2013-08-13 10:42:02

Cheche za Neno la Mungu!


Wazee wanang'atuka.. !
Safari ya Waisrael kwenda nchi ya ahadi iliwachukua wana wa Israeli miaka 40. Musa alipewa kazi hiyo akiwa na umri mkubwa, takribani miaka 80. Yeye anawaambia wana wa Israeli ".. Nina miaka mia na ishirini.." (Kumb 31:2). Musa anang'atuka na kumuachia kijiti kijana mdogo Joshua. Hii ni sura njema ya wazee wenye busara na unyoofu wa kuruhusu wakati upeperushe mambo na vitu viende "to let it go.."
Somo la kwanza la Leo Augosti 13, 2013 kutoka kitabu cha Kumbu Kumbu ya Torati (Kumb 31:1- lataka kutuambia yafuatayo:
1. Ni wajibu kwa wazee kuwaandaa vijana kwa nafasi mbali mbali za uongozi katika jamii. Na sio tu kuwaandaa - bali kuwapa moyo, kuwajengea uwezo, kuwaamini na kuwaachia malengo na mikoba. Musa alikabidhiwa lengo la kuwafikisha wana wa Israeli nchi ya ahadi (kutoka 3:10). Na ndilo lengo la kudumu analomkabidhi kijana Joshua wakiwa mlima Nebo huku wakikabili bonde la Mto Yordani. Anamwambia kijana Yoshua, "..jipe moyo, Mungu ndiye atakayepigana vita badala yenu.." (Kumb 31:7).

2. Kwa wazee ye yote ni vizuri kujikubali kuwa muda wake umeisha. Kama umekwisha kula chumvi nyingi miaka 60 hadi 75, usipigane vikumbo na Vijana. Kuna heshima kubwa ya kujiondoa mapema madarakani. Ukijiondoa taratibu na kwa mpangilio utapata fursa ya kula pensheni yako vizuri na kwa utulivu. Kwa hili najua ni sawa “kumpigia mbuzi gitaa” tazama wapo wazee wanaoendelea kung’angania madarakani.

3. Mungu wetu hajafirisika kuwa na viongozi wapya, tena vijana. Mungu wetu ana kina Joshua, mwana wa Mzee Yese Daudi, Timoteo, Samueli na wengineo. Mungu pia anatumia hata watoto wadogo.
Somo letu la Injili siku ya leo linatupa picha ya Vizee ving'ang'anizi katika uongozi na madaraka. Wazee hawa hawapendi kuacha upepo wa nyakati, umri na damu changa uchukue nafasi yake. Wazee hawa huwa wanajiona kuwa wamezaliwa ili kutawala na hufanya kila liwezekanalo kuhatamia madaraka. Kristu anakemea na kuvunja kabisa roho hii ya kung'ang'ania madaraka. Anakachukua katoto kadogo na kukaweka kati yao (Matayo 18:6).
Yesu anataka kusema nasi hili katika siku hii :
1. Uongozi ni wa watu wote. Kuongoza ni kushirikishana na kuonesha dira - yaani, mbinu shirikishi itumike daima (participatory approach). Katika kushirikisha hata mtoto mdogo, maskini, mlalahoi, asiyesoma ana kitu cha kuchangia katika Jumuiya yetu kubwa. Maendeleo ni mchanyato wa mawazo, uzoefu, mang'amuzi na uelewa tofauti wa kila mwana jumuiya.

2. Tusiwakwaze wadogo na wa tabaka la chini kwa kuona wao kuwa wapo wapo tu. kwamba uwepo wao katika jumuiya au familia ni kutusindikiza tu sisi wenye majina. Wao nao pia ni sehemu muhimu ya muhimiri wa maamuzi yetu. Wao si wa kuburuzwa katika maamuzi - "pedagogy of the oppressed" Wadogo wo wote na wanyonge katika jamii daima huwa na moyo safi, na daima wanamwona Mungu katika unyonge wao (Matayo 5:8). Hivyo, tuwaogope na kuwaheshimu maskini na wasio na kitu katika jamii kwa vile wana watetezi muhimu mbinguni, yaani - malaika.

Tusali kwa ajili ya nchi yetu ya Tanzania ili michakato yote ya uongozi katika ngazi zote, na hasa ule wa 2015, utawaliwe na roho ya kushirikisha madaraka - na ikibidi waliokula chumvi nyingi wawe na unyenyekevu wa kama mzee Musa, wa kung'atuka kutoka madarakani.

Imeandaliwa na Padre Beno Kikudo, Jimbo kuu la Dar es Salaam.








All the contents on this site are copyrighted ©.