2013-08-13 07:55:08

Onesheni ukomavu wa kisiasa na kidemokrasia kwa kulinda na kudumisha amani na utulivu!


Baraza la Maaskofu Katoliki Zimbabwe linasema linaweza kusaidia upatikanaji wa suluhu ya amani na upatanisho miongoni mwa vyama vya kisiasa nchini Zimbabwe baada ya Chama cha upinzani cha MDC kukataa matokeo ya uchaguzi mkuu uliofanyika nchini Zimbabwe hivi karibuni na Rais Robert Mugabe wa Chama cha ZANU-PF akaibuka kidedea kwa kupata asilimia 62% ya kura halali zilizopigwa na mpinzani wake Morgan Tsvangirai kutoka Chama cha MDC akapata asilimia 34%. RealAudioMP3

Baraza la Maaskofu Katoliki Zimbabwe linawataka wanasiasa kuanzisha mchakato wa majadiliano ya amani na utulivu kwa ajili ya ustawi na mafao ya wananchi wa Zimbabwe ambao kwa miaka kadhaa kwa sasa wanateseka kutokana na kinzani za kisiasa nchini humo.

Padre Frederick Chiromba, Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Zimbabwe anasema, viongozi wa Makanisa nchini humo wanavitaka vyama vya siasa kuonesha uungwana kwa kutafuta suluhu ya kasoro zilizojitokeza kwenye uchaguzi mkuu kwa njia ya majadiliano, amani na utulivu.

Wananchi wa Zimbabwe wanahitaji mshikamano wa kidugu na umoja wa kitaifa ili kukabiliana na changamoto mbali mbali zinazoendelea kuwakabili. Inasikitisha kusikia kwamba, nchi nyingi zimeonesha kutoridhishwa na mchakato mzima wa uchaguzi mkuu nchini Zimbabwe, jambo ambalo linatia kichefuchefu kwa wananchi waliokuwa wana matumaini ya kuanza upya ujenzi wa nchi yao ambayo inaendelea kupitia hali ngumu ya maisha na vikwazo kwa kimataifa.

Watazamaji wa kimataifa wameitaka Serikali ya Zimbabwe kufanya uchunguzi wa kina ili kuweza kubainisha kasoro zilizojitokeza na kuchukua hatua madhubuti. Chama cha MDC kinachosema kwamba, kimedhulumiwa katika uchaguzi, kinapaswa kutumia njia halali kufikisha madai yake badala ya kufanya vurugu kwa maandamano mitaani yanayoweza kuvuruga amani na utulivu nchini Zimbabwe, kiasi kwamba, watu wakaendelea bado kugawanyika kwa misingi ya kisiasa.

Licha ya kasoro zinazozungumzwa katika mchakato wa uchaguzi nchini Zimbabwe, lakini jambo la msingi ambalo viongozi wa Makanisa wanapenda kuwashukuru wananchi wa Zimbabwe ni kufanya uchaguzi mkuu kwa njia ya amani na utulivu. Inasikitisha kuona kwamba, Zimbabwe bado inaendelea kutengwa na Jumuiya ya Kimataifa kutokana na kinzani za kisiasa, kwa wanasiasa kuendelea kutunishiana misuri!








All the contents on this site are copyrighted ©.