2013-08-17 10:15:11

Mazoea yakizidi huleta dharau!


Mimi na Nyumba yangu tutamtumikia Bwana...

Mazoea yakizidi sana huleta dharau. Waisraeli wameanza kumzoea Joshua na watumishi wa Mungu wana wa Haruni. Wamezoea sadaka zao na sanduku la Agano. Katika utulivu wa nchi ya ahadi hakuna jipya tena. Wanaanza kuvutika na miungu mwingine. Wanataka kuuacha mbacha kwa msala upitao. Yoshua anawaambia chagueni ninyi wenyewe nani wa kumtumikia. ".. Lakini mimi na nyumba yangu tutamtumikia Bwana" (Yoshua 24:14-29).

Leo Agosti 17, 2013: - Mungu kwa kinywa cha Yoshua anataka kusema,

1. Mungu daima kwetu sisi lazima kila siku awe mpya. Tusidhani kuwa kwa kusoma masomo Kanisani, kwa kuimba kwaya au kuwa kiongozi parokiani tumekwishamjua Mungu. Hata kama tukilala na kuamkia Kanisani tumche Mungu kwa uzito wote na kutetemeka kana kwamba tumemjua Leo. Njia za Mungu daima huwa hazichunguziki.

2. Kumtumikia Mungu kunahitaji familia zima ihusike. Baba ahakikishe watoto wanafuata utaratibu na nidhamu ya nyumbani ikiwemo kusali. Na ndio maana ”Shema Israel” (Kumb 6:4) ilimtaka baba wa familia awafundishe watoto wake kumpenda Mungu. Baba anamtumikia Mungu na watoto wake anaposali nao kabla ya kulala, anapokwenda nao Kanisani na kushiriki shughuli nyingine za kikanisa. Baba akienda, watoto wote watafuata.

3. Kuna familia zetu ambazo zina wasichana wa kazi nyumbani ambao ni Wakristo na tena Wakatoliki, lakini Jumapili wanazuiwa kufika Kanisani. Siku za jumapili ndio wanatoa nguo zote za kufua na kumpatia ”house girl”. Au kwa familia nyingine wasichana wengine huwa hawajapata Komunio ya kwanza au Kipaimara. Ni jukumu la wenye familia kuhakikisha kuwa wasichana hawa wanafuata mafundisho na kupata huduma ya Sakramenti pindi wakiwa katika kazi. Hii ni kuhakikisha nyumba yote inamtumikia Bwana. Na pia kutimiza vizuri amri ya kushika kitakatifu siku ya Bwana ambapo hata mjakazi hakutakiwa kufanya kazi (Kutoka 20:10)

Somo letu leo la Injili - Mt 19:13-15, Kristo anaonesha na kukumbusha wajibu wa wazazi kwa watoto. Kuna wazazi ambao hawali chakula na watoto wao, hawaongei nao, hawakagui na kukagua daftari zao. Watoto wanakua na hisia za kuachwa, kukataliwa na kutopendwa. Watoto daima huwa wanaguswa sana na hisia za mguso "sense of touch". Mguso wa baba au mama huwaachia hisia za usalama, upendo na kujaliwa. Na ndio maana Kristo, huku akiwashika na kuwabariki watoto akasema - "waacheni watoto wadogo waje kwangu.." au kwa lugha ya Kimakonde - "Valeke vadyoko vidikidiki vaide kwangu.."

Bwana Yesu anataka kusema na familia zetu yafuatayo :

1. Dini ya kwanza ya watoto ni kupendwa, kutunzwa na kujaliwa na wazazi wao nyumbani. Hii ni katekesi ya kwanza ya msingi kwao. Tunapomfundisha mtoto kuwa Mungu atupenda, ni lazima mtoto awe ameonja kwa nafasi ya kwanza kutoka upendo wa wazazi wake. Daima tunalaumu watoto wa siku hizi hawajui dini. Kumbe, tatizo ni kuwa sisi kama wazazi tulishindwa kuwaonjesha dini ya kwanza kwao - kuwapenda na kuwakumbatia kama alivyofanya Yesu.

2. Wajibu wa wazazi ni kuwapa watoto viashiria vingine vya upendo - yaani, kuwalisha chakula vizuri, kuhakikisha wanalala mahali pazuri, wanavaa nguo nzuri na mahitaji mengine. Kufanya hivi kunahitaji wazazi kujinyima. Mtoto hawezi kula matunda au mboga nzuri kama baba ataendekeza bia na nyama choma katika viti virefu baa. Kuwalisha watoto vizuri ni sadaka kubwa kwa familia ye yote. Hivyo, unapoongeza bia ya nne au ya tano ujue wazi unaacha kuwakumbatia watoto wako.

3. Mtoto akipendwa vizuri ni rahisi naye kuwapenda na kuwaheshimu
wazazi. Mtoto atatimiza amri ya nne ya Mungu kiurahisi kwa vile atakuwa ameonja utamu wa utii toka kwa wazazi. Na mwisho tuwaonye watoto wetu kwa upole. Hasira na vipigo vya kupitiliza huwaharibu kabisa watoto wetu.

Tusali kwa ajili ya watoto ambao wapo katika familia zenye matatizo. Wazazi hawaishi kugombana kila siku, mzazi mmoja ni mlevi pindukia, wazazi wao wamefariki na shida nyingine. Bwana wakumbatie watoto hawa kwa upendo wako na uwabariki wapate riziki ya kutosha na fukuto la Upendo kutoka kwako.

Fadre Benno Michael Kikudo, Jimbo kuu la Dar es Salaam.








All the contents on this site are copyrighted ©.