Uwajibikaji na ushirikiano wa pamoja katika teknolojia ni chachu ya maendeleo endelevu
kwa nchi maskini duniani
Askofu mkuu Silvano Maria Tomasi, Mwakilishi wa Vatican kwenye Ofisi za Umoja wa Mataifa
zilizoko mjini Geneva, hivi karibuni katika mkutano wa Shirika la Biashara Duniani
aliwapongeza wadau mbali mbali wa shirika hili kwa kutekeleza majukumu yao huku wakizingatia
utu na maadili. Nchi Changa zaidi
duniani ni kiungo dhaifu sana katika Jumuiya ya Kimataifa, lakini zina idadi ya watu
wapatao millioni 880, kiasi cha asilimia 12% ya idadi ya watu duniani, lakini wanachangia
kiasi cha asilimia 2% ya Pato Ghafi la Dunia, kiasi cha asilimia 1% cha biashara duniani.
Askofu mkuu Silvano Maria Tomasi anabainisha kwamba, mchango huu hafifu kutoka
katika Nchi maskini zaidi duniani unatokana na ukweli kwamba, uchumi na maendeleo
yao bado yakon yuma kutokana na ujuzi hafifu, ugawaji mbaya wa rasilimali na pato
la taifa pamoja na ukosefu wa mapato ya ndani ambayo yangeweza kuchangia katika mchakato
wa maboresho ya hali ya uchumi na biashara katika nchi hizi. Mikakati mbali mbali
ya maendeleo iliyobuiniwa kwa miaka ya nyuma, inaonekana kutofua dafu na kwamba, watu
wengi wameendelea kutumbukia katika balaa la umaskini wa hali na kipato na kwamba,
ubora wa maisha ya wananchi wengi unaendelea kufifia mwaka hadi mwaka kadiri ya takwimu
kutoka katika Jumuiya ya Kimataifa. Tangu mwaka 2002 hadi mwaka 2007 kumekuwepo na
ongezeko la maskini wapatao millioni tatu kila mwaka. Takwimu zinaonesha kwamba,
katika kipindi cha mwaka 2007, asilimia 59% ya watu Barani Afrika walikuwa wanaishi
kwa kiwango cha dolla 1.25 kwa siku. Pato la kila mwananchi linaendelea kupungua siku
hadi siku na kwamba, asilimia 50% ya wananchi wanaoishi katika nchi changa zaidi duniani
wanakabiliwa na umaskini mkubwa na kwamba, hakuna matumaini ya maboresho ya hali ya
wananchi hawa ikiwa kama Jumuiya ya Kimataifa haitachukua hatua za dharura. Nchi
nyingi zinaweza kushindwa kufikia Malengo ya Maendeleo ya Millenia kwa sababu ya uzalishaji
na tija kuwa ni katika kiwango cha chini kabisa; miundo mbinu hafifu na kwamba, kuna
kiwango kikubwa cha maambukizi ya ugonjwa wa Ukimwi unaoendelea kufyeka nguvu kazi
ambayo ingeweza kutumika kuzalishia mali na kutoa huduma. Takwimu za ugonjwa wa Ukimwi
zinaonesha kwamba, katika kipindi cha mwaka 2011 kulikuwa na wagonjwa wa Ukwimwi duniani
wapatao millioni 34, kati yao millioni 9.7 wanatoka katika nchi changa zaidi duniani.
Wagonjwa millioni 4.6 walikuwa wanahitaji kupatiwa dawa za kurefusha maisha, lakini
ni wagonjwa millioni 2.5 tu ndio waliokuwa wamefanikiwa kupata dawa hizi. Hii ina
maana kwamba, wagonjwa wengi wa Ukimwi hawana tena matumaini ya kuendelea kuishi.
Bado kuna magonjwa yasiyo ya kuambukiza yanawanyemelea wananchi katika nchi maskini
zaidi duniani kwa kasi kubwa kuliko ilivyo katika nchi tajiri zaidi duniani. Askofu
mkuu Silvano Tomasi anasema kwamba, Nchi maskini duniani zinataka ziwezeshwe ili ziweze
kujikwamua kutoka katika mkwamo wa uchumi na maendeleo, ili hatimaye, waweze kuung’oa
umaskini ambao umekuwa ni kizingiti kikubwa cha maendeleo ya wananchi. Anasema, miliki
ubunifu inapaswa kupimwa kwa kuangalia faida na maendeleo yanayoweza kupatikana kwa
Nchi changa zaidi duniani, ikiwa kama zitasaidiwa kupata teknolojia; kwa kuzingatia
haki na wajibu. Ujumbe wa Vatican kwenye mkutano huu umesisitizia kwamba, Jumuiya
ya Kimataifa haina budi kuhakikisha kwamba, miliki ubinifu inatumika kwa ajili ya
mafao ya wengi pamoja na kujenga uhusiano mwema katika Jumuiya ya Kimataifa na kwa
namna ya pekee na Nchi changa zaidi duniani. Miliki ubunifu iwe ni kikolezo cha mchakato
wa maboresho ya maendeleo na uchumi. Uwajibikaji wa pamoja na ushirikiano wa kiteknolojia
ni chachu ya maendeleo endelevu kwa nchi maskini zaidi duniani.