Kardinali Jorge Mario Bergoglio, katika uongozi wake kama Askofu mkuu wa Jimbo kuu
la Buenos Aires, alionesha moyo wa sala na bidii katika maisha na utume wake, akawa
ni mfano wa kuigwa katika kusimama kidete kulinda na kutetea maskini na wote waliokuwa
wanasukumwa pembezoni mwa Jamii kutokana na hali yao ya maisha.
Ni Baba aliyekuwa
na jicho la kuona mahitaji ya jirani zake na moyo thabiti wa kudiriki kuwasaidia kadiri
ya uwezo na nafasi yake. Kardinali Bergoglio alionesha karama na maisha ya kitawa
katika utekelezaji wa majukumu yake. Ni maneno ya Sr. Nora Antonelli, Mama Mkuu wa
Shirika la Mabinti wa Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili, Jimbo kuu la Buenos Aires,
Argentina, katika mahojiano maalum na Gazeti la Kila siku la L’Osservatore Romano.
Baba
Mtakatifu Francisko katika utume na shughuli zake za kichungaji, alitoa kipaumbele
cha pekee kwa majiundo na maisha ya kitawa. Alipenda kukutana na kuzungumza na watawa
kwani alitambua kwamba, hawa ni wadau muhimu sana katika mchakato wa Uinjilishaji
mpya. Si mtu aliyependa makuu, hata katika matukio makuu ambamo ulitegemea kumwona
miongoni mwa viongozi waliokuwa wamepewa viti vya mbele, lakini, wengi walishangazwa
kukutana naye kati ya watu wa kawaida.
Kwa maneno mengine anasema, Sr. Nora
Antonelli ni kiongozi aliyependa kuwa kati ya watu pasi na makuu! Jambo hili liliwagusa
wengi, hali ambayo inaendelea kujionesha hata wakati huu, kama Khalifa wa Mtakatifu
Petro. Hajabadilika hata katika utume wake mpya, bado ni kiongozi anayeonesha unyenyekevu
unaosheheni moyo wa upendo na utulivu wa ndani, kwa hakika ni kiongozi anayejiamini
katika maisha na utume wake.
Aliwagusa na kupendwa na vijana kutoka sehemu
mbali mbali za Jimbo kuu la Buenos Aires hasa wakati wa Maadhimisho ya Siku kuu ya
Ekaristi Takatifu, watu wengi walipokuwa wanashangaa kuona umati mkubwa wa vijana
wakiandamana kwa amani na utulivu, huku wakiimba kwa furaha wakati wa Maandamano ya
Siku kuu ya Ekaristi Takatifu. Alipenda kuwaonjesha vijana mafundisho tanzu ya imani
kwa Katekesi ya kina iliyokuwa inaacha chapa ya kudumu katika miyo ya watu wengi!
Baba
Mtakatifu Francisko katika utume wake kama Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Buenos, aliwagusa
wengi kutokana na mahubiri yake, mafupi lakini ya kina! Barua zake za kichungaji anasema
Sr. Nora Antonelli zilikuwa ni mwaliko wa kumfungulia Kristo malango ya maisha kwa
kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya huduma ya upendo kwa Mungu na jirani.
Huu
ulikuwa ni mwaliko kwa Familia ya Mungu nchini Argentina na wala si kwa ajili ya watu
wachache tu ndani ya Kanisa! Alikuwa anakazia huduma ya upendo inayobubujika kutoka
kwa Kristo na Kanisa lake; huduma inayoboreshwa kwa njia ya: Sala na Tafakari ya Neno
la Mungu linalomwilishwa katika uhalisia wa maisha ya watu! Hiki anasema Baba Mtakatifu
Francisko ni kielelezo cha ushuhuda wa imani tendaji kwa: maskini, wazee, wagonjwa
na watoto.
Kardinali Bergoglio alitambua shida na mahangaiko ya Mashirika ya
kitawa Jimboni mwake, lakini daima alikuwa tayari kuwafariji na kuwatia moyo kusonga
mbele kwa imani na matumaini pasi ya kukata wala kukatishwa tamaa na mahangaiko yao!
Wengi anasema Sr. Nora Antonelli, Mama Mkuu wa Shirika la Mabinti wa Bikira Maria
Mkingiwa Dhambi ya Asili, Jimbo kuu la Buenos Aires, wameendelea kuimarishwa kwa maneno
na mifano yake ya maisha!
Kardinali Bergoglio kama Askofu na mtawa, kila mwaka
alikuwa na utamaduni wa kuwaalika watawa kwa ajili ya kujadiliana na kushirikishana
mang’amuzi na vipaumbele vya maisha ya kitawa katika utekelezaji wa shughuli za kichungaji
Jimboni mwake. Mkutano wake na watawa ulikuwa unahitimishwa daima na Adhimisho la
Fumbo la Ekaristi Takatifu, lakini kabla ya Misa, alikuwa anatumia muda mrefu kuzungumza
na kufahamiana na watawa, akiomba sala kutoka kwao, unyenyekevu ambao ameendelea kuuonesha
tangu siku ile ya kwanza alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki kama Khalifa wa
Mtakatifu Petro.
Kama Askofu mkuu, alipenda kuwaona watawa wanaofanya shughuli
za kichungaji Jimboni mwake, wakionesha ushuhuda wa imani yao kwa Kristo na Kanisa
lake; daima wakiwa mstari wa mbele kulinda na kutetea haki msingi za binadamu. Tarehe
8 Septemba, kila Mwaka, Kanisa Katoliki nchini Argentina linaadhiisha Siku ya Watawa.
Hili lilikuwa ni tukio la pekee kabisa kwa Kanisa Katoliki Argentina kuonesha moyo
wa upendo pamoja na kuthamini mchango unaotolewa na Watawa katika maisha na utume
wa Kanisa.
Ushuhuda wa kweli unaojikita kwa Kristo Mwamba thabiti ndiyo furaha
ambayo Baba Mtakatifu Francisko anatamani kuiona ikibubujika kutoka kwa watawa wanapotekeleza
utume wao! Wawe na moyo wa: imani, matumaini na mapendo kwa watu wanaowahudumia hasa
katika sekta ya afya, elimu na maendeleo endelevu.
Sr. Nora Antonelli anasema
kwamba, Shirika la Mabinti wa Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili, lilianzishwa
na Mama Eufrasia Iaconis. Aliwapenda Watawa wa Mama Eufrasia. Itakumbukwa kwamba,
tarehe 13 Machi 2013, wakati macho na masikio ya watu wengi yalikuwa yameelekezwa
kwenye Kikanisa cha Sistina mjini Vatican, siku hiyo, Mama Kanisa alikuwa anafanya
Kumbu kumbu ya Mtakatifu Eufrasia, Bikira na Shahidi.
Kardinali Jorge Mario
Bergoglio ndiye aliyehitimisha mchakato wa kumtangaza Mtumishi wa Mungu Eufrasia Iaconis
kuwa Mwenyeheri hapo tarehe 2 Agosti 2012, kwa mara ya kwanza aliwaambia kwamba,
alipata kusikia ushuhuda wa maisha ya Mama Eufrasia kunako mwaka 1953, alipokuwa na
umri wa miaka 17 tu! Tangu wakati huo, ule ushuhuda haukuweza kufutika akilini mwake.
Alikuwa ni mwanamke wa kawaida lakini aliyebahatika kuwa na karama na vipaji vingi.
Kwa ufupi, huu ndio ushuhuda wa Sr. Nora Antonelli kuhusu maisha na utume
wa Kardinali Jorge Mario Bergoglio, Baba Mtakatifu Francisko!
Makala hii imehaririwa
na Padre Richard Mjigwa, C.PP.S Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.