Jitajirishe na Katekesi ya kina kuhusu Fumbo la Bikira Maria kupalizwa mbinguni!
Kanisa Katoliki popote duniani huadhimisha Sherehe ya kupalizwa Bikira Maria Mbinguni
na kuwekwa kwake Malkia wa mbingu; Wamisionari wa Damu Azizi, huadhimisha siku ya
kuanzishwa kwa Shirika lao; tukio lililofanyika katika Abasia ya Mt. Felix, kijijini
Giano, mkoani Umbria, nchini Italia. Gaspari Del Bufalo ndiye mwanzilishi, ambaye
aliliweka Shirika chini ya ulinzi wa Bikira Maria Mama na Malkia wa Damu Azizi. Na
hatimaye, waamini wa Parokia ya Bikira Maria wa Damu Azizi inayojumuiisha maeneo la
Kisasa na Nzuguni iliyoko katika Jimbo Katoliki Dodoma, huadhimisha siku ya somo wao.
Kupalizwa
mbinguni kwa Bikira Maria ni fundisho pekee muhimu katika Kanisa? Kanisa lafundisha
na kuishi mafundisho kadha wa kadha ya kiimani. Saba kati ya hayo, ni mafundisho muhimu
kiasi cha kusema "asiye yaamini na kuyaishi, sio mkatoliki wa kweli. Mafundisho au
mafumbo hayo ni kama ifuatavyo:
· Utatu Mtakatifu: Kwamba Mungu wetu ni mmoja
katika nafsi tatu; yaani; Baba, Mwana, na Roho Mtakatifu. Hili ni fumbo msingi na
ni fumbo mama la mafumbo mengine yote. · Umwilisho: Kwamba Kristo Mungu aliyetwaa
mwili wa kibinadamu kwa nguvu ya Roho Mtakatifu na kwa njia ya Bikira Maria, hivyo
kuwa Mungu-kweli na Mtu-kweli. · Ukombozi: Kwamba kwa mateso, kifo na ufufuko wake,
Yesu Kristo ndiye Mkombozi pekee wa ulimwengu. · Ekaristi Takatifu: Kwa mageuzi
katika adhimisho la Misa Takatifu, lile Kristo aliloliadhimisha jioni ya Alhamisi
Kuu, linatendeka tena; yaani, mkate na divai, hugeuka kuwa Mwili na Damu ya Kristo. ·
Bikira Maria Kukingiwa dhambi ya asili: yaani, ili Yesu azaliwe, Mungu Baba aliandaa
mazingiza kwa kumkinga Bikira Maria toka doa lolote la dhambi tangu tumboni mwa mamaye
Anna. · Bikira Maria Kupalizwa mbinguni:- yaani, Mungu, alimchukua mbinguni Bikira
Maria mwili na roho. · Bikira Maria Mama wa Mungu:- kwamba Maria ni Mama wa Yesu,
Yesu ni Mtu-Mungu, hivyo, Maria aliye mama wa Yesu-Mtu pia ni mama wa Mungu.
4.
Kuna mbinu iwezayo kutumika kuyakumbuka mafumbo hayo saba? ·Utatu - Umwilisho –
Ukombozi- Ekaristi – Kukingiwa- Kupalizwa Mbinguni - Mama wa Mungu. 5. Juu ya Kupalizwa
mbinguni Bikira Maria kuna angalisho la pekee? · kwa kuwa Kupalizwa mbinguni ni
moja ya mafundisho yenye hadhi ya kuitwa fumbo; yafaa, tutafakari na kuelewa vyema
nini kinachoadhimishwa.
6. Je, nini maana ya Kupalizwa mbinguni? ·Kanisa
Katoliki linaamini, linafundisha na kuhimiza kuwa: Bikira Maria baada ya kumaliza
maisha yake hapa duniani, alipalizwa mbinguni, mwili na roho. ·Hii ni sherehe kubwa
kuliko zote zinazoadhimishwa na Kanisa kwa heshima ya Bikira Maria.
·Na wasio
Wakatoliki husema na kuuliza: kwa nini Wakatoliki mnamheshimu Maria kiasi hicho; ni
kama kusema, eti tunamheshimu kupita kiasi au kuliko inavyostahili. ·Ukweli ni
kwamba, kwa kumchagua Maria, kati ya vizazi au watu wote kuwa mama wa Mwanae wa pekee
Kristo, Mungu alimheshimu Maria kuliko alivyowaheshimu wanadamu wengine wote na kuliko
sisi tunavyoweza kumheshimu Bikira Maria.
·Ikiwa Mungu kamheshimu Maria kiasi
hicho, cha kuwa Mama wa Mwanaye wa pekee, cha kuwa Mpalizwa mbinguni- mwili na roho,
kwa nini sisi tusimheshimu kwa namna tufanyavyo na hata zaidi ya hivyo?
·
Tujiulize: kwa nini tusimpende mama yetu? Je, mtu akimdharau mama yako mpendwa, huyo
atakuwa bado rafiki yako?
· Maria ni mama wa Bwana wetu: alimzaa, alimtunza,
hadi kufikia utu uzima, na akabaki chini ya msalaba siku ile Yesu alipoinuliwa, yaani,
kusulibiwa na kufa msalabani. Anastahili sio tu heshima (reverence) bali heshima kubwa
(veneration) pasipo kuvuka mipaka ya kumpa heshima ya kumwabudu (adoration).
·
Na tunapomwendea, tukiomba msaada wa maombezi yake, Maria hufikisha maombi na sala
zetu kwa Mwanae, na kama arusini Kana, Mwanae Kristo hutujalia ili mradi ombi liendane
na matakwa ya Baba wa mbinguni ya kumkomboa mwanadamu. · Basi tuzidi kumpenda na
kumsifu Bikira Maria aliyepalizwa mbinguni kwa kuimba Zab. 45:9.
7. Nini asili
au msingi wa fundisho juu ya Bikira Maria kupalizwa mbinguni? (Au fundisho fundisho
hilo lilitujia vipi?) · Kwa hakika:- fundisho halikubuniwa au kuzushwa na viongozi
wa Kanisa Katoliki kama baadhi ya wazushi na wapinzani wanavyofikiri. Msingi wake
ni wa kweli kama ifuatavyo:
· Maandiko Matakatifu: sambamba na nia ya Mungu
ya kumkomboa mwanadamu toka dhambi na mauti, Maria alikuwa katika mpango na wazo la
Mungu tangu milele na kutabiriwa katika Agano la Kale kama isomekavyo katika Mw. 3:15
na Is. 7:14. Maria aliheshimiwa na Mungu kiasi cha kuteuliwa kuwa Mama wa Mkombozi,
kama isomekavyo katika Gal. 4:4-5. Maria alishirikishwa ipasavyo na kikamilifu katika
mpango huo wa Ukombozi, naye Kwa hiari pasipo shuruti, alikubali na alitekeleza; hivyo,
ilimpendeza Mungu kuwa Maria atawale mbinguni pamoja na Mwanae Mkombozi Yesu Kristo.
·
Mkingiwa Dhambi ya Asili: hivi ni nani baada ya kujijengea nyumba nzuri apate kukaa
ndani yake atamruhusu adui yake kutangulia kuingia na kukaa humo? Ni swali awekalo
mbele yetu Mt. Sirillo wa Alexandria; kwamba Mungu alimwumba Maria, akamchagua tangu
milele awe mama wa Mkombozi; ingekuwa ajabu kama angemruhusu shetani akae rohoni mwa
Bikira Maria; ndio maana, Mungu alimkinga dhidi ya dhambi ya asilli; hivyo yeye aliyezaliwa
bila dhambi ya asili, hakustahili mwili wake uoze kaburini.
· Maria ni mshiriki
katika kazi ya ukombozi:- Alipo Yesu yuko Bikira Maria; mama Maria aliambatana na
Yesu akashiriki taabu na raha. Maria alichukua mimba na kumzaa Yesu; Maria na Yosefu
walilazimika kumtwaa mtoto Yesu na kukimbilia Misri kumwepusha mtoto na mauaji ya
Herode; alikuwa naye arusini Kana; aliambatana naye katika njia ya mateso kuelekea
Kalvari; alibaki chini ya msalaba baada ya kusulibiwa Yesu; alipokea maiti ya mwanae
na kumzika; Maria aliyeshiriki nyakati za ukombozi; Maria aliyeambatana na Yesu katika
nyakati za Mungu kudhihirisha pendo la ukombozi; alistahili kushiriki utukufu wa Mwanae.
8.
Fundisho au tamko rasmi juu ya Bikira Maria kupalizwa mbinguni linasemaje? ·
Kutokana na sababu hizo za msingi na baada ya kupata ridhaa ya maaskofu Katoliki duniani
kote; ilimpendeza Mungu, Kanisa na wote wenye mapenzi mema, kuwa tamko rasmi litolewe. ·
Hivyo, saa 3 asubuhi, jumatano ya tarehe mosi Novemba, mwaka 1950; mbele ya maaskofu
700 na waamini takribani laki 6 hivi, askofu wa Roma, khalifa wa Kristo, mchungaji
mkuu wa duniani wa Kanisa Katoliki, Baba Mtakatifu Pio XII, alitoa tamko rasmi juu
ya Bikira Maria kupalizwa mbinguni mwili na roho.
· Papa Pio XII katika tukio
hilo, alisema: "kwa sababu hii, baada ya kumtolea Mungu sala na maombi ya kudumu,
na baada ya kuomba mwanga wa Roho wa kweli, tunataarifu, tunadhihirisha, tunaeleza
wazi kabisa na kutangaza kuwa; ni ufunuo wa imani, kwamba, Mama safi wa Mungu, Maria
Bikira daima, baada ya maisha yake hapa duniani, alipalizwa mbinguni mwili na roho
katika utukufu wa mbinguni.
9. Kuna tofauti gani kati ya kupaa na kupalizwa?
·Ni
muhimu kutofautisha hayo mawili. Yesu kwa kuwa yeye ni Mungu na hivyo alikuwa na nguvu
yake mwenyewe kurudi kwa Baba, alipaa mbinguni; bali, Bikira Maria (japo kuwa alijitahidi
kuishi katika neema) kama wanadamu wengine, hakuwa na uwezo wa kuelekea mbinguni-
hivyo alifika huko kwa kuwezeshwa na Mwanae Kristo; na huko ndiko kupalizwa mbinguni. ·
Kuhitimisha tafakari hii mambo mawili tunaalikwa kuyafanya: kufahamu faida za tukio
la Bikira Maria kupalizwa mbinguni na kubainisha sala ifaayo kumtolea Bikira Maria.
10.
Sherehe ya kupalizwa Bikira Maria inatufundisha nini: · kwanza, mwanadamu akishirikiana
na neema ya Mungu, anaweza kuishinda dhambi; anaweza kuyashinda mauti; · pili:
ni ishara ya matumaini kwetu- wanadamu tumeahidiwa kushiriki furaha na utukufu wa
Kristo mfufuka; siku moja tutashiriki utukufu wa Kristo; lakini, baada ya kustahimili
kwa imani, dhiki, mateso, madhulumu ya hapa duniani. · Tatu: Maria ni mwombezi
na mgawaji wa neema- kwani Maria ni mama wa msaada na huruma, na kazi yake ni kutuombea
ili stahili za Kristo zitufikie; dhambi zetu zisamehewe; na hatimaye tupate uzima
wa milele. · Nne Bikira Maria, kama mama yeyote mwema, yuko tayari kumsaidia yeyote
anayemkimbilia katika mahangaiko yake- kama tunavyosali katika sala ya memorare: "kumbuka
ee Bikira mpole sana, haijasikilika bado hata mara moja, kwamba ulimwacha mtu aliyeukimbilia
ulinzi wako, aliyeomba msaada wa maombezi yako”; je, tunamtumia kweli mwombezi huyu
mkuu? · Tuzidi kumwomba Bikira Maria mpalizwa mbinguni- ili tuweze kupata neema
ya ukombozi toka kwa Mwanae Kristo.
11. Kuna uhusiano gani kati ya Maria
Mpalizwa mbinguni na Wamisionari wa Damu Azizi ya Yesu? · Wamisionari wa Damu Azizi:-
Ni Shirika la mapadre na mabruda, lililoanzishwa na Padre wa Jimbo la Roma, Gaspari
del Bufalo, na alilianzisha rasmi katika tarehe 15 Agosti 1815 hivyo siku ya sherehe
ya Bikira Maria kupalizwa mbinguni. · Licha ya maisha yao kusimama juu ya nguzo
au mihimili mitatu, yaani, Tasaufi ya Damu, Maisha ya Jumuiya na utume; · Kutokana
na uhusiano wa Damu ya Yesu na Maria, wanamtambua Bikira Maria Mama wa Damu Azizi
kuwa msimamizi mkuu wa Shirika; · Na kutokana na mwanzilishi wao kuvutiwa na uinjilishaji
wa Mt. Fransis Ksaveri, basi wanamtambua Mt. Francisko Ksaveri kama msimamizi wa utume
wao.
12. Tasaufi na ibada kwa Damu Azizi ina maana gani? · Katika Kanisa,
kuna ibada nyingi, nzuri na takatifu. Kati ya hizo kuna moja ya pekee inayompendeza
Mungu, ndio ibada kwa damu ya Kristo. · Sisi tunaomfahamu na kumwadhimisha Bikira
Maria, Malkia wa mbingu, tunapaswa kumpenda na kuendeleza ibada hii ya thamani na
muhimu kwa wokovu wa roho zetu. · Tena kwetu, hili sio tu jambo jema, na wajibu
wetu kumtambua Kristo, ambaye kwa Damu yake iliyomwagika katuonesha pendo la pekee
la Baba wa mbinguni kwa mwanadamu. · Kwa sabau hiyo, ni kosa la aina gani tutakuwa
tumefanya kumsherehekea Maria pasipo kuikumbuka ibada kwa damu Azizi ya Yesu. Damu
ile ilitotoka kwa Maria, kwa mapendo ya kimama alimshibisha Yesu alipokuwa tumboni
mwa mamaye.
13. Ni kipi kielelezo cha uhusika wa Maria kwa Damu ya ukombozi? ·
Sala ya Wamisionari wa Damu Azizi kwa Maria Mama wa Damu Azizi ni kielelezo cha kutosha;
nayo inasema:
Tunakuheshimu Maria kwa kuwa Mungu amekuteua kati ya wanawake
wote kuwa Mama wa Mwanawe. Kwake yeye, wewe ni kalisi safi na takatifu, kwa kuwa kwa
njia yako ameiepusha dhambi ya asili, na pamoja nawe ameanzisha uumbaji mpya.
Unang’aa
na kuangaza kwa usafi wa moyo wako. Wewe ni tunda la kwanza la ukombozi, ulioustahili
kwa Damu ya Mwanao, hata kabla ya Yesu kuwa mtu ndani yako. Mungu amekutajirisha kwa
njia ya pekee, ili uweze kutekeleza mpango wake bila kikwazo. Hivyo ulimkubalia kuwa
Mama wa Mkombozi.
Bila kuweka masharti ulifuata hatua kwa hatua mapenzi ya
Mungu kwa imani isiyotikisika. Ilikuwa njia ya majaribu, ya matukio yasiyotazamiwa,
mwendo wa imani; hivyo ukajikuta mwenyewe juu mlima Kalvari, mbele ya Mwanao aliyetapakaa
Damu, baada ya kufuatana naye maishani, na katika njia yake ya kuelekea msalaba. Tunakupenda,
ewe Mama chini ya msalaba, Mama wa Damu Azizi, kwa sababu mlimani Kalvari ulikuwa
Mama yetu sote. Damu ya Yesu, iliyotoka kwako ulipompa mwili wa kibinadamu, ni damu
ya ukombozi inayotiririka kutoka msalabani; hivyo wewe, Mama wa mwili wa Kristo, pia
ni Mama wa Kanisa.
Tunatamani kukupenda wewe na Mwanao, na kukuheshimu kama
Mwanao alivyofanya katika maisha yake, alipokuwa mtoto na mtu mzima. Pamoja naye tunapenda
kushiriki maumivu yako na pia furaha zako. Mama, tuonyeshe namna tutakavyokupenda
zaidi na hata kujisikia wanao na kukamilika ndani mwako zaidi.
Kwa kuwa Yesu
alimwaga damu yake kwa ajili ya wote, hata moyo wako uko wazi kwa wenye matumaini,
kwa waliotengwa, waliokata tamaa na wasiopendwa.
Tunataka kujiunga nawe Mama
mwenye huruma kwa wote. Pamoja nawe twataka kutuliza na kusaidia binadamu, kwa kuwa
wewe uko karibu hata na wale wasiokufahamu au kukuelewa.
Kaa karibu nasi, Mama
wa Damu Azizi, ili tuwe karibu na hao unaowapenda sana. Tupatie imani yako, tukubali
kuongozwa na Roho Mtakatifu, kama ulivyofanya wewe. Utupatie unyenyekevu wako,
ili tuwatumikie wale ambao Yesu alikufa kwa ajili yao. Tujalie msalaba wako, ili tuweze
kuwa na huruma kama yako kwa wale wanaoishi bila neema.
Maria, Mama yetu, utusaidie
kuchukua nafasi yako katika dunia hii, ili Yesu zaidi na zaidi apate kuishi kati ya
watu na ufalme wake ukue. Utusaidie kufuata mfano wako ili tujitoe wenyewe pamoja
na Damu ya Kristo, kwa utukufu wa Mungu Baba na kwa wokovu wa ulimwengu mzima. Amina.
14.
Ulimwengu wa sanaa unawahusianisha vipi Bikira Maria, Yesu na Mt. Gaspari Del Bufalo? 14.1.
Mama Maria na Damu ya Ukombozi:
·Wachoraji mbali mbali wameonesha katika picha
zao namna wote wawili, yaani, Yesu na Maria wanavyochangia katika kikombe cha ukombozi. ·
Huko Bersanzone Italia, wanaiheshimu picha ambamo Maria anapokea katika chombo kichanya
cha zabibu; na huko Geneva- nchini bado Italia, wanaiheshimu picha inayomwonesha Maria
akimkabidhi Yesu zabibu. · Vielelezo hivi viwili, ni msaada mwingine kulielewa
na kulieleza fundisho juu ya Maria Mama wa Damu Azizi.
· Picha ile ya pili,
yaani, Maria kumkabidhi Yesu zabibu, inamkumbusha Yesu, jinsi mama yake alivyofanya
matone ya damu yatiririke. Matone hayo yatakusanywa katika kalisi; · Na katika
picha ya kwanza, Yesu anapomkabidhi mamaye zabibu, ishara ya kumwahidi Maria kuiweka
Ekaristi inayofichika katika maumbo ya divai.
14.2. Mama Maria na Gaspari
Del Bufalo: ·Huko Rimini, mji ulioko Italia, katika Madhabahu ya Malkia wa Huruma,
katika kikanisa kidogo cha Mt. Gaspari, kuna kielelezo kingine bayana. Maria anaoneshwa
akimkabidhi kalisi padre Gaspari, ili kumtia moyo aeneze ibada kwa Damu Azizi ya mwanae
Yesu; naye Gaspari, akijidhatiti katika utume huo, kiasi cha kuhitimisha maisha yake
katika miaka 51 tu, kwa kujituma katika kazi, akitolea uwezo na karama zake zote za
kipadre kwa Kristo na wale aliokabidhiwa na Kristo, hasa wanyonge na wagonjwa; Gaspari
alitoa maisha yake kama ishara ya kuungana na sadaka ya mwana wa Maria, sadaka ya
Kristo msalabani.
· Gaspari alipenda watu wote wamfuate Kristo; akithibitisha
kwa kwa kubeba katika safari za kuhubiri picha ya Mama aliyembeba mtoto mwenye kushika
kalisi na kwa kuamini kwa dhati kuwa damu ya Kristo ni silaha imara ya kuyashinda
mauti na nguvu zote za giza au kishetani; na katika hili alipata uthibitisho.
15.
Damu ya Kristo ina nguvu gani katika maisha ya watu? ·Licha ya miujiza mingi aliyoitenda
Mungu kupitia Gaspari Del Bufalo alipoomba kwa jina la Damu ya Kristo, mwaka 1836,
yaani mwaka mmoja kabla ya kufa kwake Gaspari Del Bufalo, mtawa mmoja wa kike, wa
monasteri ya Priverno ya huko Italia- alisumbuliwa na sauti zilizosikika daima katika
makazi yake. Gaspari alipokwenda kuhubiri katika mji huo, mtawa huyo alimwomba Gaspari
anyamazishe sauti hizo zinazomsumbua.
Naye Gaspari alimshauri aandike juu
ya mlango wake maneno yafuatayo: "Viva il divin Sangue", yaani: idumu au isifiwe Damu
Azizi; ndio maneno yaliyoonekana hata katika bendera aliyoibeba Gaspari alipokwenda
kuhubiri. Baada ya mtawa huyo kutekeleza alivyoelekezwa na Gaspari, kelele sumbufu
hazikusikika tena.
· Ni maneno hayo hayo, kwa amri ya Gaspari, kama zinavyoelekeza
kanuni za Wamisionari wa Damu Azizi, maneno hayo lazima yaandikwe juu ya milango ya
nyumba waishimo wamisionari wake; na yaandikwe juu ya milango ya wote wanaoiheshimu
Damu ya Kristo kama Damu ya ukombozi.
· Gaspari aliye mtume wa Damu, na kielelezo
cha heshima kwa Bikira Mpalizwa mbinguni, atuwashe kwa mapendo yale yaliyousukuma
moyo wake kuwaelekea Yesu na Maria,; yaliyomsukuma kuanzisha shirika la Wamisionari,
watakaohamasisha na kusambaza ibada kwa Damu Azizi.
16. Kwa nini Parokia ya
Kisasa-Medeli-Nzguguni ishangilie kwa namna ya pekee sikuu ya kupalizwa mbinguni? ·
Japokuwa parokia tajwa inajumuisha vigango vinne kwa sasa, yaani; cha Mt. Anna (Medeli),
cha Mt. Maria De Mathias (Nyumba 300), cha Mt. Paulo wa Msalaba (Nzuguni Maweni) na
cha Mt. Yohane Mbatizaji (Nzuguni Sokoine); Kigango cha Mt. Anna (Medeli) kinabeba
historia iliyopelekea maeneo ya Kisasa na Nzuguni kuteuliwa na kutangazwa Parokia
tena parokia yenye jina la Bikira Maria Mama wa Damu Azizi.
· Kigango cha Mt.
Maria De Mathias kimezaliwa wakati huduma za kichungaji eneo hilo zikitolewa tayari
na Wamisionari wa Damu Azizi ya Yesu mnamo 2010; vigango vya Mt. Anna, Mt. Paolo wa
Msalaba na Mt. Yohane Mbatizaji vilihudumiwa kwa miaka mingi na Parokia ya Kanisa
Kuu, kisha Parokia ya Kiwanja cha Ndege, na hatimaye Parokia ya Makole.
· Mwaka
2002, Wamisionari wa Damu Azizi walianzisha jumuiya yao Kisasa ili kuhudumia Radio
Mwangaza, Kijiji cha Matumaini na sehemu mbili zingine zilizotarajiwa kujengwa, yaani,
nyumba ya Makao yao Makuu Tanzania na kituo cha kiroho, kilichobadilishwa baadaye
kuwa kumbi za Mkutano na Hoteli ya Mt. Gaspari.
· Tangu wakati huo (2002) Wamisionari
wa Damu Azizi walioishi na kufanya kazi kisasa, wakitambua wajibu wao msingi ni uchungaji
wa roho, waliomba kibali toka parokia ya Makole kuhudimia kigango cha Medeli, huduma
iliyoendelea hadi 2007, mwaka ambao eneo lililoombwa kuhudumiwa likajumuisha Nzuguni
Maweni na Sokoine.
· Ujenzi wa nyumba 300 kwa ajili ya viongozi wa serikali
pamoja na uwepo wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) kulipelekea uwepo wa Waamini wanafunzi
na walimu wa chuo pia wafanyakazi wengine; ambao walianza kusali katika chapel ya
Kijiji cha Matumaini, kisha ibada za Jumapili kufanyika nje ya nyumba zao kwa zamu
na hatimaye kujenga Kanisa la kigango lililoanza kutumika mwaka 2011.
· Ikumbukwe
kuwa, mwaka 2008, Askofu Ruwaichi aliwaomba Wamisionari wa Damu Azizi kusimamia uchungaji
wa maeneo ya Kisasa-Medeli akitaja sababu za msingi za ombi hilo ikiwemo- wamisionari
hao wana nyumba Kisasa, kwamba Jimbo la Dodoma ndilo lililowapokea walipokuja Tanzania
mara ya kwanza hapo mwaka 1966 na kwamba hawakuwa na Parokia Dodoma.
· Ombi
hilo la mhashamu Askofu lilijibiwa kwa ujumla mwaka huo 2008 na kwa namna ya pekee,
mwaka 2010 wakipendekeza jina la parokia kumheshimu Maria, kwa namna anavyoheshimika
katika shirika lao, yaani, Maria Mama wa Damu Azizi. · Sambamba na Mhashamu Askofu
Ruwaichi kufurahia ukubali wa wamisionari hao, aliridhia Parokia hiyo kuwa chini ya
ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria wa Damu Azizi.
· Parokia ya Bikira Maria
Mtakatifu wa Damu Azizi (The Blessed Virgin Mary- Our Lady of the Precious Blood)
ilizaliwa rasmi hapo 2 Januari 2011, kwa mujibu wa Hati ya uzinduzi ya tarehe 1 Januari
2011 ya Mhashamu Askofu Jude Thaddeus S. Ruwaichi OFMCap, Msimamizi wa Kitume wa Jimbo
la Dodoma; alitoa tamko hilo kwa kuzingatia Mkusanyo wa Sheria za Kanisa na. 515:1&3
Sambamba
na tamko hilo, Mhashamu Askofu Ruwaichi alisema, mosi; Parokia hiyo ya Kisasa-Medeli,
itajumuisha maeneo yafuatavyo, ambayo yote yanamegwa kutoka Parokia ya Makole, nayo
ni: Kisasa, Medeli, Nzuguni Maweni na Nzuguni Sokoine; pili; Parokia ya Kisasa ni
sehemu ya Dekania ya Mt. Paulo wa Msalaba; na tatu; aliwaagiza wanaparokia wa Kisasa
kuzingatia: mosi, kuliheshimu agizo la Kristo la kupendana na kukuza umoja wa watoto
wa Mungu.
Pili, kujituma kwa kufanya juhudi za dhati zenye lengo la kurithisha,
kulea, kulinda na kuimarisha imani; tatu, kujitahidi kuela dhamiri na kujenga maadili
bora miongoni mwa waamini wa marika yote; nne, kushikamana na kujituma katika juhudi
za kuijenga parokia na kulitegemeza kanisa na utume wake mtakatifu; tano, kushirikiana
na wadau wote wa uinjilishaji, wakiwemo wenye daraja, watawa na walei; pia, kukuza
ushirikiano na ngazi nyingine za Kanisa kama vile Dekania, Vikarieti, Jimbo, nk; sita,
kukuza na kudumisha sauti ya unabii na ushuhuda unaowapasa kila mmoja binafsi na wote
kwa pamoja.
Makala hii imetayarishwa kutoka Radio Mwangaza FM Dodoma, Tanzania.