Askofu mkuu Georg Ganswein, Mwandamizi mkuu wa Nyumba ya Kipapa, Jumamosi jioni, tarehe
24 Agosti 2013, anatarajiwa kuongoza Ibada ya Misa Takatifu kwenye Parokia ya “San
Tommaso da Villanova” iliyoko mjini Castel Gandolfo kama sehemu ya Maadhimisho ya
Kumbu kumbu ya Miaka 36 tangu Kanisa la “Madonna della Lago” lilipotabarukiwa.
Mara baada
ya Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu, waamini watafanya maandamano kuzunguka Ziwa.
Itakumbukwa kwamba, miaka 35 iliyopita Papa Paulo VI aliwakabidhi Wamissionari
wa Salesiani wa Don Bosco dhamana na wajibu wa shughuli za kichungaji kwa waamini
wanaoishi maeneo haya. Baada ya tafakari ya kina kwenye eneo hili, Baba Mtakatifu
Paulo VI akaridhia ujenzi wa Kanisa la “Madonna della Lago”, lililotabarukiwa kunako
tarehe 15 Agosti 1977 katika Sherehe ya Bikira Maria kupalizwa mbinguni mwili na roho.
Papa Paulo VI aliwaalika waamini kumwangalia Bikira Maria aliyepalizwa mbinguni
katika maisha ya sala, tafakari ya kina, maendeleo endelevu na uwiano bora wa maisha,
kama kielelezo cha ushuhuda wa imani tendaji. Wakati huo, Papa Paulo wa VI aliwatakia
kheri na baraka katika hija ya maisha yao hapa duniani, daima wajitahidi kutafuta
mafao ya wengi na kudumisha Ibada kwa Bikira Maria, Mama wa Mungu na Kanisa.
Mwenyeheri
Yohane Paulo II alitembelea Kanisa hili hapo tarehe 2 Septemba 1979 na kuadhimisha
Ibada ya Misa Takatifu kwa umati mkubwa wa waamini waliokuwa wamekusanyika Kanisani
hapo.