2013-08-21 08:27:58

Someni alama za nyakati ili kuwahamasisha waamini kuchangia mchakato wa Uinjilishaji mpya kwa hali na mali!


Askofu mkuu Protase Rugambwa, Katibu mkuu mwambata wa Baraza la Kipapa la Uinjilishaji wa watu na Rais wa Mashirika ya Kipapa ya kazi za Kimissionari katika mahojiano na Radio Vatican anasema, kwamba, Wakurugenzi wa Mashirika ya Kipapa katika nchi mbali mbali wanapaswa kusoma alama za nyakati kwa kuwaelimisha na kuwahamasisha waamini na watu wenye mapenzi mema kushiriki kikamilifu katika mchakato wa Uinjilishaji mpya kwa hali na mali. RealAudioMP3

Mashirika ya Kipapa ya kazi za kimissionari yatambue wajibu na dhamana ya kuendeleza kazi ya Uinjilishaji mpya, kwa kuwahamasisha waamini ili waweze kujitoa kikamilifu ili kushiriki katika utume huu. Mashirika haya yajiwekee mikakati ya uhamasishaji pamoja na kujijengea nguvu ya rasilimali fedha. Wakurugenzi wa PSM wajitahidi kuwatambua waamini wao ili kuweza kuwashirikisha kila mtu kadiri ya uwezo na nafasi yake.

Umefika wakati wa kubadilisha mfumo wa uhamasishaji wa jumla na kuanza kuwalenga watu au makundi ya watu kwa njia: mitandao ya kijamii, barua, matumizi sahihi na makini ya vyombo vya upashanaji habari. Watu wahabarishwe kuhusu kazi na utume wa Mashirika ya Kipapa ya Kazi za Kimissionari, ili waweze kujitoa kikweli kweli. Wakurugenzi hawa watambue kwamba, fedha inayopatikana kama sehemu ya mchango wa waamini kwa ajili ya kazi za kimissionari inapaswa kutumiwa kadiri ya lengo lake kwa kuzingatia misingi ya ukweli, uwazi na uwajibikaji.

Wakurugenzi wa Mashirika ya Kipapa ya Kimissionari yasome alama za nyakati na kuanza kushiriki katika mchakato wa maboresho wa uhamasishaji, ukusanyaji na matumizi ya rasilimali fedha.







All the contents on this site are copyrighted ©.