Mtakatifu Maximilian Maria Kolbe Padre na Shahidi wa Mwanga wa Imani
Mama Kanisa kila mwaka ifikapo tarehe 14 Agosti, anafanya kumbu kumbu ya Mtakatifu
Maximiliani Maria Kolbe, Padre na Mfia dini. Ni Padre aliyependa kwa dhati, akalimwilisha
pendo hili kwa matendo na katika ukweli kama Padre na shahidi wa mwanga angavu wa
imani inayomwilishwa katika matendo.
Ni shahidi aliyeongozwa na Mwanga wa
Kristo Mfufuka, kiasi cha kuyatoa maisha yake kwa ajili ya Mungu na jirani. Baba Mtakatifu
Francisko katika Waraka wake wa Kichungaji Lumen Fidei, Mwanga wa Imani anasema, huu
ni mwanga wenye nguvu na uwezo wa kumwangazia mwanadamu katika maisha yake yote, kwani
ni Mwanga unaobubujika kutoka kwa Mwenyezi Mungu, aliye hai, Mungu ambaye ni upendo
mkalimifu, unaomchangamotisha mwamini kujenga maisha thabiti.
Kanisa linaadhimisha
kumbu kumbu ya Mtakatifu Maximilian Maria Kolbe katika Mwaka wa Imani, ambao waamini
wanaalikwa kuishuhudia imani yao katika matendo, kwa kujiaminisha kwa Kristo aliyeyamimina
maisha yake kwa ajili ya kumkomboa mwanadamu kutoka katika lindi la dhambi na mauti,
kama kielelezo cha juu kabisa cha upendo wa Mungu kwa binadamu.
Kutokana na
ukweli huu, Baba Mtakatifu Francisko anasema, Msalaba ni kielelezo cha hali ya juu
kabisa cha Imani kwani unafumbata upendo wa Mungu, ushuhuda na tafakari ya kina, ili
kila mtu anayemwangalia Yesu pale Msalabani aweze kuamini na kuokoka.
Mtakatifu
Maximilian Maria Kolbe alizaliwa kunako mwaka 1894, akajiunga na Shirika la Ndugu
Wadogo wa Mtakatifu Francisko kama mtawa. Akakuza na kuimarisha Ibada kwa Bikira Maria
Mama wa Mungu na Kanisa, kiasi hata cha kuanzisha "Jeshi la Bikira Maria".
Ni
Padre aliyetekeleza utume wake kwa njia ya mahubiri ya kina yaliyokuwa yanabubujika
kutoka katika Neno la Mungu. Alikuwa ni mwandishi mahiri aliyetumia taaluma yake kuendeza
Habari Njema ya Wokovu na Kweli za Kiinjili. Alionesha ari na mwamko mkubwa wa shughuli
za kimissionari Barani Ulaya na Asia.
Wakati wa madhulumu ya Kinazi, alitupwa
kizuizini na kuonja mateso na madhulumu ya utawala wa kinazi kwenye kambi ya mateso
ya Auschwitz, wakati wa Vita Kuu ya Pili ya Dunia. Akiwa gerezani akaamua kutoa sadaka
ya maisha yake kama Padre ili kuokoa maisha ya Baba wa familia, aliyekuwa mwenza pale
gerezani, ushuhuda wa hali ya juu wa imani inayomwilishwa katika matendo. Akafariki
dunia kwa njaa hapo tarehe 14 Agosti 1945.
Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili
wakati akielezea sifa za Mtakatifu Maximilian Maria Kolbe alisema kwamba, ni msimamizi
wa hali tete katika karne hii. Mama Kanisa anapofanya kumbu kumbu ya Mtakatifu Maximilian
Maria Kolbe sanjari na Mwaka wa Imani anapenda kuweka mbele ya macho ya waamini matatizo
na changamoto zinazoendelea kumwandama mwanadamu katika nyakati hizi za utandawazi
na maendeleo ya sayansi na teknolojia.
Licha ya maendeleo makubwa katika sayansi
na teknolojia, lakini kutokana na utandawazi usiojali wala kuguswa na matatizo pamoja
na mahangaiko ya wengine, kama anavyosema Baba Mtakatifu Francisko, kuna mamillioni
ya watu wanaoteseka kutokana na balaa la njaa na utapiamlo duniani. Uchu wa mali na
madaraka ni kati ya mambo ambayo yameendelea kusababisha vita na madhulumu kwa watu
wasiokuwa na hatia, changamoto ya kusimama kidete kulinda na kutetea misingi ya haki,
amani na upatanisho wa kweli unaojikita katika toba na wongofu wa ndani.
Mtakatifu
Maximilian Maria Kolbe kwa ushuhuda wa maisha yake ni mwaliko kwa waamini na watu
wote wenye mapenzi mema kuthamini tunu ya uhai ambayo ni zawadi kubwa kutoka kwa Mwenyezi
Mungu na kwamba, waamini wajitahidi kujiandaa kwa ajili ya kukabiliana na Fumbo la
Kifo kwa: Sala, Tafakari ya Neno la Mungu linalomwilishwa katika matendo ya huruma.
Katika mwaka wa Imani, hii ndiyo imani katika matendo inayoongozwa na Mwanga wa Kristo
Mfufuka.
Tafakari hii imeandaliwa na Padre Richard Mjigwa, C.PP.S. Idhaa
ya Kiswahili ya Radio Vatican.