2013-08-16 10:47:10

Utoto Mtakatifu nchini Madagascar wafanya kongamano la kwanza


Kwa mara ya kwanza Baraza la Maaskofu Katoliki Madagascar limehitimisha Kongamano la Utoto Mtakatifu kitaifa, tukio ambalo limehudhuriwa na watoto 2,000 wenye umri kati ya miaka 6 hadi 14 kutoka katika Majimbo 20 yanayounda Baraza la Maaskofu Katoliki Madagascar.

Kongamano hili la kitaifa sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani uliotangazwa na kuzinduliwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, limeongozwa na kauli mbiu "Watoto wanaomwamini Yesu Kristo na kushirikiana kati yao ni vitalu vya Kanisa". Tukio hili liliandaliwa na Tume ya Walei, Baraza la Maaskofu Katoliki Madagscar. Kwa siku nne mfululizo, wanachama wa Utoto Mtakatifu wamebahatika kupata katekesi ya kina kuhusu: watoto na imani; mtoto na mabadiliko katika ulimwengu wa utandawazi; haki msingi za mtoto mintarafu Mafundisho Jamii ya Kanisa.

Hizi ni Katekesi zilizokuwa zinatolewa na Maaskofu kutoka Madagascar kwa ajili ya majiundo makini ya watoto hawa ambao ni tumaini la Kanisa na Jamii kwa sasa na kwa siku za usoni. Imekuwa ni nafasi kwa watoto hao pia kushiriki michezo na masuala mbali mbali ya kijamii kadiri ya umri na nafasi yao.

Katika Ibada ya Misa Takatifu ya kufunga Kongamano la Kwanza la Utoto Mtakatifu nchini Madagascar iliyoongozwa na Askofu mkuu Jean Claude Randrianarisoa, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Madagascar alisema kwamba, shule ya kwanza yenye wajibu wa kurithisha tunu msingi za maisha ya kiimani, kimadili na utu wema ni familia. Wazazi na walezi wanaendelea kuhamasishwa ili kuhakikisha kwamba, wanashiriki kikamilifu katika malezi na makuzi ya watoto wao katika: upendo, msamaha na upatanisho.

Hizi ni mada msingi zinazoendelea kufanyiwa kazi na Familia ya Mungu Barani Afrika, kama sehemu ya utekelezaji wa Maagizo ya Mababa wa Awamu ya Pili ya Sinodi ya Maaskofu wa Afrika. Baada ya Misa Takatifu, watoto wa Utoto Mtakatifu nchini Madagascar wametumwa kuwainjilisha watoto wenzao kwa njia ya ushuhuda wa mifano bora ya maisha, kwa maneno na matendo adili.







All the contents on this site are copyrighted ©.