Papa Francisko, bado anaendelea kuwashukuru wenyeji wa Rio de Janeiro!
Baba Mtakatifu Francisko amemwandikia barua ya shukrani Askofu mkuu Oran Joao Tempesta
wa Jimbo kuu la Rio de Janeiro kutokana na moyo wa ukarimu waliomwonjesha wakati wa
Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani. Vijana wameonesha nguvu ya imani dhidi
baridi na mvua zilizoambatana na Maadhimisho haya.
Baba Mtakatifu anawashukuru
na kuwapongeza viongozi wote wa Jimbo kuu la Rio de Janeiro, Kamari kuu ya maandalizi
na vijana wote waliojitolea kuwahudumia ndugu zao kwa moyo wa upendo na mshikamano,
bila kuwasahau wananchi wa Brazil kwa ujumla wao!
Baba Mtakatifu anamwomba
Askofu mkuu Tempesta kumfikishia salam zake za upendo kwa vijana wanaopata matibabu
kutoka katika Hospitali ya Mtakatifu Francisko wa Asisi ambao alipata bahati ya kuwatembelea
na kuzungumza nao, bila kuwasahau wakazi wa kitongoji cha Varginha na Copacabana.
Baba Mtakatifu mwishoni, anamwomba Askofu mkuu amfikishie salam zake za pekee
kwa wananchi wa Guaratiba, mji ambao haukubahatika kutumika kwa ajili ya kufunga Maadhimisho
ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013 kutokana na mvua kubwa, iliyosababisha
matope kujaa kwenye Uwanja wa Campus Fidei uliokuwa umeandaliwa kwa ajili ya shughuli
hizi.