2013-08-09 07:26:33

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya 19 ya Kipindi cha Mwaka C wa Kanisa


Tunakutana tena mpendwa msikilizaji wa Radio Vatican katika kipindi tushirikishane Neno la Mungu kila Dominika. Ni Dominika ya 19 ya mwaka C.RealAudioMP3

Mwaliko ni subira wakati tukitenda kazi kwa ukarimu na kwa furaha mpaka atakapokuja Bwana wa mavuno Bwana katika Injili anatufundisha kuwa tayari tukizitenda kazi zetu vema yaani tukitimiza mapenzi ya Mungu. Tunaalikwa daima kuwa watu wa kesha. Neno kesha haliondoi wajibu bali linatualika kubaki macho tukitenda jambo mwafaka kadiri ya mapenzi ya Mungu.

Mpendwa msikilizaji kumsubiria Bwana kwaweza kupelekea katika mawazo ya kutofanya kazi kama yalivyokuwa mawazo katika karne za kwanza za Kanisa, mawazo ambayo tunayapata hata katika Waraka wa Pili wa Mtakatifu Paulo kwa Watesalonike. Mara moja Paulo alikemea jambo hilo na kuwaonya wafanye kazi kwa ajili ya mkate wao wa kila siku. Ndiyo kusema hivi leo lazima kujibidiisha katika kuufanya ulimwengu uwe mahali pazuri pa kuishi na mahali ambapo utukufu wa Mungu unajidhihirisha wazi.

Katika kuwajibika katika ulimwengu huu lazima kuyatazama yaliyo ya juu yaani kutafuta kuokoa roho zetu. Katika kutawala ulimwengu huu Injili inatudai kuongoza vema mali ya mwenye mali, yaani mali na utajiri tuliokabidhiwa. Injili haidai faida bali inadai kutumia vema mali kwa ajili ya wale waliokuwa wategemezi wake!

Mpendwa mwana wa Mungu, tunapaswa kuiga mfano wa Mitume wakati wa mwujiza wa mikate jinsi ambavyo walijibidiisha kugawa chakula kwa walengwa wa Bwana. Huu ndio wajibu wa Kanisa kuhakikisha kila mmoja aliyemwana wa Mungu anapata habari njema itokayo katika Neno la Mungu. Neno la Mungu ndio mkate wa uzima na kwalo watu wapate uzima wa milele. Vivyo hivyo wazazi wanawajibika katika familia zao kutoa mkate wa kila siku katika nyanza zote mbili, kiroho na kimwili.

Mpendwa msikilizaji katika kutenda kazi ya Bwana tunapaswa pia kuzingatia moyo wa huduma na si hicho tunachokifanya, hapa ndo kuna Roho ya Injili ya Bwana. Tunasubiria ujio wa pili wakati tukijenga roho ya huduma na mapendo kwa wengine. Huo ndio utajiri wa kweli.

Mpendwa kuna jambo jingine muhimu ambalo yatupasa kulitafakari katika kusubiria na kutenda kazi zetu yafaa kupambanua wapi tunaweka moyo wetu. Daima Injili inasema kama mmoja akiweka akiba yake benki basi moyo wake waweza kulala pale na mwingine akiwekeza katika majengo na ardhi basi moyo huelekea huko! Basi Bwana atuonya kuchagua mahali ambapo roho yetu ikilala huko basi inahakika ya wokovu. Kusubiri kwetu lazima kukae katika kujenga furaha ya kimungu furaha itakayotupatia nafasi ya uzima wa milele.

Hatua nyingine ambayo tunapaswa kuitafakari ni hatua ya kifo. Injili haisemi juu ya kifo bali inazungumza juu ya Ujio wa Bwana. Kifo hatujui siku wala saa vivyo hivyo hatujui ujio wa Bwana ni lini! La msingi ni kujiandaa kwa ajili ya yote mawili. Kifo ni mlango wa kumwelekea Bwana, kama tutajiandaa na hivi tutaweza mapema kukabiliana na woga na hofu itujiayo mara tusikiapo kifo.

Tujiulize swali sasa kama Bwana angekuja sasa tungewasilisha nini mbele yake? Kaza moyo mwana wa Mungu katika kuhudumu taifa lake ambayo ndiyo zawadi yako kwake. Hata hivyo Bwana ni mwenye huruma atafunika mipasuko yetu, cha msingi tuishi maisha ya huduma kwa wengine. Tumsifu Yesu Kristo.

Tafakari hii imeletwa kwako na Padre Richard Tiganya, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.