhusu: utamaduni wa kazi; unyanyasaji na unyonyaji unaofanywa maeneo ya sekta ya utalii; mikakati ya kuwawezesha wajasiriamali ili kujikwamua kiuchumi; utalii kwa wote na mwono wa utalii katika jicho la kimissionari. Mkutano huu umekuwa ni fursa kwa wajumbe kusikiliza shuhuda mbali mbali zilizotolewa na wadau wakuu katika sekta ya utalii kutoka ndani na nje ya Argentina.







All the contents on this site are copyrighted ©.