2013-08-21 11:38:04

Watu wengi bado wana majeraha ya vita, chuki na kinzani za kijamii!


Askofu Alexis Touably wa Jimbo Katoliki Agboville, nchini Pwani ya Pembe ambaye pia ni Mwenyekiti wa Tume ya Majadiliano, Ukweli na Upatanisho nchini humo anasema, kuna haja kwa Serikali kuongeza muda wa kazi kwa tume hii ili iweze kukamilisha vyema zaidi dhamana iliyokuwa imepewa katika mchakato wa kutafuta haki, amani na upatanisho miongoni mwa wananchi wa Pwani ya Pembe ambao wanaendelea bado kuponya makovu ya vita, kinzani na migogoro ya kijamii.

Si rahisi kwa Tume hii kuweza kukamilisha dhamana hii nyeti kwa kipindi cha mwaka mmoja, ukizingatia kwamba, vita na kinzani za kijamii zimeleta athari kubwa kwa wananchi wengi. Kwa haraka haraka watu wanaweza kuona kwamba, katika kipindi cha Mwaka mmoja, tume imeshindwa kukamilisha lengo na wajibu iliyokuwa imekabidhiwa kwao, lakini wanasahau kwamba, wananchi wengi bado wanaendelea kuponya majeraha kiasi kwamba, walishindwa kuonesha utashi wa ushirikiano na tume wakati wa kutekeleza dhamana yake.

Mchakato wa uponyaji unazingatia pia uhuru wa mtu binafsi anayeweza kujifungua kwa ajili ya kushirikiana na wengine katika kuleta mabadiliko, au kukataa kabisa na kuendelea kubaki amejifunga katika undani wake. Baadhi ya watu wamekataa kuonesha ushirikiano kwani wanasema wameathirika sana na kwamba, itawachukua muda mrefu kurudi katika hali ya kawaida. Yote haya ni madhara ya vita, machafuko ya kisiasa na chuki za kidini.

Askofu Touably anasema kwamba, bado Tume ya Majadiliano, Ukweli na Upatanisho inahitajika ili kuponya madonda ya vita, chuki na kinzani za kijamii nchini Pwani ya Pembe.







All the contents on this site are copyrighted ©.