2013-08-19 11:19:42

Kongamano la IV la Kimissionari Kitaifa nchini Argentina


Baraza la Maaskofu Katoliki Argentina linaadhimisha Kongamano la IV la Kimissionari Kitaifa kama fursa ya kuwatia moyo na kuwaimarisha waamini kutekeleza dhamana na wajibu wao wa Kimissionari katika Majimbo na Kanisa kwa ujumla, mintarafu maelekezo ya Mkutano wa nne wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Amerika ya Kusini na Caraibi, uliofanyika mjini Aparecida.

Maadhimisho ya Mwaka 2013 yanaongozwa na kauli mbiu Wamissionari wa Argentina, shirikisheni imani yenu". Maadhimisho haya yanafanyika wakati huu Mama Kanisa anapoendelea kuadhimisha Mwaka wa Imani. Hii pia ni sehemu ya Maandalizi ya Kongamano la IV la Amerika na lile la IX yatakayofanyika nchini Venezuela.

Kwa sasa Maadhimisho haya yanawapatia waamini nafasi ya kutafakari changamoto zinazokwamisha mchakato wa Utangazaji wa Habari Njema ya Wokovu katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia; Ulimwengu ambao umesheheni kila dalili za ukanimungu.

Maadhimisho ya Kongamano hili yamefunguliwa kwa ujumbe wa Baba Mtakatifu Francisko anayewapongeza kwa ari na moyo wa kimissionari wanaouonesha na kwamba, umefika wakati wa kutoka katika undani mwao ili kwenda kutangaza Injili ya Kristo pembezoni mwa maisha ya Jamii. Kongamano hili la kitaifa liwe ni nafasi ya kukua na kukomaa katika utume wa kimissionari kwa kutumia vyema na bila woga, karama na mapaji waliyokirimiwa na Roho Mtakatifu.

Baba Mtakatifu anawaombea ili kwamba, Yesu mwenyewe aweze kuwaondoa kutoka katika kishawishi cha kutaka kuponda raha mustarehe. Baba Mtakatifu anapenda kuwahakikishia uwepo wake kwa njia ya Sala na Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu.







All the contents on this site are copyrighted ©.