Jengeni utamaduni wa majadiliano ya kina ili kudumisha haki, amani na mafao ya wengi!
Baraza la Maaskofu Katoliki Benin katika ujumbe wake kwa Waamini na wananchi wa Benin
wakati huu wanapoanza mchakato wa mabadiliko ya Katiba ya Benin, wanawaalika wadau
wote kuhakikisha kwamba, wanajenga utamaduni wa majadiliano ya kina, ili kudumisha
misingi ya haki na amani; kwa kuthaminiana na kuheshimiana kama sehemu ya mchakato
wa ujenzi wa umoja wa kitaifa unaopania mafao ya wengi.
Hivi karibuni Rais
Yayi Boni wa Benin ameanzisha mchakato wa mabadiliko ya Katiba nchini Benin, jambo
ambalo limezua mjadala mkubwa nchini humo kutokana na ukweli kwamba, mabadiliko haya
yanapania kumwongezea Rais madaraka pamoja na kuimarisha dhamana ya Mahakama ya Kikatiba.
Baraza la Maaskofu Katoliki Benin linasema, Kanisa halina majibu ya kiufundi
wala kisiasa katika mjadala huu, lakini lina dhamana na utume wa Kinabii na Kimaadili
unaolisukuma kuwakumbusha Waamini na wananchi wote wa Benin kwamba, hakuna demokrasia
ya kweli inayolenga kuwaganywa watu; bali daima demokrasia uwe ni utawala shirikishi
kwa ajili ya mafao ya wengi, ustawi na maendeleo ya wananchi wote wa Benin.
Wananchi
wa Benin kwa sasa wanakabiliana na baa la umaskini wa hali na kipato, lakini kuna
baadhi ya wananchi wanaokula na kusaza kutokana na ubinafsi, rushwa na ufisadi, mambo
ambayo yanaendelea kuchangia kinzani na migogoro ya kijamii nchini humo. Kuna kundi
kubwa la vijana ambalo halina fursa za ajira, hali ambayo inatishia amani na usalama
wa wananchi wa Benin. Madai ya kutaka kuipindua Serikali halali iliyoko madarakani
ni mambo yanayoendelea kuzua hofu na wasi wasi miongoni mwa raia wenye mapenzi mema.
Baraza
la Maaskofu Katoliki Benin linasema, shida na changamoto zote hizi zinaonesha kwamba,
kuna umuhimu wa kujenga utamaduni wa majadiliano ya kina, kwa kujikita katika huduma
bora na makini kwa wananchi wa Benin; kwa pamoja wakitafuta na kudumisha mafao ya
wengi, ili kujenga na kudumisha umoja na mshikamano wa kitaifa. Maaskofu wanakumbusha
kwamba, si rahisi wala haki kwa baadhi ya wanasiasa kujitwalia madaraka na jukumu
la kutaka kutatua matatizo yote ya wananchi wa Benin.
Kuna haja ya kujenga
dhamana ya uwajibikaji na mshikamano wa pamoja, kutoka kwa mwananchi, wakuu na wadau
wa sekta mbali mbali kwa ajili ya mafao ya wengi. Jamii ijikite zaidi katika ukweli,
uwazi na uaminifu kwa kuzingatia makubaliano yaliyokwishakufikiwa katika hatua mbali
mbali za majadiliano kuhusu mafao na maendeleo ya wananchi wa Benin.
Baraza
la Maaskofu Katoliki Benin, linawakumbusha wanasiasa sehemu ya hotuba iliyotolewa
na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, Mwezi Novemba 2011, alipokuwa
nchini Benin kwa ajili ya kuzindua Matunda ya Maadhimisho ya Awamu ya Pili ya Sinodi
ya Maaskofu wa Bara la Afrika, kwa kuwataka wanasiasa na wachumi kutoka Barani Afrika
na Jumuiya ya Kimataifa katika ujumla wake, kuhakikisha kwamba, hawathubutu kupokonya
matumaini kutoka kwa wananchi wao na wala wasiwe ni kikwazo cha maendeleo yao kwa
siku za usoni.