2013-08-17 11:46:18

Shukrani kwa Familia ya Mungu nchini Brazil


Baba Mtakatifu Francisko amemwandikia barua Kardinali Raymundo Damasceno Assis, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Brazil ili kumshukuru kwa niaba ya Familia ya Mungu nchini Brazil kwa makaribisho makubwa waliyomwonesha wakati wa hija yake ya kichungaji nchini Brazil, lakini kwa namna ya pekee kabisa wakati alipotembelea Madhabahu ya Bikira Maria wa Aparecida.

Baba Mtakatifu anasema, ndani ya sakafu ya moyo wake anahifadhi kumbu kumbu ambazo haitakuwa rahisi kufutika kwa haraka. Anaukumbuka umati mkubwa wa waamini na watu wenye mapenzi mema, uliojitokeza kuhudhuria Ibada ile pamoja na mkutano na Baraza la Maaskofu Katoliki Brazil na Amerika ya Kusini katika ujumla wake. Baba Mtakatifu anaendelea kumshukuru Bikira Maria wa Aparecida kwa maombezi na tunza yake ya kimama.

Anamwomba Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Brazil kumfikishia salam na matashi mema kwa Familia ya Mungu nchini Brazil kwa jitihada walizoonesha katika maandalizi na hatimaye Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013 iliyofanyika mjini Rio de Janeiro. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu kwamba, Maadhimisho haya ya Imani yatakuwa ni kipindi cha neema, baraka na mwanzo mpya kwa Kanisa nchini Brazil.

Baba Mtakatifu Francisko anahitimisha barua ya shukrani kwa Kardinali Raymundo Damasceno Assis kwa kuliweka Kanisa na wananchi wote wa Brazil chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria wa Aparecida. Anawatakia wote baraka zake za kitume.







All the contents on this site are copyrighted ©.