Baraza la Maaskofu Katoliki India, Jumapili iliyopita limeadhimisha Siku ya 30 kwa
ajili ya kuombea amani nchini India. Kauli mbiu ya Maadhimisho haya kwa mwaka huu
ni “Amani duniani katika haki”. Mada hii imechaguliwa kwa makusudi kama sehemu ya
mwendelezo wa Maadhimisho ya Waraka wa Kichungaji ulioandikwa na Papa Yohane wa XXIII,
“Pacem In Terris”, Amani Duniani na kutiwa mkwaju hapo tarehe 11 Aprili
1963.
Baraza la Maaskofu Katoliki limewakumbusha waamini na watu wenye mapenzi
mema nchini India umuhimu wa Mafundisho ya Waraka huu katika mchakato wa kukuza, kudumisha
na kuendeleza misingi ya haki, amani na mshikamano miongoni mwa Jamii.
Dunia
mpya inasimikwa katika misingi ya ukweli, upendo na uhuru. Hivi ndivyo Baba Mtakatifu
Yohane wa XXIII alivyobainisha katika Waraka wake wa Amani Duniani na kwamba, amani
inapatikana pale tu: haki msingi, mahusiano, utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa
kwa sura na mfano wa Mungu vinatambuliwa na kuthaminiwa. Waraka huu unafafanua kwa
kina maana ya haki msingi za binadamu kuwa ni mambo yote yanayofumbatwa katika haki
msingi za binadamu.
Ili amani na utulivu viweze kutawala miongoni mwa Jumuiya
ya Kimataifa na Kitaifa, kuna haja ya kukuza na kudumisha msingi wa majadiliano na
kwamba, vita na kinzani ni mambo ambayo yamepitwa na wakati kwa sasa kama njia ya
kuleta suluhu ya matatizo ya kijamii. Haki inapaswa kueleweka kuwa ni utambuzi wa
kweli wa utu wa mwanadamu unaohitaji kulindwa dhidi ya mashindano ya utengenezaji
wa silaha za mahangamizi.
Huu ni mwaliko kwa Jumuiya ya Kimataifa kusitisha
utengenezaji, ulimbikizaji na matumizi ya silaha za mahangamizi ambazo zinaweza kuleta
maafa makubwa kwa binadamu. Ujumbe huu ni muhimu kwa India ambayo ni mnunuzi mkubwa
wa silaha kutoka nje na kwamba, India hivi karibuni ilijitoa katika Mkataba wa Umoja
wa Mataifa kuhusu udhibiti wa silaha za mahangamizi.
Baraza la Maaskofu Katoliki
India linasema, yamekuwa ni Mapokeo ya Kanisa Katoliki nchini India kuadhimisha Jumapili
ya kuombea haki, kila jumapili inayofuatia baada ya Maadhimisho ya Uhuru wa India.
Baraza la Maaskofu Katoliki India kunako mwaka 1983 katika mkutano wao uliofanyika
mjini Bombay uliamua kwamba, Kanisa nchini India liadhimishe Jumapili ya Kuombea Haki,
kama sehemu ya mwaliko kwa waamini na watu wenye mapenzi mema kutambua changamoto
zinazoikabilia haki nchini India.
Mwaliko huu unakwenda sanjari na Sheria
za Kanisa zinazomtaka kila mwamini kuhakikisha kwamba, anakuza na kuendeleza haki
jamii mahali anapoishi; shughuli hii itekelezwe na viongozi wa Kanisa mintarafu kweli
na moyo wa Kiinjili kuhusiana na masuala ya hakijamii.