2013-08-12 08:32:25

Familia na changamoto zake katika ulimwengu wa utandawazi, sayansi na teknolojia!


Katika mwaka huu wa imani tunaalikwa kutafakari zaidi na zaidi kuhusu maisha ya familia kwani uhai wa familia ni uhai wa Kanisa na taifa zima la Mungu. Maisha ya familia ni zawadi kubwa ambayo Mungu ametujalia tangu pale alipoumba ulimwengu kwani yeye aliona kuwa “si vema huyu mtu awe peke yake, nitamfanyizia msaidizi wa kufanana naye” (Mwanzo 2:18). RealAudioMP3
Hapa tunaona hekima ya Mungu ya kumwumba mume na mke na kuwaambia kuwa “mwanaume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja” (Mwanzo 2:24). Tunaishi katika ulimwengu wenye changamoto nyingi ambazo tusipokuwa macho zinaweza kuhatarisha ule umoja kati ya mume na mke, umoja amboa Mwenyezi Mungu anatuambia kuwa “mwanadamu asiutenganishe” (Mk 10:9).
Tunapoendelea kutafakari kuhusu maisha ya familia na changamoto zake katika ulimwengu wa utandawazi, sayansi na teknolojia, leo hii ningependa tutafari pamoja kuhusu tatizo la kuvunjika kwa Agano la ndoa kati ya Mume na Mke katika jamii zetu. Jambo hili linaonekana kama kitu cha kawaida katika ulimwengu wetu wa leo.
Kadiri ya Mafundisho ya Kanisa ambayo msingi wake ni Maandiko Matakatifu kama tulivyoona, Agano la Ndoa Takatifu ambalo linatambulika na Kanisa kama Sakramenti linaweza kutenganishwa na Mungu pekee pale kinapotekea kifo cha mwenzi mmoja wapo. Hivyo basi, pale wenzi wawili(Mume na Mke) wanaposema kuwa wanapendana kwa dhati, upendo huo sio upendo wa majaribio bali ni upendo unaowaalika wapenzi hao wawili kila mmoja kujitoa kwa mwenzake mzima mzima bila kujibakisha.
Hii hali ya kijotoa kwa mwingine ni sadaka kubwa katika maisha kwani wapenzi hawa wanakubali kupokeana kama walivyo katika raha na taabu, maana yake wanakubali kusaidiana kuubeba msalaba wa maisha katika mazingira yoyote kwa lengo la kuupata utakatifu.
Bila shaka kila mmoja wetu anaweza kuonja madhara makubwa yanayoteka katika jamii pale wenzi wawili wanapotengana. Kwanza kabisa tunaweza kuonja mahagaiko wanayowapata wenzi hao, lakini madhara makubwa zaidi tunayouna mateso makubwa wanoyopata watoto kama wenzi hao walijaliwa zawadi hiyo kutoka kwa Mungu. Katika mazingira hayo, watoto wanashindwa kufurahia upendo wa Baba na Mama wakati wazazi wao bado wapo hai.
Wapendwa, binadamu sio wasisi wa Agano Takatifu la Ndoa bali ni Mungu peke yake. Mungu anatupatia zawadi ya maisha ya ndoa na akiwa na lengo la kututaka tutumie vizuri zawadi hiyo kusudi itusaidie kuupata Utakatifu na mwisho wa maisha yetu hapa duniani tuweze kuwa na muunganiko mkamilifu naye huko mbinguni.
Zawadi hii sio mali yetu na hatuwezi kufanikiwa kuiihishi kama zilivyo zawadi za miito mngine katika kanisa bila kuwa na ushirikiano mzuri na yule aliyetupatia zawadi hizo yaani Mungu. Ushirikiano na Mungu unafanyika katika maisha yetu ya kila siku pale tunapo shiriki kiaminifu katika kutafakari Neno la Mungu, maisha ya sala na Masakramenti ya Kanisa hasa Sakramenti ya Kitubio na Ekaristi Takatifu.
Leo hii tunaweza kujiuliza sisi wenyewe katika familia zetu; Ni wangapi kati yetu wana Maandiko Matakatifu nyumbani na ni wangapi angalu tunajitolea muda Fulani katika siku kumsikiliza Mungu anatueleza nini katika neno lake! Ni wangapi kati yetu tunafanya sala za familia nyumbani kwetu! Ni wangapi kati yetu tunajipatanisha na Mungu kwa Sakramenti ya kitubio pale tunapo tenda dhambi na kumpokea Yesu katika Ekaristi Takatifu!
Ndugu zangu wapendwa, tujaribu kujiuliza ni mambo gani katika ulimwengu wetu wa leo yanayokuwa kikwazo ya kutafuta muda wa kutafari uhusiano wetu na Mungu? Bila shaka kila mmoja wetu atakuwa na sababu zake. Mwaka huu wa imani tunaalikwa kutafari tena vikwazo vinayotuweka mbali na Mungu na kujiwekea mikakati ya mabadiliko ya kweli ya kutoka moyoni.
Katika maisha yetu tukumbuke kwamba, hakuna Agano la ndoa au agano lolote tunaloweka na Mungu linaloweza kusimama imara bila kuwa wanyenyekevu kwa Mungu na kumweka Mungu kuwa msimamizi mkuuu. Umoja katika maisha ya ndoa unapatikana pale wanandoa wanapokuwa na mapendo ya kweli kutoka moyoni, mapendo ambayo ni ishara ya uwepo wa Mungu aliye asili ya mapendo yote katika maisha ya binadamu . Kama Mungu hana nafasi katika mioyo yetu, kamwe hatuwezi kujua kupenda nini na hali hiyo pia ni mwanzo wa kuvunjika kwa ndoa zilizo nyingi au kuishi katika migogoro ya kila siku isiyokuwa na mwisho.
Kwa maombezi ya familia Takatifu ya Yesu Maria na Yosefu tuombe neema ya kutambua thamani ya Agano la ndoa na kuliishi Agano hilo mpaka kufa na pia Baraka za Mungu katika familia zetu kusudi tuweze kudumu katika imani, matumaini na mapendo. Amina
Kutoka Studio za Redio Vatican ni Mimi Padre Titus Nkane OSB.








All the contents on this site are copyrighted ©.