Baada ya miaka 22 ya sadaka na majitoleo, waamini wakamilisha ujenzi wa Kanisa!
Katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria kupalizwa mbinguni mwili na roho, hapo
tarehe 15 Agosti 2013 sanjari na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani nchini Burkina Faso,
Kanisa la Bikira Maria Mama Yetu wa Yagma, limetangazwa kuwa ni Kanisa kuu dogo.
Hayo
yamesemwa na Abate Narcisse Guigma, msimamizi mkuu wa Kanisa kuu dogo la Bikira Maria
Mama Yetu wa Yagma, katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Bikira Maria Kupalizwa mbinguni
ambayo kwa Mwaka 2013 yameongozwa na kauli mbiu "Pamoja na Bikira Maria, mfano bora
wa imani, tumshukuru Mungu aliyewainua wanyonge kutoka mavumbini".
Kanisa hili
limejengwa kwa mfano wa Madhabahu ya Bikira Maria wa Lourdes, Ufaransa, ili kutoa
heshima kwa Bikira Maria Mama wa Mungu na Kanisa. Jiwe la msingi wa ujenzi wa Kanisa
hili liliwekwa kunako mwaka 1978. Kutokana na sababu mbali mbali ujenzi huu ulicheleweshwa.
Kunako Mwaka 1991 wakati wa hija ya kichungaji ya Mwenyeheri Yohane Paulo II nchini
Burkina Faso, ujenzi wa Kanisa hili ukaanza kushika kasi. Kunako Mwaka 1998, Baraza
la Maaskofu Katoliki Burkina Faso likatangaza kwamba, Kanisa la Bikira Maria Mama
Yetu wa Yagma kuwa ni Madhabahu ya hija za kitaifa.
Ujenzi wa Kanisa hili
umedumu takribani miaka 22, lakini waamini hawakukata tamaa, bali waliendelea kuwa
na imani na matumaini kwamba, iko siku wangeweza kukamilisha ujenzi wa Kanisa hili
kwa heshima ya Bikira Maria Mama wa Mungu na Kanisa. Mradi huu mkubwa umegharimiwa
kwa asilimia 85% na mchango wa waamini na watu wenye mapenzi mema nchini Burkina Faso.
Waamini wakiamua kulitegemeza Kanisa wanaweza.
Kila mwaka, Mwezi Februari
ni kipindi cha hija za waamini kutoka Majimbo mbali mbali wanaokwenda kutoa heshima
kwa Bikira Maria Mama wa Mungu na Kanisa. Waamini kutoka nchi jirani wanahudhuria
pia, kilelezo cha mshikamano wa imani katika hija ya maisha ya Wakristo.