2013-08-10 12:17:37

Balozi wa Vatican nchini Benin aanza utume wake rasmi!


Askofu mkuu Brian Udaigwe, Balozi wa Vatican nchini Benin, hivi karibuni ameanza utume wake nchini Benin kwa kuwasilisha hati za utambulisho kwa Serikali ya Benin. Katika tukio hili, Askofu mkuu Udaigwe alipata fursa ya kubadilishana mawazo na viongozi wakuu wa Benin kuhusu hija ya kichungaji iliyofanywa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, wakati wa kuwasilisha matunda ya Maadhimisho ya Awamu ya Pili ya Sinodi ya Maaskofu wa Afrika.

Viongozi hao wameguswa kwa namna ya pekee na kipaumbele kinachoendelea kutolewa na Baba Mtakatifu Francisko kwa maskini na utunzaji bora wa mazingira. Askofu mkuu Udaigwe aliwasilisha salam na matashi mema kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko kwa Rais Thomas Boni Yayi wa Benin. Serikali inalishukuru Kanisa Katoliki katika mikakati inayopania kumwendeleza mtu mzima: kiroho na kimwili na kwa ajili ya mafao ya wananchi wa Benin katika ujumla wao.

Rais Thomas Boni Yayi anasema amekuwa ni Rais wa kwanza kutoka Afrika kuweza kukutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko mara tu baada ya kuchaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki. Kwa pamoja viongozi hawa wawili wameendelea kuhimiza umuhimu wa Jumuiya ya Kimataifa kushirikiana katika mchakato wa kudumisha misingi ya haki, amani, utulivu, maendeleo na mafao ya wengi.

Hivi karibuni Askofu mkuu Brian Udaigwe amepata fursa ya kukutana na kuzungumza na viongozi mbali mbali wa Kanisa na Kijamii nchini Benin pamoja na kuwasilisha hati za utambulisho kwa viongozi wa Kanisa kutoka kwa Kardinali Tarcisio Bertone, katibu mkuu wa Vatican.

Amepongeza ushuhuda na mwamko wa kimissionari uliooneshwa na Familia ya Mungu nchini Benin pamoja na wale waliofika nchini Benin kwa ajili ya kutangaza Habari Njema ya Wokovu. Wakavumilia taabu na mahangaiko mengi, lakini matunda ya utume wao yanaendelea kuchanua katika medani mbali mbali za maisha nchini Benin.







All the contents on this site are copyrighted ©.