2013-08-22 09:03:47

Dumisheni udugu, amani na mshikamano na maskini kama kielelezo cha imani tendaji!


Padre Raniero Cantalamessa, mhubiri wa nyumba ya kipapa anasema kwamba, Baba Mtakatifu Francisko inaonekana ni mtu mwenye maneno machache, lakini mengi anayaonesha kwa njia ya vitendo na ushuhuda wa maisha yake mwenyewe.

Kati ya mambo mengi ambayo kamwe hayataweza kufutika akilini mwa maelfu ya waamini na watu wenye mapenzi mema waliokuwa wanafuatilia tukio la kutangazwa kwake hadharani kwa njia ya vyombo vya mawasiliano ya jamii, ni pale alipoinamisha kichwa, akawaomba waamini na wote waliokuwa wamemiminika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, kusali kwa ajili yake katika ukimya!

Kufumba na kufumbua, Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, ukawa kimyaaaaa kwa kitambo! Waamini wakawa wa kwanza kumbariki Baba Mtakatifu Francisko, kabla hata ya Yeye mwenyewe kutoa baraka zake za kitume. Hili ni tukio ambalo kwa hakika lilikuwa linatoka katika undani wa maisha yake, kielelezo makini cha utume wake kama mchungaji mwenye uzoefu na mang’amuzi ya kina!

Padre Cantalamessa anasema, si haba kwamba, ameamua kuchagua jina la Mtakatifu Francisko wa Assisi mtu aliyejitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kuwahudumia maskini na wote waliokuwa wanasukumizwa pembezoni mwa Jamii. Mtakatifu Francisko ni mtu aliyeshuhudia vita na kinzani za kijamii na kidini, akageuka na kuwa ni chombo cha amani, urithi ambao Baba Mtakatifu Francisko anapenda kuurithisha kwa Kanisa na Jamii inayokabiliana na kinzani, migogoro na vita vinavyoendelea kupelekea taabu, mahangaiko na mateso ya watu wasiokuwa na hatia.

Mtakatifu Francisko alipenda na kuthamini mazingira, ambayo kimsingi ni haki ya uumbaji ambayo Mwenyezi Mungu amemkabidhi mwanadamu.

Lakini, dira na mikakati yote hii anasema Padre Raniero Cantalamessa inaweza kufanikiwa tu, ikiwa kama Waamini na Jumuiya ya binadamu katika ujumla wake, itashikamana katika umoja na udugu, kwa kutambua kwamba, wote wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu wanapaswa kupendana, kuheshimiana na kuthaminiana.

Kwa maneno machache anasema Padre Cantalamessa, Baba Mtakatifu Francisko anataka kukazia: udugu, amani, mshikamano wa dhati na maskini kama kielelezo cha imani tendaji, changamoto kwa Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.








All the contents on this site are copyrighted ©.